Picha na mtandao
NA VERONICA ROMWALD – DAR ES SALAAM
NI wazi kwamba sasa kila mmoja wetu anapaswa kuwa makini na
kuzingatia jinsi anavyokula chakula tangu asubuhi hadi anapokwenda kulala usiku.
Ingawa wataalamu wa lishe wanaeleza kiuhalisia hakuna
chakula ambacho binadamu anazuiwa kula katika maisha yake hapa duniani lakini
ni lazima azingatie kiasi na aina ya chakula anachokula kila siku.
Kwa sababu ili aweze kuishi akiwa na afya njema duniani
anahitaji kula chakula hata hivyo wanashauri kwamba ni vema azingatie kula
chakula bora na si bora chakula.
Wanasisitiza iwapo binadamu hatazingatia ulaji unaofaa huwa
anajiweka kwenye hatari ya kupata magonjwa mengi hasa yale yasiyo kuwa ya
kuambukiza.
Magonjwa hayo ni pamoja na magonjwa ya moyo, kisukari,
shinikizo la damu, saratani na mengineyo ambayo kasi yake ya maambukizi
inaonekana kuongezeka ikilinganishwa na kasi ya magonjwa ya kuambukiza.
Kulingana na takwimu zilizotolewa hivi karibuni na Shirika
la Afya Duniani (WHO), inakadiriwa kila mwaka takribani watu milioni 17
hufariki dunia kutokana na kuugua magonjwa ya moyo.
WHO inaeleza kila mwaka zaidi ya watu milioni 75
hugundulika kuwa na magonjwa hayo duniani huku likibainisha kwamba hali ni
mbaya zaidi katika nchi zinazoendelea, Tanzania ikiwamo.
Mafuta
ya nazi/mawese
Mtaalamu wa Lishe wa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete
(JKCI), Louiza Shem, anasema matumizi ya mafuta ya nazi na mawese katika
maandilizi ya chakula yanaweza kumsababishia mtu kupata magonjwa ya moyo.
“Mafuta haya na yale yatokanayo na wanyama yanapaswa
kutumiwa kwa kiasi na si kwa wingi kwa sababu huwa yana kiwango kikubwa cha
lehemu.
“Yanapoingia mwilini huenda kuganda kwenye mishipa ya damu
na inapotokea hali hiyo moja kwa moja mtu huwa kwenye hatari ya kupata magonjwa
ya moyo hasa shinikizo la damu,” anasema.
Nyama
zilizonona
“Ni vizuri pia kuzingatia ulaji wa nyama, nyama ya kuku na
zilizonona huwa na mafuta mengi ambayo yakiingia mwilini huweza kuleta madhara.
“Unywaji wa vinywaji vyenye sukari nyingi huchangia
ongezeko la mafuta kwa wingi na uzito mkubwa kwenye mwili wa binadamu.
Unavyopaswa
kula
“Kwa bahati nzuri hakuna chakula ambacho mtu hatakiwi
kutumia ili kujiepusha na magonjwa ya moyo lakini tunashauri jinsi gani na kwa
kiasi gani uvitumie ili kuepuka kupata magonjwa.
“Mfano ukiangalia vyakula vya wanga (ugali, wali viazi na
vinginevyo) unakuta mtu anakula kupita kiasi, anajaza sahani… wakati mtu anapaswa
kula chakula kulingana na aina yake ya kazi anayoifanya.
“Wengi tunaofanya kazi ofisini hatutumii nguvu nyingi
kulinganisha na wale wanaobeba mizigo, wengi tunakula nyama kwa kiwango
kikubwa, ni vema kupunguza kiasi.
“Mafuta yanayopatikana kwenye nyama yanaongeza uzito kupita
kiasi na huenda kuziba mishipa ya damu, ikiwa ni ya kichwani utapooza mwili na
ikiwa ni kwenye moyo utapata ‘heart attack’,” anafafanua.
Anashauri kwamba ni vema jamii ikajenga tabia ya kupunguza
kiwango cha matumizi ya chumvi wakati wa maandilizi ya chakula.
“Waepuke na waache kabisa tabia ya kuongeza chumvi mezani
wakati wa kula kwani ni hatari kwa afya ya moyo,” anasema.
Anasema kundi linaloathirika ni la vijana ambao wengi wapo
katika umri wa uzalishaji mali.
“Tunaona jinsi umri unavyokwenda ndivyo ambavyo mtu anakuwa
kwenye hatari zaidi ya kupoteza maisha kutokana na magonjwa haya kwa sababu
wengi huchelewa kupata matibabu,” anasema.
Wanawake
Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo wa Taasisi ya Moyo
Jakaya Kikwete, Bashir Nyangasa, anasema wanawake ni kundi ambalo pia lipo
kwenye hatari ya kupata magonjwa hayo.
“Maumbile yao jinsi yalivyo ni rahisi kupata maambukizi kwa
mfano ya njia ya mkojo (U.T.I), anapokuwa kwenye kipindi cha hedhi ni muhimu
kuzingatia usafi.
“Ikiwa atatumia pedi moja kwa muda mrefu anakuwa anajiweka
kwenye hatari zaidi kwa sababu ile damu ikajaa kwenye pedi hutengeneza bacteria
(wadudu) ambao husababisha maambukizi kwenye kizazi.
“Wadudu hao huweza kusafiri na kufika hadi kwenye moyo na
kuuathiri pamoja na viungo vingine ikiwamo figo.
“Hivyo ni muhimu kuzingatia suala la usafi wa mwili wakati
wote na hasa mwanamke anapokuwa katika kipindi cha hedhi,” anasisitiza.
Watoto
Dk. Nyangasa anasema wakati mwingine hutokea mtoto
akazaliwa na magonjwa ya moyo ambayo kitaalamu huitwa ‘congenital heart
disease’.
“Wengi huzaliwa na matundu kwenye moyo au unaweza kukuta mishipa
yao ya damu haijakaa sawasawa, au wakati mwingine kama mama aliugua magonjwa
mbalimbali wakati wa ujauzito kwa mfano kaswende huweza kusababisha mtoto wake
kuzaliwa na magonjwa haya.
“Kuna magonjwa ya kurithi pia kwenye familia, kuna magonjwa
ya surua, rubella ambayo huweza kusababisha mtoto kuzaliwa na magonjwa ya moyo,”
anasema.
Daktari huyo anasema mtoto akizaliwa njiti huwa kwenye
uwezekano mkubwa wa kupata tatizo kwenye moyo wake.
“Kunakuwa na mambo mawili, vile ambavyo havijatimia kwa
rehema za Mwenyezi Mungu vitaendelea kutimia au vinaweza visiendelee kutimia,
ndiyo utakuta wale ambao ukiuliza historia ya mtoto ujagundua ana tatizo,”
anaeleza.
Jinsi
ya kubaini tatizo
Anasema mzazi anaweza kubaini tatizo la moyo kwa mtoto hata
kabla ya kumfikisha hospitalini.
“Unakuta hawezi kushika chuchu ya mama yake kwa dakika
mbili au tatu ili anyonye kama inavyotakiwa, utaona anashika kwa dakika kadhaa
na kuachia chuchu, akiachia utaona anapumua kwa shida kwa kutumia mdomo wake,”
anabainisha.
Hali
ilivyo JKCI
Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo wa JKCI, Tulizo Sanga, anasema
katika taasisi hiyo kila siku wanapokea na kuhudumia wagonjwa zaidi ya 300
wanaosumbuliwa na magonjwa hayo.
Dk. Sanga ambaye pia ni Mkurugenzi wa Huduma Bora za Afya
wa Taasisi hiyo, anasema wengi hufika wakiwa wamechelewa.
“Ni kwa sababu hatuna utamaduni wa kupima afya mara kwa
mara, ni vema jamii ikabadilika na kuanza kupima afya,” anashauri.
Matibabu
Dk. Nyangasa anasema ili kuzibua mishipa iliyoziba kwenye
moyo huwa wanatumia chuma maalumu ambacho kimetengenezwa kwa uwezo wa hali ya
juu.
“Kile huwa ni ‘stain- less steel’ ni mfano wa vile
vinavyotumika kutengeneza ndege huwa havishiki kutu,” anabainisha.
Anasema mtu aliyewekewa chuma anaruhusiwa kufanya kazi zote
isipokuwa zile za kutumia nguvu nyingi.
“Kwa mfano kina mama tukiweka kile chuma lazima tumfuatilie
sana kuhusu suala la kubeba ujauzito, msichana ambaye hajawahi kuzaa akiwekewa
kile chuma ni lazima atumie dawa za kuyeyusha damu maisha yake yote.
“Akishika ujauzito badala ya kutumia vidonge, miezi mitatu
ya awali tutampa dawa kwa njia ya sindano kila siku,” anasema.
“Wagonjwa wangu huwa wananiuliza… watatumia dawa maisha
yote, na mimi nawatania mbona wanakula kila siku, jambo la msingi mama akifikia
kipindi cha kujifungua lazima ajitahidi aende kwenye hospitali kubwa ili
wamsaidie inapotokea tatizo.
Changamoto
Dk. Nyangasa anasema changamoto kubwa inayowakabili ni
upatikanaji wa vifaa ambavyo vingi hununuliwa kutoka nje ya nchi.
“Vifaa vyote ambavyo vinatumika katika matibabu ya moyo,
vingi havitengenezwi Afrika, vinatengenezwa Ulaya na Marekani. Kwa mfano
Kampuni ya St. Jude wale wameshika soko kwa ajili ya kutengeneza ‘valve’ na
ukitaka kuwa wakala hapa lazima upate kibali maalumu kutoka kwao.
“Na si vifaa vya moyo tu bali vifaa vingi vya hospitalini
vinakuja kutoka huko, sasa changamoto ni kwamba kile kifaa unaweza kukuta kule
kinauzwa Dola 1000 (zaidi ya Sh milioni mbili).
“Yule wakala hadi akilete hapa Tanzania akilipie Mamlaka ya
Mapato Tanzania (TRA), mnunuzi wa mwisho unakuta gharama imeongezeka hadi kufikia
Sh milioni tano, ni changamoto kubwa,” anasema.
Makala haya kwa mara ya kwanza yamechapishwa Oktoba 12, mwaka huu kwenye gazeti la MTANZANIA
Chapisha Maoni