Recent Post


 


moja

Responsive Advertisement

http://photos.demandstudios.com/getty/article/220/191/sb10062916b-001_XS.jpgMara nyingi watoto wenye tatizo hili, huwa waharibifu na hawapendi kujifunza, Picha na Mtandano

NA VERONICA ROMWALD – DAR ES SALAAM

TANGU mimba inapotungwa tumboni mwa mama hadi mtoto anazaliwa baada ya miezi tisa kipindi chote hicho mtoto huwa katika hali ya uchangamfu.

Hiyo ni kwa sababu binadamu ameumbwa kuchangamka, wakati wa ujauzito, mama huhisi hali hiyo ya uchangamfu wa mtoto tumboni mwake.

Mtoto akiwa tumboni mwa mama yake, mama huweza kuhisi vema namna ambavyo mtoto husogea au kugeuka kutoka upande mmoja hadi mwingine na hata kuzunguka zunguka.

Mtaalamu wa Tiba ya Mazoezi katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Rosemary Kauzeni anasema Hiyo ni hali ya kawaida ambayo hudumu kwa kipindi chote cha ujauzito.

“Wakina mama ambao tayari wamepitia hali ya ujauzito na kubahatika kujifungua wanaelewa vema jinsi hali hii inavyokuwa, kuna wakati huweza kuhisi kabisa mtoto akiwa amelala upande mmoja baadae anahamia upande wa pili au anacheza cheza tumboni,” anabainisha.

Baada ya kuzaliwa

Mtaalamu huyo anasema kisayansi kuna uchangamfu ambao umeainishwa unaoashiria uchangamfu wa mtoto baada ya kuzaliwa.

“Mtoto anapozaliwa anaanza kujifunza kazi mbalimbali, kazi yake ya kwanza ambayo anajifunza ni kunyonya… hakuna mtu anayemfundisha mtoto kunyonya hata siku moja,” anasema.

Anataja kazi zingine ambazo mtoto hujifunza mwenyewe kuzifanya pasipo kufundishwa na mtu ni kurusha mikono na miguu yake.

“Hii ni hatua ya kwanza ya uchangamfu wa mtoto ambao tunaouona mara tu anapozaliwa, hatua ya pili tunaouona ni uchangamfu wa lugha,” anasema.

Anafafanua “Lugha ya mtoto mchanga ni kulia, akizaliwa tu iwe kwa njia ya kawaida au ya upasuaji tunahitaji kuuona uchangamfu huu, mara nyingi mtoto huwa anawasiliana kwa njia ya kilio.

Wakati wa ukuaji

Anasema  baada ya kuzaliwa mtoto huendelea kuonesha uchangamfu wa aina mbalimbali hadi kipindi cha miezi mitatu.

“Katika kipindi hicho mtoto huonesha uchangamfu mwingi ambao mama huuona kadri siku zinavyozidi kusonga mbele, kwa mfano mtoto huonesha uchangamfu wa kuzungusha macho, usikivu wake, hisia za kugusa,” anasema.

Dk. Kauzeni (pichani) anasema jinsi mtoto anavyozidi kukua mama huona uchangamfu wake katika kusogea hasa anapokuwa akijirusha rusha au kusogeza miguu yake.

“Uchangamfu zaidi huonekana hasa anapofikisha wiki nne tangu alipozaliwa, hapo mama anaweza kuona mtoto wake akianza kucheka, akisikia sauti mbalimbali anaweza hata kutoa hisia ya kufurahi,” anasema.

Anaongeza “Anapofikisha umri wa miezi mitatu shingo ya mtoto hukaza vizuri zaidi, uchangamfu huendelea kubadilika badilika kadiri anavyokua.

“Kimsingi tangu mwaka sifuri hadi miezi mitatu mtoto huwa anacheza mwili mzima, lakini anapofikisha miezi mitatu shingo yake hukaza.

“Hapo utaona uchangamfu wake ukiwa umebakia kwenye kiwili wili, sehemu ya tumbo na mgongo huonekana ikicheza zaidi, au utaona mikono na miguu ikiwa haijakaza vizuri,” anasema.

Anasema hali hiyo huendelea hadi anapofikia umri wa miezi minne na kwamba katika kipindi hicho mama huona uchangamfu wa mtoto kukaa na au kuanza kutumia zaidi mikono yake.

“Huanza kushika vitu mbalimbali anavyoviona mbele yake, husikilizana na watu wanaomzunguka na sauti anazozisikia, huu ni uchangamfu wa kawaida ambao hutegemea makuzi salama,” anasema.

Anaongeza “Mtoto atakua katika hali hiyo hadi kipindi cha miezi mitano hadi sita ambapo huanza kujivuta kusogea kutoka eneo moja hadi jingine.

Tatizo huanzia wapi?

Mtaalamu huyo ambaye pia ni Mkuu wa Idara ya Utengamao na Tiba hospitalini hapo, anasema iwapo mtoto anakabiliwa na tatizo la haraka nyingi huonesha uchangamfu usio wa kawaida.

“Dalili huanza kuonekana hasa katika kipindi ambacho huanza kukaa chini au kutembea, huwa anakuwa na kasi isiyokuwa ya kawaida,” anabainisha.

Anasema mara nyingi mtoto mwenye tatizo hilo anapowekwa chini huanza kuvamia vitu mbalimbali anavyoviona mbele yake.

“Kutokana na hali hiyo wengi huwa ni lazima washikiliwe na mtu, au unakuta ameanza kutembea na kasi yake huwa kubwa kuliko kawaida ya umri wake, hapo utasikia wazazi wengi wakisema mtoto ni mtundu mno,” anasema.

Anasema huwa hawataki kushika kitu chochote kwenye mikono yao, wakishika wanatupa hata wakipewa maagizo hawatekelezi (hawafuati oda ya mzazi).

Anaongeza “Hata akiwa anacheza na wenzake hawezi kufuata zile taratibu za mchezo na wenzake ili kucheza pamoja, ni vigumu kushirikiana na wenzao ingawa wanaongea, wanatembea  kama watoto wengine.

Anasema ingawa kwa hali ya kawaida tatizo hilo si ugonjwa lakini huweza kumsababisha mtoto kupata magonjwa  mbalimbali yatakayoathiri afya yake baadae katika maisha yake.

Magonjwa yenyewe

Mtaalamu huyo anasema mtoto mwenye tatizo hilo huwa kwenye hatari kubwa ya kuathirika afya ya ubongo na baadae kupata magonjwa ya akili (mood dis-order).

“Yaani anakuwa hisia zake zinabadilika badilika, mara mwenye hasira nyingi, mara furaha, hali hiyo huweza kumpelekea ubongo wake kuathirika na kumsababishia magonjwa ya akili,” anabainisha.

Anasema hali huweza kuwa mbaya zaidi na hata kupeleka mtoto kupata ugonjwa wa kifafa baadae.

Anasema kutokana na hali hiyo hulazimu wazazi, ndugu au familia kutumia muda na akili yao yote kumwangalia mtoto kwa umakini mkubwa.

Daktari huyo akionesha baadhi ya vifaa wanavyotumia kuwatibu watoto wenye tatizo la haraka nyingi

Matendo yasiyo ya kibinadamu

Anasema kwa kawaida mtoto anapokuwa hutakiwa kuonesha matendo ya kibinadamu lakini yule mwenye tatizo huonesha matendo yasiyo ya kibinadamu.

“Mtoto anapokuwa na umri wa mwaka mmoja huwa anachezea au kuunganisha vitu mbalimbali unavyompatia lakini mtoto mwenye tatizo hili kamwe hawezi kutulia na kuchezea vitu unavyompatia.

“Utaona chochote unachompatia anakitupa ovyo, maana yake ni kwamba anakuwa haoneshi ufundi hata kidogo ambao tunautarajia. Kwa kawaida mtoto tunarajia ajifunze kwa mfano mara nyingi mtoto wa kiume akiona gari achukue chochote kilichopo mbele yake na kuanza kukisogeza kama gari linavyokwenda.

“Akiwa mtoto wa kike akikaa karibu na mama au dada yake wakati wa kupika chakula jikoni, utaona na yeye anachukua vikopo na kukaa chini akiigiza anapika,” anasema.

Anaongeza “Mtoto mwenye haraka nyingi hana huo muda wa kujifunza, yeye hufanya matendo ya vurugu tu, wengi wanawaita watundu ingawa si neno zuri kulitumia.

Anasisitiza kwamba mtoto ambaye hana tatizo huonesha ufundi wake kwani hutulia na kunuia kutazama  kile anachotaka kukitazama.

Namna linavyotokea

Mtaalamu huyo anasema kila binadamu ana milango ya fahamu ambapo mtoto mwenye tatizo la haraka nyingi, mara nyingi huwa anakuwa na milango ya fahamu isiyo wiana.

“Yaani… tunatumia macho kutazama kitu na kupeleka taarifa kwenye ubongo ambao hutafsiri kitu tunachokiangalia, ukigusa kitu taarifa hupelekwa kwenye ubongo na wenyewe hutafsiri umegusa nini.

“Ukinusa harufu yoyote nayo ni hivyo hivyo, na mwili nao hupeleka taarifa kwenye ubongo kwa mfano ukiwa ukitaka kupanda ngazi unapeleka taarifa kwenye ubongo na ndipo pale unajikuta unainua mguu wako,” anasema.

Anaongeza “Mtoto mwenye tatizo upo uwezekano mkubwa kwamba kuna shida ya mawasiliano katika mwili wake, lakini kwa bahati mbaya hakuna kipimo tunaweza kukitumia kubaini tatizo hili mapema, tutakachokiona ni ule uharaka wa kupindukia kutokana na haraka ya kupindukia.

Athari zaidi

Anasema kutokana na tatizo hilo kumekuwa na ajali nyingi za moto kwa watoto.

“Unakuta mama ameinjika maji jikoni au ameweka chupa ya chai mezani ghafla anakuta mtoto ameshafika, ameshavunja na tayari ameungua,” anasema.

Anafafanua “Yaani ukimuweka chini haraka anakuwa amevamia kitu, ni lazima ashikiliwe, katika hilo lazima uanze kuwa na wasiwasi wa uchangamfu wa mtoto huyo.

Anasema kutokana na hali hiyo hulazimu wazazi, ndugu au familia kutumia muda na akili yao yote kumwangalia mtoto kwa umakini mkubwa.

Hali ipoje

Anasema ingawa bado hakuna utafiti uliofanywa kubaini ukubwa wa tatizo hilo nchini lakini katika Idara hiyo wamekuwa wakipokea watoto wenye tatizo hilo.

“Kwa mfano mwaka 2012 tulipokea watoto 32 katika kipindi cha miezi mitatu ambao walikuwa wameungua moto na tulipozungumza na wazazi wao wengi walidai watoto wao ni watundu sawa na asilimia 10 (si taarifa rasmi),” anasema.

Anasema watoto wengi hufariki dunia kwa kutumbukia kwenye maji, wapo ambao hushindwa kumudu masomo darasani.

“Tunapokea watoto wengi ambao wanakataliwa shuleni kwa sababu wana tatizo hili la haraka nyingi. Hawa si ‘slow learners’… hawa ingawa wana akili nyingi mno lakini wanashindwa kujifunza kwa sababu ubongo wao upo haraka,” anasema.

Anasema kutokana na hali hiyo anakusudia kufanya utafiti wa kina kuhusu tatizo hilo kwamba lipo kwa kiasi gani nchini.

Sehemu ambayo madaktari hutumia pia kuwatibu watoto wenye tatizo la haraka  nyingi

Matibabu

Anasema kwa kuwa si ugonjwa ambao huonekana wazazi wengi hubaki na watoto wao nyumbani wakidhani ni hali ya kawaida.

“Si rahisi kubaini kwa sababu saa zote mtoto huwa ‘active’ ingawa wanaweza kuonesha dalili kwa mfano kukosa usingizi, kukosa hamu ya kula au kula chakula kingi, muda wote wenyewe hupenda kucheza,” anasema.

Anasema iwapo mtoto anakuwa tayari amepata magonjwa ya akili na kifafa wataalamu humuanzishia dawa maalumu.

“Lakini tiba nyingine ambayo huwa wanapatiwa ni tiba kwa njia ya vitendo. Tiba hii inatolewa na mtaalamu na mwanasayansi aliyesomea jinsi ya kutoa matibabu hayo.

Anasema zipo tafiti nyingi ambazo zimefanywa na kueleza jinsi gani mtaalamu anaweza kubaini milango ya fahamu ya mtoto na jinsi gani inavyopokea taarifa na kuzituma kwenye ubongo wake kutafsiriwa.

“Kwa hiyo anaangalia je ubongo wa mtoto unapokea taarifa sahihi na zinafika kwa kiasi gani. Hapa tunatumia vifaa mbalimbali kwa kumgusisha kwenye mikono yake,” anasema.

Anaongeza “Tunatumia njia hiyo kwa sababu, viganja vina mishipa midogo midogo mingi mno ambayo hupeleka taarifa na kuiwasilisha kwenye ubongo wake.

Anasisitiza kitendo hicho hufanywa kwa kurudia rudia pale tu tatizo linapogundulika.

“Huwa pia tunaangalia mpangilio wake wa mwili, jinsi Mungu alivyoumba mwili umepangiliwa kama kuna tatizo mtaalamu anao uwezo wa kubaini na kumsaidia mtoto tunaita kitaalamu (handling technique),” anasema .

Ushauri

Mtaalamu huyo anashauri wazazi kuwa karibu na watoto wao kufuatilia mwenendo wao wa ukuaji kwani itasaidia kubaini mapema iwapo mtoto ana tatizo hili au la.

“Ni rahisi zaidi mama kubaini, kwa sababu anao uwezo wa kujua kilio cha mtoto kina maana gani, lakini tatizo siku hizi watoto wanalelewa na ‘house girls’.

“Suala la malezi ni muhimu mno kwa mtotio, zamani wazee walikuwa wanakaa na mama aliyejifungua hata siku saba kwa mfano wakimfundisha jinsi ya kulea mtoto walijua umuhimu wake, lakini leo hii hakuna, ni tatizo” anasema.

 Makala haya kwa mara ya kwanza yamechapishwa Agosti 31, mwaka huu kwenye gazeti la MTANZANIA

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement