WAPO ndugu, jamaa na rafiki zetu ambao hudai kuwa huwa
wanakosa kabisa usingizi wakati watu wengine wakiwa wamelala hasa nyakati za
usiku.
Kuna ambao hudai hali hiyo huwatokea mara nyingi na sasa
wameizoea kabisa hali hiyo na kuiona ni ya kawaida kabisa kwao.
Ingawa wapo ambao hutafuta msaada lakini wengi hukosea
kwani huishia kwenda katika maduka ya dawa na kununua dawa za kuwasaidia na wao
waweze kupata usingizi.
Hatua hiyo huwaweka katika hatari ya kupata matatizo mengi
zaidi pasipo kujua kwamba kukosa usingizi pekee ni tatizo linalohitaji ufumbuzi
tena wa haraka.
Daktari Bingwa wa Afya na Magonjwa ya Akili wa Hospitali ya
Taifa Muhimbili (MNH), Said Bakari anasema kukosa usingizi ni tatizo ambalo
baadae huathiri afya ya akili.
“Wengi hawajui jambo hili, kuna watu wenyewe hupenda ama
kuonanekana wanajua sana kufanya kazi ofisini, hawana muda wa kupumzika kila
wakati wanafanya kazi hawana muda wa kupumzika kabisa, wanapaswa kujua kwamba
kufanya hivyo kunawaweka kwenye hatari ya kuathirika afya ya akili,” anasema.
Daktari huyo anasema watu wanapaswa kujua kwamba ubongo na
akili navyo huhitaji kupumzika kama ilivyo kwa viungo vingine vya mwili wa
binadamu.
“Mtu akifanya kazi nyingi pasipo kupumzika na akakosa
usingizi baadae hali hiyo humsababishia kushindwa kufanya kazi kwa ufanisi na
hivyo kujikuta akiharibu kazi ofisini kwake,” anasema.
Anaongeza “Aliyekosa usingizi hataonesha dalili sawa na
yule aliyeanza kutembea barabarani, kwamba ataanza kuleta vurugu, watu wataona
kiwango chake cha kufanya kazi kinashuka,” anasema.
Anasema wapo pia ambao hupata maumivu makali ya kichwa,
hushindwa kuona vema na hata kupooza mwili.
“Unakuta mtu analalamika anasumbuliwa na maumivu ya kichwa
mwaka wa pili kwa mfano akipimwa hakuna ugonjwa anaokutwa nao au haoni na
akipimwa macho hayana tatizo, wengine walalamika tumbo linauma lakini wakipimwa
pia hakuna matatizo. Akili ikipata mshtuko husababisha matatizo makubwa,”
anasema.
Anasema wengine hupata matatizo ya akili kutokana na
matatizo ya kifamilia.
“Unakuta mama na baba hawaelewani kwa kipindi cha muda
mrefu baadae hali hiyo huweza kusababisha matatizo ya akili hata kwa watoto
wao,” anasema.
Dalili
Anasema mtu mwenye matatizo ya akili mara nyingi huonekana
kuwa na mawazo ambayo huwa hayapo katika hali ya uhalisia.
“Yaani ile ‘thinking capacity’ yake au na imani yake
inakuwa imetoka kabisa nje ya uhalisia, kwa mfano unasikia wote tunajua sisi ni
binadamu na si Mungu na tunaamini kwamba Mungu yupo lakini anakuja mtu na
kuanza kusema yeye ni Mungu na anasimama na msimamo wake huo.
“Unakuta anaanza kufanya vitu anavyodhani ni vya kimungu anapoulizwa
ametoa wapi anatoa utetezi ambao mkiutazama mnaona kabisa anakabiliwa na tatizo
la akili,” anasema.
Anaongeza “Wakati mwingine hutokea mtu na kudai wanadamu
wote ni wake, yupo mmoja ambaye alitueleza karibu watoto wote wa Tanzania ni wa
kwake na anao wengine wengi Marekani, alisema amezaa na rais mmoja mkubwa
duniani na kwamba hakuna mtu atakayemuambia amuelewe lolote, sisi tulijua moja
kwa moja hilo ni tatizo la akili.
Anasema wapo pia ambao hujikuta wakisema magari yote
yaliyopo jijini Dar es Salaam ni ya kwao na iwapo ikatokea akaingia katika gari
la mtu huishia kuambulia kipigo.
“Wanapigwa mno wapo wengine wanakamatwa hadi ikulu na
wengine wanazuka tu huko barabarani na kuanza kuwafanyia maombezi watu
wanaopita barabarani,” anasema.
Anasema watu waliopata tatizo la akili huhisi vitu ambavyo
havipo katika hali ya uhalisia.
“Tunajua kuna njia tano za utambui, kugusa, kunusa, kuonja,
kuona na kusikia lakini watu walio katika hali ya kuchanganyikiwa huwa
wanahisi, vitu ambavyo havipo.
“Kwa mfano anaweza kuona watu wameshika silaha na
mkimuuliza wapo wapi hao watu, mtamuona anawashangaa ninyi kwanini hamuwaoni, wakati
mwingine wanaweza kusikia sauti ambazo nyie mliomzunguka hamzisikii kabisa,”
anasema.
Anaongeza “Wengine hudai wamerogwa, ni imani ambayo ipo
kwenye jamii zetu, wakati mwingine mtu mwenye tatizo la akili anaweza kudai
amerogwa na kuwataja hao waliomroga, sasa ikiwa ni watu wa karibu yake, matokeo
yake huishia kuzua ugomvo kwenye jamii na familia husika.
“Ndugu wanaposhtuka na kumleta hospitalini hugundulika kuwa
hakurogwa bali alikuwa anasumbuliwa na tatizo la akili, basi hapo amani na
furaha hurejea katika familia,” anasema.
Anaongeza “Wapo wengine huletwa wanadai kuwa wanasikia vitu
au nyoka wanatembea ndani, tumboni. Yaani huwa wanakuwa na hisia potofu ambazo
wakati mwingine humsababishia hofu kubwa na kuhisi kuwa hawapo salama.
“Ndipo pale unakuta mtu anashinda amejifungia ndani tu,
anashindwa kwenda kazini au hata sokoni na wapo ambao hufikia hatua ya kuacha
kazi kabisa.
“Unakuta kwanza anahama ofisi moja anakwenda nyingine
ambako hadumu, anahama tena, yaani anaweza kuhama ofisi hata 10 na baadae
anaamua kukaa nyumbani, kwa sababu, kwa mfano anakuwa analalamika kila akitoka
anakuwa analalamika kuona watu wanaomfuata wakiwa wameshika silaha lakini nyie
mkiangalia watu hao hamuwaoni,” anasema.
Anasema kukosa usingizi ni sababu kubwa ya maradhi ya akili
kwani husababisha kutetereka afya ya akili kwa haraka.
Madhara
Anasema iwapo mtu hatawahi hospitalini kupata tiba tatizo
hilo huanza kumuathiri yeye mwenyewe.
“Kwa sababu hushusha kiwango chake cha kufanya kazi kama
awali hivyo uchumi wake utatetereka na jamii yake nayo huathirika maana
hulazimu watu kuwa karibu naye wakimuhudumia.
“Afya ya mwili wake nayo hutetereka kwani kinga zake
hushuka kwa kiwango kikubwa, magonjwa haya huleta matatizo pia kwenye ndoa nyingi
na mwisho husababisha vifo,” anasema.
Yanatibika
Daktari huyo anasema magonjwa hayo yanatibika kama maradhi
mengine ingawa yapo machache ambayo hayatibiki.
“Huwa tunatumia dawa kutibu maradhi haya lakini kama
yametokana na hitilafu za kemikali (ya kurithi) huwa hayatibiki ingawa zipo
dawa zinazosaidia kurekebisha kemikali hizo,” anasema.
Anasema huwa pia watumia njia ya ushauri wa kisaikolojia na
matibabu ya jamii.
“Tunaposema matibabu ya kijamii tunamaanisha kwamba huwa
tunaipa elimu jamii inayomzunguka mgonjwa, kwamba wasimtenge kwa hali aliyonayo
maana hiyo itamfanya kuwa mpweke kama wanaandaa kikao kwa mfano basi na yeye
ashirikishwe na akitoa maoni yapokelewe na ikiwezekana wampongeze.
“Ile inamsaidia kuona kwamba naye anathaminiwa lakini si
kumkejeli na kumtamkia maneno ambayo ni ya kuudhi mfano kumuita kichaa au chizi
si sahihi, huku ni kumnyanyapaa, huwa pia tunawapa matibabu ya kazi,” anasema.
Makala haya kwa mara ya kwanza yalitoka Februari, mwaka huu katika gazeti la MTANZANIA
Chapisha Maoni