NA VERONICA ROMWALD – DAR ES SALAAM
TAASISI ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) inatarajia
kufanya uchunguzi wa kupima magonjwa ya moyo kwa ujauzito unaoanzia wiki 18.
Uchunguzi huo utafanyika hospitalini hapo kwa muda wa
siku tatu kuanzia Oktoba 12 hadi 14, mwaka huu.
Mkuu wa Kitengo cha
Mawasiliano wa JKCI, Maulid Kikondo amesema uchunguzi huo utafanyika bure.
“Tumegundua watoto wengi wanazaliwa na magonjwa ya
moyo lakini upo utaalamu ambao wenzetu wamekuwa wakiutumia wa kupima ujauzito
ukiwa na wiki 18 na kuendelea ambapo huweza kubaini mapema iwapo mtoto aliyeko
tumboni ana matatizo au la.
“Sasa mwenzetu Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo kwa
Watoto, Naiz Majani alikwenda nje ya nchi na akapata mafunzo, amerudi hivyo tutaanza
kuwachunguza wajawazito,” amesema.
Amesema uchunguzi huo utafanywa kwa kutumia kifaa maalumu
kiitwacho kitaalamu Fetal Echo-cardiology .
Amesema hawajaweka idadi maalumu ya wajawazito
wanaotarajia kuwapima kwa kutumia kifaa hicho na kwamba wanawasihi wafike kwa
muda uliopangwa.
“Kila atakayekuja atahudumiwa, mtoto anapogundulika
kuwa na tatizo ni rahisi kutibiwa punde tu anapozaliwa na kuwa na afya njema akafurahia
maisha kuliko akizaliwa na baadaye kugundulika kwani matibabu yake yanachukua
muda ikizingatiwa wengi huletwa wakiwa wamechelewa,” amesema.
Mkurugenzi wa JKCI, Profesa Mohamed Janabi akiwa na Balozi wa China - Tanzania, Dk. Lu Youqing, China ndiyo waliosaidia ujenzi wa JKCI
Kikondo alisema pamoja na hilo, Oktoba 9 hadi 16,
mwaka huu wataendesha kambi nyingine ya upasuaji kwa watoto 30 wenye magonjwa
hayo.
“Madaktari wa JKCI watafanya upasuaji huo kwa
kushirikiana na madaktari wenzao kutoka Addis Ababa wa hospitali ya Al
muntada,” amesema.
Chapisha Maoni