Matumla akizungumza na mmoja wa madaktari waliomtibu katika Taasisi ya Tiba ya Mifupa na Mishipa ya Fahamu (MOI) kabla ya kuruhusiwa kurudi nyumbani mapema wiki hii.
NA VERONICA ROMWALD – DAR ES SALAAM
BONDIA Mohamed Matumla (30) aliyekuwa amelazwa
katika Taasisi ya Tiba ya Mifupa na Mishipa ya Fahamu (MOI), ameruhusiwa kurudi
nyumbani.
Akizungumza na MTANZANIA jana, Ofisa Uhusiano wa
MOI, Patrick Mvungi alisema Matumla aliruhusiwa jana na madaktari wake ambao
walijiridhisha maendeleo ya afya yake kuwa ni mazuri.
“Tunapenda kuwaarifu wanamichezo wote hususani
wapenzi wa Mchezo wa Ngumi Tanzania kwamba tumemruhusu Matumla kwenda nyumbani.
Tumejiridhisha kwamba afya yake imetengamaa vizuri,” alisema.
Mvungi alisema wataendelea kumfuatilia kama
mgonjwa wa nje (Out patient) kwenye kliniki zao.
“Hivyo tuendelee kumuombea ili Afya yake iendelee
kuimarika zaidi,” aliongeza.
Bondia huyo hivi karibuni alifanyiwa upasuaji mkubwa
wa ubongo kuondoa damu iliyokuwa imevilia ndani ya kichwa chake.
Alipatwa na hali hiyo baada ya kupigwa ngumi kichwani na
bondia mwenzake, Mfaume Mfaume katika raundi ya saba katika pambano lisilo la
ubingwa lililofanyika hivi karibuni, jijni Dar es Salaam.
Kaimu Mkurugenzi wa MOI, Dk. Othuman Kiloloma alisema,
Matumla atalazimika kukaa nje ya ulingo kwa kipindi cha miezi minane hadi 12
baada ya kufanyiwa matibabu.
Alisema atarejea ulingoni baada ya kuisha kwa muda huo hata
hivyo atalazimika pia kupta kibali cha daktari.
“Matumla atalazimika pia kuvaa kofia ngumu maalumu (helment)
kichwani ili kuzuia eneo ambalo tulifumua ili kuondoa damu iliyoingia ndani ya
ubongo lisije likapata madhara akiwa ulingoni,” alisema.
Chapisha Maoni