Na Mwandishi Maalumu, Dar es Salaam
MKATABA kati ya Bodi ya Utalii Tanzania (TTB) na Kampuni ya
‘Sunderland Association Football Club’ ya nchini Uingereza ulioidhinishwa mwaka
2013/14, sasa unaitesa bodi hiyo ambayo
inadaiwa Sh. bilioni 3.7.
Deni hilo limetokana na matangazo ambayo kampuni hiyo
iliyatangaza kupitia michezo yake.
Akizungumza jana jijini Dar es Salaam wakati akizindua bodi
mpya ya Wakurugenzi wa TTB, Waziri wa Maliasili na Utalii, Profesa Jumanne
Maghembe (Pichani) alisema mkataba huo ni wa hovyo na sasa unaligharimu Taifa.
“Tunadaiwa kwa kuingia mikataba ya hovyo, Mkurugenzi aliyekuwepo
wakati ule alikataa kuupitisha matokeo yake akafukuzwa kazi, sijui wengine
ilikuwaje wakaupitisha na tunapolipa hili deni nadhani kuna mtu anafaidika nalo
hapa nchini.
“Sasa kazi ya Mwenyekiti wa Bodi (Jaji Mstaafu Thomasi
Mihayo) ni kututoa hapa tulipo na kuhakikisha kuwa haturudi tena huko. Naiomba
bodi hii isije ikakubali kuingia katika mtego wa namna kama hiyo, tumepelekwa
mahakamani… tumeshikwa pabaya na lazima tuwalipe sunderland fedha zao,”
alisema.
Waziri Maghembe aliitaka bodi hiyo kuhakikisha kuwa
inatelekeza majukumu yake ipasavyo ikiwa ni pamoja na kutangaza vivutio vyote vya
utalii vilivyoko nchini ili kuongeza idadi ya watalii.
“Andikeni makala pelekeni kwenye mashirika ya ndege watu
watazisoma, msikae ofisini nendeni kule viliko , sekta hii ni kubwa mno kwa
sasa inachangia asilimia 17 kwenye pato la Taifa tunahitaji ifike asilimia 30
ifikapo 2018,” alisema.
Aliwataka kutafuta soko la utalii nchini Urusi na
kuimarisha lile la Marekani.
“Nendeni Urusi kutafuta soko si kufanya ‘shopping’ warusi
wale wana fedha nyingi na sisi tunahitaji fedha. Najua kuna wakurugenzi watatu
wa kitengo cha ugavi, utafiti na sheria wameacha kazi kutokana na kwamba
mnaidai serikali, tunajua tutashughulikia.
“Lakini naomba mfanye kazi, tuna vivutio vingi ambavyo
hatujavitangaza vema matokeo yake Kenya wanatangaza vingine vipo kwao,
tusikubali, lazima muongeze idadi ya watalii kutoka milioni moja iliyoko sasa
hadi milioni tatu, nitawapima kwa kazi mkishindwa nitawaondoa wote,” alisema.
Naye Mwenyekiti wa Bodi hiyo, Jaji Mstaafu Mihayo (aliyesimama) alimuomba
Waziri Maghembe kuisaidia bodi hiyo kwa kulipa madeni ya wafanyakazi yanayotokana
na marupurupu yaliyofikia Sh milioni 300.96.
“Viwango vya mishahara havilingani na sekta hii, naomba
hilo ulitazame na kutusaidia kulitatua ili watendaji wetu wapate hari ya
kufanya kazi na hatutaiangusha serikali,” alisema.
Chapisha Maoni