Na Mwandishi Wetu, Njombe
KUTOKANA na ushirikishwaji wa
wakulima wadogo katika zao la chai kupitia Kampuni ya Kuhudumia Wakulima Wadogo
Njombe (NOSC), viongozi wa Mkoa wa Njombe wanajivunia mafanikio yaliyopatikana
katika kilimo cha chai kilichosaidia kuinua kipato cha wakulima wadogo na
kuongeza fedha za kigeni.
Hayo yamesemwa na Katibu Tawala
Msaidizi Uchumi na Uzalishaji Mkoa wa Njombe, Bwana Lameck Noah kwa niaba ya
Mkuu wa Mkoa huo Bw. Christopher Ole Sendeka mkoani hapa jana katika mahafali
ya mwaka mmoja kuhusiana na mafunzo ya kilimo cha chai kilichohusisha wakulima
zaidi ya 206.
“Katika mkoa wetu tulijiwekea
utaratibu kuwa kila mkulima alime mazao ya aina mbili ya chakula na biashara,
kwa upande wa chai tatizo lilikuwa ni aina ya miche, ilikua inachukua muda
mrefu kukua lakini tunaishukuru NOSC imetuletea mice inayokua kwa miezi 12
mkulima anaanza kupata majani mabichi ya chai,” alisema Bw. Noah.
Alibainisha kuwa elimu hiyo ina maana
kubwa kwa mkoa wake kwa sababu itawasaidia kulima kisasa na kuwaongezea kipato
wananchi wa mkoa huo, lakini pia viwanda vitapata malighafi hiyo muhimu kwa
ajili ya soko la ndani na nje.
“Tunafahamu chai inapendwa na mataifa
ya magharibi, zao hili lina fedha nyingi za kigeni. Soko la chai lipo na
tunawahakikishia wakulima serikali inahangaika kupata mnada wa chai katika
ukanda huu badala ya kufanyika Mombasa nchini Kenya.
“Elimu kwa wakulima kupitia huu mfumo
ni suala zuri kwa kuwa wakulima watakua na kilimo endelevu waliofundishwa
watawafundisha wenzao ili kupata mafuno mazuri na mazao yenye ubora, tunafahamu
katika eneo hili kuna kiwanda cha Uniliver kinakaribia kukamilika maana yake
watahitaji majani mengi ya chai ili kulisha kiwanda.
Wakiendelea kulima zaidi
tutawavuta wawekezaji wengi zaidi katika mkoa wetu ili kufikia azama ya
serikali ya viwanda,” alisema Bw. Noah.
Mkurugenzi Mtendaji wa NOSC, Bwana
Filbert Kavia alisema utaratibu wa kuwafundisha wakulima shambani watajitahidi
kuusambaza katika maeneo mengine ya nchi ili wafundishwe wakulima wa mazao
mbalimbali kwa lengo la kupunguza tatizo la maofisa ugani.
“Tulianza na vikundi vinane na
tutaendelea na vikundi vingine mwakani, huu utaratibu ni mzuri kwa sababu
unampa fursa mkulima kujifunza kwa vitendo, kwa kawaida wakulima huelewa zaidi
kwa kuona shambani.
“Vilevile nchi yetu ina uhaba wa
maofisa ugani, hawa wakulima watawafundisha wakulima wenzao, kama eneo
linahitaji maofisa ugani 20 wanaweza kutumika chini ya hapo. Tunaamini kwa sasa
tutapata mavuno mengi na yenye ubora kwenye chai baada ya mafunzo haya,”
alisema Bw. Kavia.
Akizungumza kwa niaba ya wakulima
wenzie Bw. Thiemo Msemwa alisema: “nashukuru kwa kupewa cheti cha mklulima bora
wa chai, nimefurahia mafunzo haya ya kilimo endelevu na kanuni kumi za kilimo
endelevu na hata wananvu ninapowaambia waje kwenye shamba la chai wanafurahi
kuja shambani kwa sababu kuna mambo mengi ninawafunza.”
Mafunzo hayo yamedhaminiwa na mpango
wa Chai Project kwa lengo la kusaidia viwanda vya chai nchini kwa msaada kutoka
The Wood Foundation Africa (TWFA), Gatsby Cheritable Foundation (Gatsby) na
UKAID ambapo NOSC imedhamiria kulima chai katika eneo lenye ukubwa wa jhekta
3,800 na kufikia wakulima 4,000.
Chapisha Maoni