Recent Post


 


moja

Responsive Advertisement
Mbu aina zote hueneza ugonjwa wa matende na mabusha.
Na Veronica Romwald, Dar es Salaam


WENGI wetu tunajua kwamba busha ni hali inayowapata wanaume pekee ambayo husababisha kuvimba kwa maumbile yao katika sehemu za siri.

Miaka ya nyuma, jamii nyingi hasa zile zinazoishi katika maeneo ya Pwani ziliwapa heshima kubwa watu waliokuwa na hali hiyo.

Huwaita Mamwinyi mara nyingi huwa wakivaa  vazi maalumu liitwalo msuli na kila walipotembea hushika fimbo maaalum mkononi mwao iliyowawezesha kutembea kutoka eneo moja hadi jingine.

Jamii iliwaogopa pia watu waliokuwa na hali hiyo kwani wengi wakihusishwa na imani za kishirikina kwamba wana nguvu za kipekee zinazoweza kumdhuru au kumwadhibu mtu yeyote anayekwenda kinyume na matakwa yao.
Hatukujua kuwa hali ile ni ugonjwa ambao huweza kumsabishia mwanaume kukosa nguvu za kushiriki tendo la ndoa kikamilifu na hata kumsababishia ugumba au utasa kabisa.

Hali huwa mbaya zaidi pindi anapochelewa kwenda hospitalini kufanyiwa uchunguzi kisha upasuaji kutibu tatizo, wengi walikuwa wakijificha majumbani.

“Hiyo ni changamoto kubwa ambayo tumekabiliana nayo kwa muda mrefu katika mapambano dhidi ya ugonjwa huu, wengi wanaogopa kujitokeza hasa wanawake,” anasema Kaimu Meneja Mpango wa Taifa Magonjwa yaliyokuwa Hayapewi Kipaumbele, Oscar Kaitaba (pichani chini).
Image result for busha, ngiri maji velipoje
MTANZANIA / matukionamaisha limezungumza kwa kina na Kaitaba juu ya ugonjwa huo, namna unavyoambukizwa na nini hasa husababisha mtu kupata hali hiyo.

Anasema ugonjwa huo hutokana na minyoo iitwayo kitaalamu….. ambayo huenezwa na mbu kutoka kwa mtu mwenye ugonjwa hadi kwa mtu ambaye hana ugonjwa huo.

“Mbu hunyonya damu kwa mtu ili kurutubisha mayai yake sasa inapotokea amemng’ata mtu mwenye minyoo hiyo huibeba na ikiwa atamng’ata yule ambaye hana minyoo hiyo basi humwambukiza,” anasema.

Anasema ikiwa minyoo hiyo inapoingia kwenye mwili wa binadamu itakwenda kuziba mirija ya mfumo wa damu iliyopo katika maeneo mengine ya mwili kwa mfano miguuni basi hapo huitwa tende.

“Lakini minyoo ile ile ikiwa itakwenda kuziba mirija ya mfumo wa damu iliyopo katika sehemu za siri basi hapo huitwa busha, hivyo huu ni ugonjwa aina moja ambao unatokana na minyoo ambayo husambazwa na mbu,” anabainisha.

Anasema maeneo ya Pwani yanaonekana kuathirika zaidi na ugonjwa huo kuliko mengine kwani huko mbu huzaliana kwa wingi zaidi.

“Na kadiri mtu anavyoumwa na mbu wengi ndivyo anavyokuwa kweneye uwezekano mkubwa zaidi wa kupata ugonjwa huu kuliko wengine,” anasema.

Maji ya dafu

Kaitaba anasema si kweli kwamba maji ya dafu huweza kumsababishia mtu kupata ugonjwa huo kama ambavyo wengi wamekuwa wakidai.

“Maji ya dafu yanahusianishwa tu na tatizo hili lakini ukweli ni kwamba maeneo ya Pwani nazi ni zao lao la kibiashara.

“Sasa unakuta watu wanakula madafu kisha wanatupa ovyo vile vifuu, kumbuka awali nimesema kwamba minyoo inayosababisha tatizo hili.

“Kwa hiyo wanapotupa vile vifuu ikitokea mvua ikanyesha vile vifuu vikajaa maji basi mbu huzaliana kwa wingi na hivyo kuongeza ule uwezekano wa watu kupata maambukizi,” anasema.

Anaongeza “Kwa hiyo si kweli kwamba ile ni ishara ya ukuu (umwinyi), wanajifariji tu na wala wasihusianishe na nguvu za kishirikiana watu wanapaswa kuelewa kwamba ule ni ugonjwa unaosababishwa na minyoo.

“Wajue ni tatizo la kiafya na linalohitaji matibabu ya haraka ili kukabiliana nalo ikiwa tayari mtu amepata zile athari za kuvimba (maji na manyanyama) katika sehemu zake za siri.

Dalili

Kaimu Meneja huyo anasema kwa kawaida dalili za ugonjwa huo huanza kujitokeza miaka mitatu baadae tangu mtu alipoambukizwa.

“Dalili hizo ni pamoja na kupata homa za mara kwa mara, maumivu na kuvimba mitoki, miguu kuwaka moto, maumivu ya kichwa na mengine mengi,” anabainisha.

Wanawake

Anasema miaka ya nyuma wengi walijua tatizo hilo huwapata wanaume pekee lakini si kweli.

“Linawapata pia wanawake lakini wengi huwa hawajitokezi na nadhani kwa sababu zamani kwa mfano walikuwa wakijifungua kwa wakunga wa jadi ilikuwa rahisi kwao kujificha.

“Lakini leo hii wanakuja hospitalini na wakunga wanapowagundua huwapatia ushauri nasaha na kuwahimiza waanze matibabu mara moja,” anabainisha.

Inakuwaje

Kaitaba anasema wakati wanaume huwa wanavimba sehemu wanawake hupata pia uvimbe katika sehemu zao za siri hasa eneo la mashavu ya uke.

“Huwa yanavimba kiasi cha kuziba kabisa eneo lote la uke na wakati mwingine uvimbe unapozidi huweza kuziba ile njia ya mkojo na hivyo kusababisha kupata mkojo kwa kiwango kidogo mno,” anabainisha.

Anaongeza “Ikiwa mwanamke hupata maumivu kutokana na hali hiyo na kwamba ikiwa hatakwenda mapema hospitalini kutibiwa huweza kujikuta mwili wake hukitoa harufu mbaya.

“Lakini kama nilivyosema awali wanawake si wengi wanaojitokeza kama ambavyo wanaume wanagundulika na kujitokeza, hadi sasa nafahamu wanawake watatu ambao wamejitokeza na kutibiwa.

“Mmoja makazi yake ni huko Mkuranga mkoani Pwani, kuna ambaye anaishi Mororogo na mwingine yupo Muheza mkoani Tanga,” anasema.

Hofu

Anasema watu wengi wenye tatizo hilo huogopa kujitokeza kufanyiwa upasuaji kwa hofu ya kufariki dunia wakati wakipatiwa matibabu hayo.

“Hofu hiyo imejenga tangu zamani, unajua wakati ule teknolojia ilikuwa haijakuwa kama ilivyo sasa, mtu aliyehitaji upasuaji alilazimika kuchomwa sindano ya ganzi mwili mzima.

“Sasa unakuta watu wengi waliokuwa na tatizo walikuwa na umri mkubwa walipopewa ganzi kuna baadhi yao walijikuta wakipata tatizo la shinikizo la juu la damu na hivyo kupoteza maisha.

“Lakini leo hii mambo yamebadilika, teknolojia imekuwa kwa kiwango cha hali ya juu sana, siku hizi tunapomfanyia mtu upasuaji hatuhitaji tena kumpa ganzi mwili mzima.

“Tunachofanya tunachoma ganzi katika eneo tunalohitaji kufanya upasuaji na mtu anaweza kushuhudia kila tunachofanya katika mwili wake na tunapomaliza ikiwa ulikwenda vizuri basi anaweza kuruhusiwa kurudi nyumbani kwake hata baada ya saa mbili tangu upasuaji kumalizika,” anasema.

Anaongeza “Tena anakwenda nyumbani kwake akitembea bila kusaidiwa na mtu yeyote akiwa amepona kabisa tatizo lililokuwa linamsumbua.

Anasema kutokana na mafanikio hayo sasa jamii imekuwa na mwamko mkubwa wa kujitokeza kufanya uchunguzi na kisha kufanyiwa upasuaji kutibu tatizo hilo.

“Ingawa bado kuna maeneo machache kwa mfano Tanga kuna changamoto kidogo mwamko si mzuri kama ilivyo kwa maeneo mengine ya Pwani kama Mtwara na Lindia,” anabainisha.

Anasema wanaume wengi wanaowafanyia upasuaji huo huwa wanawatoa uvimbe wenye kilo zipatazo 20 hadi 30 na kwamba kama haukuathiri zaidi basi huweza kushiriki tendo la ndoa kama kawaida na mwezi wake.

“Kuna kipindi nakumbuka tuliwahi kumfanyia upasuaji mwanamume mmoja pale Hospitali ya Taifa Muhimbili alikuwa na uvimbe ambao ulikuwa na kilo 60, ni hatari kubwa.

“Kutokana na kuongezeka huko kwa uvimbe ikiwa mwanaume atachelewa kufanyiwa upasuaji basi huweza kumsababishia tatizo la nguvu za kiume na au korodani zake kuoza,” anasema.

Anaongeza “Hivyo ikiwa korodani zake zitaoza basi tutalazimika kumfanyia upasuaji kuziondoa lakini kama zitakuwa salama basi tunaondoa tu ule uvimbe na anakuwa na uwezo wa kushiriki na kuzalisha kama kawaida.

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement