Na Veronica Romwald, Dar es Salaam
NOVEMBA, mwaka jana Jumanne Salum (34) aligundulika
kuwa na dalili za awali za saratani ya tezidume aliamua kwenda kufanyiwa uchunguzi
katika hospitali moja ya binafsi jijini hapa.
“Awali nilikuwa napata shida kupata haja ndogo
tatizo hilo lilianza taratibu na liliongezeka kadri muda ulivyokuwa unasonga,
nikaamua kuchukua hatua,” anasema.
Anasema alidhani ni ugonjwa wa kawaida lakini
alishtushwa na majibu ya awali aliyopatiwa na daktari wake.
“Alinieleza nina dalili za awali za saratani ya
tezidume, basi akanishauri tufanye vipimo zaidi ili kujiridhisha nikakubali,
baada ya uchunguzi alisema kuna majimaji katika kiungo hicho ambayo yamevuka
kiwango kinachostahili,” anasema.
Anasema daktari huyo alimuuliza maswali mbalimbali
ikiwamo uwezo wake wa kushiriki tendo la ndoa na mwenzi wake.
“Sikumficha… nilimueleza kila kitu kwamba huwa
siwezi kushiriki zaidi ya mara moja pindi ninapokutana faragha na mwenzi wangu.
“Basi alinieleza vyanzo mbalimbali vinavyosababisha
tatizo hilo ikiwamo kitendo cha kutoshiriki vema tendo la ndoa kwamba ni
mojawapo ya visababishi, nikastaajabu, nikaanza matibabu ambayo naendelea nayo
hadi sasa,” anasema.
Kelvin Johnson anasema hana uwelewa wowote kuhusu
saratani ya tezidume na iwapo kutoshiriki tendo hilo kunaweza kuwa chanzo cha
mwanaume kupata ugonjwa huo.
Picha ya mtandao inaonesha mahala tezidume ilipo
“Mimi najua usipozingatia ulaji unaofaa, kufanya
mazoezi, unywaji wa pombe kupitiliza ni miongoni mwa mambo yanayoweza
kusababisha mwanaume kupata ugonjwa wa saratani ya tezidume.
“Kuhusu kutoshiriki tendo la ndoa ni suala jipya
kwangu, sijawahi kusikia kabla labda kama wataalamu wa afya wakituelewesha juu
ya hilo tuanze kuchukua hatua,” anasema.
MTANZANIA limezungumza na Daktari Bingwa wa
Magonjwa ya Saratani wa Taasisi ya Saratani Ocean Road (ORCI), Mark Mseti
ambaye anafafanua kwa kina katika makala haya.
Tezidume
ni nini?
“Tezidume ni
kiungo muhimu kilichopo ndani ya mwili wa mwanamume, chini kidogo ya kibofu
cha mkojo kikiuzunguka mrija wa kutolea haja ndogo.
“Kamwe huwezi kuiona kwa nje, ipo kwa ndani ni
kiungo chenye umuhimu wa kipekee katika kukamilisha mfumo wa uzazi wa
mwanamume,” anasema.
Anasema kiungo hicho hutengeneza majimaji maalumu
ambayo huambatana na mbegu za kiume wakati wa tendo la ndoa zikilinda mbegu
hizo hadi kulifikia yai la mama na kutengeneza mtoto.
“Kwa kawaida tezidume huwa na ukubwa unaolingana na
punje ya njegere au mbaazi na huongezeka ukubwa kutokana na mambo mawili,”
anasema.
Anataja mambo hayo kuwa ni kule kuongezeka kwa umri
wa mwanaume au tatizo la saratani ya tezidume.
“Tezidume huweza kuongezeka hadi kufikia ukubwa wa
tunda la apple,” anabainisha.
Saratani
ni nini?
Anasema saratani ni jina ambalo limetungwa na
wataalamu likiwa na mkusanyiko wa kundi la magonjwa mengi yanayofanana kwenye
njia kuu mbili.
“Kwanza ni kule kukosekana kwa udhibiti wa
uzalianaji wa seli au chembechembe hai za mwili, pili ni kutodhibitiwa kwa zile
chembechembe hai zinazozaliana kwa wingi ambazo huweza kusafiri kutoka sehemu
zilipozaliwa kwenda sehemu mbalimbali za mwili,” anasema.
Anasema chembechembe hizo, huko huendelea kuota na
kuzaliana kwa wingi na pindi zinapoanza kusambaa humanisha ugonjwa umefikia
hatua ya nne ambayo huwa ni ya mwisho.
Anasema inapotokea tezidume limepata saratani
dalili kadhaa hujitokeza ambazo pia huwa zinafanana kwa ukaribu na dalili za
magonjwa ambayo hushambulia njia ya haja ndogo.
“Hivyo, hatuwezi kujua iwapo ni saratani au la,
hadi tutakapofanya vipimo mbalimbali hasa kile cha kuchukua sampuli (kinyama)
kutoka kwenye tezidume na kuifanyia uchunguzi maabara,” anabainisha.
Takwimu
za WHO
Takwimu za Shirika la Afya Duniani (WHO) za mwaka
2012 kila mwaka wagonjwa wapya milioni 14.1 hugundulika kati ya hao milioni 8.2
hufariki dunia ikiwa ni sawa na asilimia 13.
WHO inakadiria kwamba vifo hivyo vinategemewa
kuongezeka kufikia milioni 22 ifikapo 2030.
Hali
ilivyo nchini
Takwimu zilizotolewa na Wizara ya Afya, Maendeleo
ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Oktoba, 2017 zinaonesha kila mwaka wagonjwa
wapya 50,000 hughundulika wakiwa na magonjwa ya saratani.
Waziri Ummy Mwalimu anasema Tanzania ni mojawapo ya
nchi za Kusini mwa Afrika ambazo zinakadiriwa kuwa na idadi kubwa ya wagonjwa
na kwamba idadi hiyo inakadiriwa kuongezeka kwa asilimia 50 ifikapo mwaka 2020.
Kulingana na Waziri Ummy, taarifa kutoka Taasisi ya
Saratani ya Ocean Road kwa kipindi cha mwaka 2006 hadi 2015 zinaonyesha kwamba
aina za Saratani inayoongoza kuwa na idadi kubwa ya wagonjwa ni ya mlango wa
kizazi yenye asilimia 34.
“Ikifuatiwa na saratani ya ngozi (kaporsis Sarcoma)
asilimia 13, saratani ya matiti asilimia 12, saratani ya mfumo wa njia ya
chakula asilimia 10, saratani ya kichwa na shingo asilimia saba.
“Saratani ya Matezi asilimia sita, saratani ya damu
asilimia nne, saratani ya Kibofu cha mkojo asilimia tatu, saratani ya ngozi asilimia
tatu, saratani ya macho asilimia mbili.
“Nyingine ni saratani ya tezi dume asilimia mbili,
mbaya zaidi, asilimia 80 ya wagonjwa
wote hao hufika Ocean Road wakiwa katika hatua za mwisho za ugonjwa na kufanya matokeo ya matibabu
kutokuwa mazuri,” anasema.
Kuhusu
tendo
Dk. Mseti (Pichani) anasema zipo tafiti ndogondogo ambazo
zimewahi kufanyika duniani ambalo zinathibitisha ukweli uliopo juu ya suala
hilo.
“Ingawa hakuna utafiti mkubwa uliofanyika
kuthibitisha mtu anapofanya ngono mara ngapi kwa wiki hawezi kupata saratani
hiyo.
“Lakini zipo tafiti ndogo ndogo ambazo zinaeleza
mwanaume ambaye yupo ‘sexually active’ ana uwezekano mdogo kupata saratani ya
tezidume kuliko yule ambaye hayupo ‘sexual active’,” anabainisha.
Anaongeza “Hata hivyo, hii haimaanishi mtu awe
mzinzi la hasha, kwa sababu akiwa na wapenzi wengi atapata magonjwa hasa ya
zinaa ikiwamo Ukimwi na kuyaweka maisha yake hatarini zaidi.
“Inashauriwa angalau mwanaume ashiriki mara tatu
kwa wiki ingawa wapo wengine wanaojiweza zaidi ya hapo,” anasema.
Dalili
zenyewe
Anasema zipo dalili nyingi ambazo hujitokeza na
kawaida katika hatua ya awali huwa hazimsababishii usumbufu wa aina yoyote
mwanaume husika.
Anasema hiyo ndiyo sababu wanaume wengi hufika
hospitalini wakiwa wamechelewa.
“Dalili za awali ambazo mwanamume akiziona
tunamshauri awahi hospitalini kwa uchunguzi ni pamoja na kutoa mkojo ambao
hauna nguvu, wakina baba kwa kawaida mkojo wao huweza kuruka umbali wa mita moja
hadi mbili.
“Ingawa kadri umri unavyoongezeka ile kasi ya kurusha
mkojo hupungua, kwa mtu ambaye ana tatizo la saratani ya tezidume ile kasi
hupungua zaidi hata akiwa na umri mdogo,” anasema.
Dk Mseti ambaye pia ni Mkuu wa Kitengo cha Huduma
za Tiba na Mifumo ya Kulipia (bima za afya) ORCI, anataja dalili nyingine ni
kutoa mkojo ambao hukatika-katika.
“Ingawa, dalili hii hatuwezi kusema moja kwa moja
kila ambaye mkojo wake hauruki kwa kiwango hicho ana tatizo kwani wapo baadhi
ya wanamume ambao tangu wamezaliwa wanapata mkojo unaokatika-katika.
“Lakini kwa yule ambaye zamani walikuwa wakienda
haja ndogo wanatoa mkojo bila kukati-katika mwanzo hadi mwisho na ghafla
anaanza kupata mkojo unaokatika-katika ni wazi hiyo ni dalili ya awali ya
saratani hii,” anasema.
Daktari huyo anataja dalili nyingine ya awali ni
mwanaume kushindwa kutoa mkojo pindi tu anapofika chooni.
“Yaani anahisi kabisa kutoa haja ndogo lakini
akifika chooni mkojo hautoki, inabidi asubiri… aubembeleze na wengine hadi
wajikamue ndipo utoke, si dalili nzuri,” anabainisha.
Anaongeza “Kitendo cha mkojo kutoka huku ukiwa
unawasha washa au kuchoma choma inaweza kuwa dalili ya awali ya saratani,
ingawa inaweza pia kuwa dalili ya magonjwa mengine ya kuambukiza ni muhimu
kuwahi hospitalini.
Anataja nyingine ni mkojo kushindwa kutoka vema na
kwamba wapo ambao hulazimika kujikamua tumboni na hivyo kujikuta wakipata
maumivu ya tumbo na mkojo hutoka ukiambatana na maumivu makali.
“Inapofikia hapo maana yake ni kwamba tayari
saratani ya tezidume imekua na sasa imeubinya (imekandamiza) ule mrija wa mkojo
hivyo unashindwa kabisa kupita ipasavyo,” anabainisha.
Anaongeza “Kwa kawaida mkojo huwa unatoka mweupe
hasa mtu anapokuwa anakunywa maji ya kutosha, lakini unapotoka ukiwa na damu
damu ni dalili ya hatari.
Visababishi
Anasema sababu kuu ni kuzaliwa jinsi ya kiume
kwamba kila mwanaume ana uwezekano wa kupata saratani hii.
“Umri unapoongezeka hasa kuanzia miaka 50 na
kuendelea muhusika anaweza kupata saratani hii, pia unywaji wa pombe kupita
kiasi, unene uliopitiliza ni miongoni mwa visababishi,” anasema.
Anasema wapo pia ambao hupata saratani hiyo
kutokana na sababu ya kurithi hasa ikiwa kwenye familia au ukoo kuna ndugu wa
damu ambaye amewahi kuugua saratani hiyo.
Hukua
taratibu
Anasema saratani ya tezidume ni miongoni mwa
saratani ambazo hukua taratibu mno na inaponekana maana yake huwa imeanza muda
mrefu.
“Na hii ndiyo taasisi yetu sasa hivi inajikita
zaidi katika kuelimisha jamii, watu wajitokeze mapema kufanya uchunguzi wa
awali,” anasema.
Anaongeza “Wengi walikuwa wanaogopa baada ya
kusikia kipimo ni kidole lakini wasiogope hicho ni kipimo cha juu mno, awali
tunafanya hicho cha PSA (cha damu).
Uchunguzi
Anasema muhusika anapofika hospitalini hufanyiwa
vipimo mbalimbali ili kujua iwapo ana tatizo hilo au la.
“Tunaanza kwa kufanya vipimo vya awali… tunapima
mkojo wake tujue nini hasa kinamsumbua iwapo ni saratani ya tezidume au
magonjwa mengine ya maambukizi,” anasema.
Anaongeza “Tunafanya kipimo cha ultra sound ambacho
hutuwezesha kuona vizuri ile tezidume na mtaalamu anaweza kutueleza pia limekua
kwa ukubwa gani.
“Watu wengi hudhani zile kende (korodani) ndiyo
tezidume la hasha, hivi ni viungo viwili tofauti, tezidume ipo chini kidogo ya
kibofu ndani ya mwili wa mwanamume.
“Ule mrija wa mkojo unapita katikati ya tezidume na
ndiyo maana dalili nyingi nilizotaja utaona ni kupata shida wakati wa kukojoa
kwa sababu linapoongezeka ukubwa huziba ile njia,” anabainisha.
Kuhusu
kidole
Anasema ni kipimo muhimu pia katika kufanya
uchunguzi na kwamba kamwe huwa hawakifanyi kwa nia mbaya kama wengi
wanavyodhani.
“Mtaalamu anajua jinsi ya kutumia kipimo hiki, anapoingiza
kidole chake huweza kulipapasa lile tezidume kwa ndani na akajua iwapo kuna
tatizo au la,” anasema.
Anasema kipo pia kipimo cha damu (Full Blood
Picture) ambacho hukitumia kufanya uchunguzi huo na huchunguza viungo vingine
vya mwili ikiwamo ini, figo na vinginevyo iwapo vinafanya kazi yake sawa sawa
au la.
“Tunatumia kipimo maalumu kinaitwa PSA (Prostate
Specific Antigen), ni kipimo cha juu sana kwa mtu ambaye ana tatizo hili,”
anasema.
Anafafanua kwamba PSA ni kemikali maalumu ambayo
hutengenezwa na tezidume huwa wanatumia kipimo cha damu kupima kiwango cha kemikali
hiyo mwilini.
“Kwa kawaida, mwanaume aliyekamilika kiwango cha
kemikali yake huwa ni kati ya sifuri hadi nne hiki ni kiwango cha kawaida na
huashiria hana tatizo.
“Lakini inapokuwa zaidi ya nne hadi 20 hapo
humaanisha kemikali hiyo imetengenezwa kwa wingi na matokeo hayo yanatoa
tafsiri kwamba kuna hali isiyo ya kawaida kwenye tezidume.
“Inaweza ikawa ni ukuaji wa kawaida wa tezidume
(usio ugonjwa) kutokana na umri mkubwa au maambukizi na pia inaweza kuwa ni
saratani,” anasema.
Kwanini
Anasema mara zote ukuaji wa tezidume usio wa
saratani (Benign Proestate Hypertrophy – BPH) dalili zake huwa zinafanana dalili zake na ukuaji wa tezidume ulio
saratani.
“Dalili zinafanana kwa ukaribu kwa mfano wanaume
wengi wenye umri mkubwa hupata matatizo ya haja ndogo ile ni kutokana na kukua
kwa tezidume lakini tutajua ni ukuaji wa kawaida au saratani pindi
tutakapomfanyia vipimo,” anabainisha.
Anasema mara nyingi vihatarishi vya saratani ya
tezidume vinafanana na vihatarishi BPH lakini kwa BPH kihatarishi kikuu ni umri
mkubwa.
“Mwanaume mwenye umri mkubwa atapata shida ya haja
ndogo kwa sababu ya kule kukua kwa tezidume yake,” anafafanua.
Anaongeza “BPH humaanisha tezidume limekua lakini
seli zimeendelea kudhibitiwa ingawa nayo huweza kupandisha kiwango cha PSA huwa
juu ya nne lakini haizidi 20.
“Tutamfanyia upasuaji mgonjwa kuongeza kidogo njia
yake ya mkojo ili utoke kwa wepesi kama kawaida.
Anasema ikiwa mgonjwa atakutwa na PSA zaidi ya 20
huwa ni dalili kubwa kwamba ule ukuaji wa tezidume si wa kawaida bali saratani.
“PSA test zipo aina mbili, kuna qualitative PSA
test, hii hutuonesha iwapo kile kiwango kimezidi au la na kuna quantitative PSA
test ambacho hutuonesha idadi, zipo
ngapi.
“Kuna watu huwa wanafika hadi 1000 wakati normal
range haitakiwi kuzidi nne, mgonjwa atalazimika pia kwenda kwa daktari bingwa
wa upasuaji wa mkojo ambaye atamfanyia kipimo maalumu cha ‘cystescopy’.
Kinavyofanyika
“Daktari huingiza mpira wenye kamera kwenye njia ya
mkojo hadi sehemu ya ndani akiangalia ile njia jinsi ilivyo na ile tezidume
ataenda hadi kwenye kibofu pia kwani dalili zile zinaweza kuashiria kuna shida kwenye
kibofu au tezidume,” anasema.
Anaongeza “Vipimo vinapotoka ikiwa vimeonesha kuna
uvimbe kwenye tezidume mgonjwa hufanyiwa kipimo kingine cha biopsy ambacho
daktari huchukua sampuli (kinyama) kutoka kwenye ile tezidume na kuifanyia
uchunguzi maabara.
“Kuna namna mbili za kuchukua sampuli, kwa njia ya
haja kubwa au ndogo kulingana na daktari atakavyoamua, atachonga ile tezidume
kutoa sampuli hiyo na majibu hayo ya maabara ndiyo yatabainisha iwapo ni ukuaji
wa kawaida wa tezidume au saratani,” anasema.
Matibabu
Anasema saratani inapogundulika mapema hutibika na
matibabu ya awali yanaweza kufanyika kuliondoa kabisa lile tezidume.
“Unaweza
kufanyiwa upasuaji kwa njia ya mikono au kwa teknolojia, lakini huwa kuna
‘risk’ ikiwamo kupoteza nguvu za kiume ikiwa baadhi ya mishipa itakatwa kwa bahati
mbaya,” anasema.
Anaongeza “Lakini ikiondolewa bila kubughuzi vitu
vingine hakuna madhara yoyote yanayoweza kujitokeza, ikiwa ugonjwa umeanza
kusambaa kwenda kwenye viungo vingine vya mwili basi huwa tunawapa tiba
nyingine ikiwa ile ya hormonal therapy.
“Hapo tunatibu kwa njia ya vichocheo, ili tezidume
ikue huwa inasimamiwa na homoni ya kiume
iitwayo testosterone inayotengenezwa kwenye korodani kwa amri ya homoni
nyingine inayotengenezwa kichwani kwenye ‘Pituitary gland’.
“Tunafanya upasuaji na kukata mawasiliano, kuzuia
homoni inayotoka kichwani hatua hiyo itafanya tezidume inywee na ile PSA
itashuka, tunaweza pia kufanya upasuaji mdogo wa kuziondoa kabisa zile korodani,”
anabainisha.
Anasema kwa kundoa korodani moja kwa moja tezidume
hunywea na mkojo kuanza kupita kama kawaida.
“Lakini ukiondoa korodani pekee bado kuna homoni ya
testosterone ambayo inatengenezwa kwenye tezi zingine zilizopo juuya figo
(hdrino glands) hivyo itabidi umpatie dawa maalum mgonjwa ili kuzuia homoni
hizo,” anasema.
Anasema wapo wanaume ambao huwa hawapo tayari
kufanyiwa upasuaji kuondoa korodani zao hivyo huwapatia matibabu ya sindano
kila baada ya miezi mitatu kuzia uzalishaji wa homoni hiyo.
“Kuna ambao pia huwa tunawapa dozi ya vidonge
ambavyo humeza kila siku kuzuia uzalishaji wa homoni hiyo,” anasema.
Anasema hata hivyo tiba hiyo hufanya kazi miaka
miwili hadi mitatu baada ya hapo huwa haiwezi tena kuzuilika na tezidume
huendelea kukua.
“Inapofikia hatua hiyo, huwa tunawabadilishia tiba
na kuanza kuwapatia ile ya chemotherapy (tiba ya dripu ya saratani) kwa
mizunguko sita kila baada ya wiki tatu, mgonjwa hupata madhara kadhaa.
“Huchoka mwili, hunyonyoka nywele lakini huwa ni
kwa kipindi kile cha tiba, akimaliza basi nywele huota kama kawaida na kule
kuchoka huisha,” anabainisha.
Tiba
ya mionzi
“Yenyewe hutokea kwa mashine, mashine tuliyonayo
sasa tunatoa mionzi ya variation yenye uwezo wa kuzia ule uzalianaji wa seli” anasema.
Anaongeza “Lakini tayari tumeanza kufunga mashine
mbili zenye uwezo wa kutibu tatizo hili na tunatarajia kutoa tiba hiyo mapema
Januari, mwakani.
“Mionzi ya mashine hizi ipo aina mbili, kuna ya nje
na ndani… huwa wanapandikiza mbegu (gold seeds) ni sindano fulani ambazo huwa
zina-radiate mule ndani na kutibu saratani,” anabainisha.
Athari
Anasema pamoja na hayo ni muhimu muhusika kuwahi
hospitalini kwa uchunguzi ili kutibiwa mapema pindi anapogundulika kuwa na
saratani hiyo.
“Kwa sababu akichelewa kupata matibabu haya, huwa
inakimbilia kwenye uti wa mgongo na kusababisha maumivu ya kiuno, mgongo, miguu
na hatimaye hupooza kabisa na kushindwa kutembea,” anasema.
Anaongeza “Ikiwa hali hiyo itajitokeza na akafika
hospitalini ndani ya saa 72 tunamfanyia tiba ya mionzi ya dharura na tiba hiyo
inatolewa pia pale Hospitali ya Bugando.
Wito
Anawashauri wanamume kujitokeza kufanyiwa uchunguzi
mapema ili kupatiwa matibabu kwa wakati ikiwa wanagundulika kuwa na tatizo
hilo.
“Unaonekana kuwa ni ugonjwa unaoshambulia zaidi
watu wenye hali ya juu ya kiuchumi na kielimu kuliko wa hali ya chini, inaamana
huenda ni mfumo wa maisha wanayoishi kundi hilo.
“Unywaji wa pombe kupitiliza, uvutaji sigara ni
miongoni mwa visababishi vinavyotajwa kusababisha ugonjwa huu,” anasema Dk.
Mseti.
Naye, Mkurugenzi wa Idara ya Kinga wa taasisi hiyo na
Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Saratani, Crispin Kahesa, anasema kila mwaka huwa
wanaona wagonjwa 120 wa saratani ya tezidume.
“Hivyo, tunashauri kwamba ni muhimu mwanaume
kuzingatia ulaji unaofaa hasa vyakula vinavyojenga mwili na kufanya mazoezi ya
viungo kuepuka ugonjwa huo.
“Idadi ya watu wanaougua magonjwa ya saratani
inazidi kuongezeka, mwaka 2016 tuliona wagonjwa wapatao 5200 lakini idadi
imeongezeka kwa asilimia 20 katika mwaka 2017 ambapo tumeona wagonjwa zaidi ya
6,000,” anasema.
Anasema idadi hiyo imeongezeka kwani wamefanya
uhamasishaji mkubwa kwa kushirikiana na vyombo vya habari na wadau mbalimbali
kuwasihi wananchi wajitokeze mapema ili kufanyiwa uchunguzi.
“Wengi wamehamasika na kuja kufanya uchunguzi wa
awali, imechangiwa pia na uboreshaji wa huduma za afya ambazo zimesogezwa
karibu zaidi na wananchi awali zilikuwa zinatolewa hapa ORCI lakini sasa
zinatolewa pembezoni mwa nchi ikiwamo Mwanza, Mbeya, KCMC (Kilimanjaro).
“Kumekuwa pia na ongezeko la hali ya upatikanaji wa
dawa kiasi cha mara kumi zaidi mwaka 2017 kuliko ilivyokuwa 2016.
“Lakini bado tunazidi kuhamasisha jamii ibadilishe
mfumo wa maisha hasa wazingatie suala la ulaji unaofaa, kufanya mazoezi na
kupima afya mara kwa mara ili kuepuka magonjwa ya saratani na mengineyo,”
anasisitiza.
Makala haya kwa mara ya kwanza yametoka Januari 11, 2018 katika gazeti la MTANZANIA ambalo nalitumikia.
Chapisha Maoni