Recent Post


 


moja

Responsive Advertisement
Na Veronica Romwald, Dar es Salaam

WATOTO 15 kati 100 wanaofariki dunia nchini vifo vyao huwa vimetokana na ugonjwa wa nimonia, imeelezwa

Nimonia unatajwa kushika nafasi ya pili kusababisha vifo vya watoto wachanga nchini na kwamba ni miongoni mwa magonjwa yanayochangia vifo vya watoto wachanga duniani.

Kaimu Meneja Program ya Afya ya Mtoto wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk Felix Bundara amesema hayo hivi karibuni katika mahojiano mahojiano maalumu na mtandao huu.

Dk Bundara amesema hiyo ni kwa mujibu wa utafiti wa Utafiti wa Afya ya Uzazi na Mtoto na Malaria Tanzania wa mwaka 2015/16 (TDS).

“Utafiti huo ulionesha wazazi na walezi hawapeleki watoto kutibiwa pindi wanapopata kikohozi hali ambayo inawaweka kwenye hatari, kati ya watoto 100 waliopata kikohozi 55 pekee ndiyo walifikishwa hospitalini,” amebainisha.

Amesema jamii inapaswa kuamka na kuhakikisha mtoto anapopata tatizo la kikohozi anafikishwa mapema hospitalini kwa uchunguzi.

“Watoto 45 hawakufikishwa hospitalini, wapo ambao wamejenga mazoezi ya kwenda kununua dawa za ‘antibiotics’ madukani na kuwapatia watoto wanapopata kikohozi,” amesema.

Ameongeza “Si jambo sahihi, wajue kwamba si kila kikohozi ni nimonia kitendo cha kuwapatia dawa bila ushauri wa daktari kunaweza kusababisha kutengeneza usugu wa dawa mwilini.

Dk. Bundara amesema ingawa ugonjwa huo huwapata pia watu wazima hata hivyo watoto wapo hatarini zaidi kupoteza maisha kwa sababu kinga yao haipo ya kutosha.

“Ni ugonjwa ambao unaathiri mapafu unaweza kuupata kwa kupata maambukizi ya bacteria, virusi au fangasi,” amesema.

Amesema dalili kuu ya kwanza huwa ni kukohoa na kupata shida ya kupumua.

Amesema watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi kwa mfano yenye moshi wa kuni, mkaa, sigara, nyumba isiyo na hewa ya kutosha wapo hatarini zaidi kupata ugonjwa huo.

“Mtoto anapaswa kunyonya maziwa ya mama miezi sita bila kupewa kitu chochote ile humsaidia kupata lishe, akikosa lishe anakuwa kwenye hatari pia ya kupata ugonjwa huo,” amesema.

Amesema wazazi wanapaswa kuwawahisha hospitalini watoto ili wapate matibabu sahihi na si kwenda kuwakata kimeo.


“Huko wanapoteza damu nyingi na hivyo kufariki dunia, serikali inafanya jitihada nyingi na tunatoa chanjo katika kila kituo chenye huduma ya afya ya mama na mtoto, wawalete wafanyiwe uchunguzi,” ametoa rai.

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement