Na Veronica Romwald, aliyekuwa Dodoma
HAIKUWA rahisi Kijiji cha Gwandi, Kata ya Zajirwa, Tarafa
ya Itiso, Wilaya ya Chamwino mkoa wa Dodoma, kufikia lengo la kila kaya kuwa na
choo bora.
Kijiji hicho kina vitongoji 10 vyenye wakazi zaidi ya 4,000
kati ya wakazi hao kulikuwa na kaya 931 na kati kaya zaidi ya 500 hazikuwa
kabisa na vyoo.
Rozina Mpombo ni Ofisa Mtendaji wa kijiji hicho anasema kaya
zaidi ya 300 ndizo zilizokuwa na vyoo ambavyo hata hivyo havikuwa bora.
“Miongoni mwa kaya hizo kuna taasisi 15 pia za serikali,
zisizo za serikali na za dini za kikristo na kiislamu. Taasisi ambazo zilikuwa
na vyoo japo si bora ni tano pekee, hata taasisi yangu ya utawala haikuwa na
choo kabisa,” anabainisha.
Anasema hata hivyo hivi sasa taasisi zote na kaya zote zina
vyoo bora na hilo limewezekana baada ya kuhamasishwa katika kikao maalum
wilayani.
“Tuliitwa wilayani kulikuwa na maofisa tarafa, wadau wa
maendeleo, madiwani, wenyeviti na watendaji tulihamasishwa na tulichefuliwa, nilitoka
na hasira kwanini wananchi wangu wanakula uchafu kwenye kijiji changu nikafanya
maamuzi.
“Nilifika na mwenyekiti wangu nikamsihi aweke siasa pembeni
tukaita vikao vya kijiji na tukaelimisha jamii ili tufikie lengo letu, jamii
ilituelewana na viongozi wa vijiji walituelewa tukashirikiana vema,” anasema.
Anasema wataalamu wa Shirika la Plan International kupitia
mradi wake wa Usafi wa Mazingira Tanzania (Umata) waliungana nao kuwaongezea
nguvu.
Anasema walianza kupitia kaya moja baada ya nyingine
kuhakikisha iwapo kweli wananchi wameitikia wito wa kujenga na kutumia vyoo
bora.
“Awamu hii tukabaini tena kuna kaya zaidi ya 500 ambazo
hazikuwa na vyoo, lakini katika kuhamasisha huko tulipitia changamoto nyingi,”
anasema.
Vitisho
“Siku moja tulikimbizwa na kijana mmoja ambaye alitoka na
panga lake nje na kututishia, tulitoka lakini tulijiuliza tutarudi vipi kwa
sababu hatuwezi kumuacha na lengo letu awe na choo na akitumie.
“Tulirudi tena na tena tukakaa naye tukamuelimisha,
akatuelewa na sasa amejenga choo chake na anakitumia, uelewa wa jamii ulikuwa
mdogo ilituchukua muda mrefu kidogo kuipokea elimu hii,” anasema.
Anasema changamoto nyingine ilikuwa ni umbali kutoka eneo
moja hadi jingine na kwamba kijiji hicho pia kipo mpakani hali iliyofanya
wanakijiji kukwepa suala hilo.
“Yaani unamuelimisha mtu anasema hajengi choo kwa sababu
hayupo kwenye kijiji changu, ikabidi tubadili mbinu na kuwaeleza ujenzi wa vyoo
ni suala la kitaifa na si kijiji pekee na ikiwa mtu hataki kujenga ahame aende
kwingine, wakatekeleza,” anasema.
Anasema sasa wameweka utaratibu wa kuafuatilia kwa ukaribu
kila mara kuhakikisha jamii inaendelea kujenga na kutumia vyoo.
“Na tumeweka amri ni marufuku mgeni yeyote kuhamia kwenye
kijiji chetu ikiwa sehemu anayekwenda kuhamia hakuna choo bora,” anasema.
Anasema suala hilo linasimamiwa kwa ukaribu na maofisa
watendaji wa kijiji hicho.
“Hawezi kuruhusu mgeni kuhamia kama anapokwenda kuishi
hakuna choo bora,” anasema.
Kijiji
kingine
Kijiji cha Chibwe ni mojawapo ya vijiji vilivyosajiliwa
mwaka 2014, kijiji hicho kipo katika Kata ya ya Igandu, Tarafa ya Mvumi, Wilaya
ya Chamwino mkoani Dodoma.
Sospeter Matonya ni Mtendaji wa kijiji hicho kipya anasema
awali wananchi wengi walikuwa hawajajenga vyoo bora kijijini hapo na kwamba
walikuwa hawazingitii suala la kunawa mikono pindi wanapotoka chooni.
“Kijiji kina jumla ya kaya 352, tulifanya ukaguzi tukabaini
kaya 156 pekee ndizo ambazo zilikuwa na vyoo huku kaya 196 hazikuwa na vyoo
kabisa,” anasema.
Anasema wakazi wa kijiji hicho walikuwa wamejenga tabia ya
kutumia choo kimoja zaidi ya kaya moja.
“Yaani unaweza kukuta katika eneo kuna kaya tatu, nne, tano
na kuendelea wote wanatumia choo kimoja, lakini baada ya Mkuu wa Wilaya kwa
kushirikiana na Shirika la Plan International kupitia mradi wa Umata
tulihamasika kujenga choo kwa kila kaya.” Anasema.
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu
Anaongeza “Tulianza kwanza kuhamasishwa sisi viongozi baadae tukatoka na kwenda kuhamasisha jamii kwamba kila kaya ijenge na kutumia choo chake.
Anaongeza “Tulianza kwanza kuhamasishwa sisi viongozi baadae tukatoka na kwenda kuhamasisha jamii kwamba kila kaya ijenge na kutumia choo chake.
“Tena kijengwe kwa kuzingatia ubora unaotakiwa, kiwe na
mlango, shimo lililosakafiwa, kiezekwe na kiwe na kibuyu chirizi,” anasema.
Anasema baada ya jamii kupewa elimu juu ya umuhimu wa
matumizi ya vyoo bora na kunawa mikono baada ya kutoka chooni sasa hivi zaidi
ya kaya 200 kijijini hapo zimejenga vyoo bora.
“Hatukutumia nguvu kubwa wa gharama tulichofanya ni
kuwahamasisha wananchi, tuliwahimiza kwamba yule ambaye hatajenga choo
tutampeleka mahakamani basi wakahamasika na kujenga vyoo vyao wenye kwa kasi
kubwa na sasa wanavitumia,” anabainisha.
Janeth Mganga ni mmoja wa wananchi katika kijiji hicho
anasema baada ya kuhamasika alishauriana na mumewe wakajenga choo wakaweka
ukuta wakaezeka vizuri wakaweka na milango,
“Tukaanza kutumia choo chetu na zile familia zingine nne
zikaona vema na kufuata nyayo zetu, zikajenga vyoo vyao,” anasema.
Anaongeza “Baada ya kukamilisha choo changu, kwa kuwa
wanakijiji wenzangu walikuwa wakinicheka kwa kuwa sikuwa na choo, niliamua
kuandika ujumbe maalum kwenye kuta zake.
“Niliweka tangazo, yeyote nitakayemuta nitamkamata na
kumchukulia hatua, nikaandika pia ‘usione vimeng’aa vimegharamikiwa, jenga choo
kwa familia yako, basi wale ambao hawakuwa wamejenga vyao walihamasika na
kujenga pia,” anasema.
Mkataba
Isabela Mgombaheka ni Mtendaji wa kijiji cha Msonjile B na
Kaimu Mtendaji wa kijiji cha Msonjile A ambavyo vipo Kata ya Sejeli Tarafa ya Kongwa Wilaya ya Kongwa.
Anasema wao waliamua kutumia mbinu ya kuwaandikisha mkataba
maalum wa hukumu ya ujenzi wa vyoo wakazi wa vijiji hivyo ili kufikia lengo la
kila kaya kujenga na kutumia choo bora.
“Kijiji cha Msonjile B kina wakazi wapatao 3048 kaya 581
taasisi za kidini na utawala saba,” anasema.
Anasema kabla ya kuanza kwa mradi wa Umata katika kijiji
hicho kulikuwa na kaya 200 ambazo hazikuwa zimejenga vyoo bora.
“Ilituchukua muda mrefu kuishawishi jamii katika kijiji
hiki kujenga na kutumia vyoo bora, kwa sababu wengi hapa ni wafugaji na
hawaamini kabisa katika ujenzi wa vyoo kwa sababu wengi wamezoea kuishi kwa
kuhamahama kutoka eneo moja hadi jingine wakitafuta malisho ya mifugo yao,”
anasema.
Anaongeza “Tulijitahidi kuhamasisha jamii kuhusu umuhimu wa
matumizi ya vyoo bora na unawaji mikono kupitia mradi wa Umata.
“Tulifanya kazi hiyo kwa kushirikiana na kamati za afya za
kitongoji za kijiji hatimaye April 11, mwaka tulitambulika kuwa kijiji
kilichokidhi vigezo kuwa na vyoo kundi A, B na C,” anasema.
Anasema wakati akiwa Mtendaji wa kijiji cha Msonjile B,
alipokea barua ya kukaimishwa kijiji cha Msonjile A ambako pia alikuta kaya 59
ambazo hazikuwa na vyoo,
Waziri Ummy alipofanya ziara mkoani humo hivi karibuni kukagua utekelezaji wa awamu ya kwanza ya kampeni ya usafi wa mazingira (NIPO TAYARI)
Mkakati
Mkakati
Anasema walitumia mbinu ya kutoa elimu kwa jamii na kufanya
ufuatiliaji wa mara kwa mara ili kujihakikishia kwamba jamii imejenga vyoo
bora.
“Ilibidi tutumie mbinu hiyo na nyingine nyingi ili
tufanikishe lengo hasa kupeleka elimu kwa jamii kuwajengea uwelewa wa umuhimu
wa matumizi ya vyoo.
“Lakini pia tuliandaa mkataba huo maalum ambao
tuliwasainisha wale ambao tuliwabaini hawana vyoo na tuliwapa siku maalum
wahakikishe wamejenga kabla ya siku hizo kwani zikiisha tutawafikisha
mahakamani kwa mujibu wa mkataba huo,” anasema.
Anaongeza “Wengi walihamasisha na kujenga vyoo kabla ya
kuisha kwa muda ambao tuliwapangia kulingana na mkataba tuliowasainisha.
“Tulitumia pia sheria ndogondogo za vijiji zilizopo, kwa
kutumia sheria hizo tuliwakamata wale ambao walifanya uzembe na kuwatoza faini
na fedha hizo zilitusaidia kuwajengea vyoo wale ambao walikuwa hawajiwezi
kabisa.
“Kwa mfano, tuliweza kumjengea choo kikongwe mmoja, mlemavu
mmoja na kipofu mmoja na wale ambao tuliwatoza faini tuliwapa mkataba kwa
kuwapa muda maalum ili wahakikishe wanajenga choo,” anasema.
Anasema kwa kuwa choo bora kinahitajika kuwa kimesakafiwa
vema na kwa kuwa jamii nyingi hazikuwa na uwezo wa kifedha walitumia mbinu
nyingine mbadala.
“Tulinunua mifuko ya sementi kwa kushirikiana na kamati ya
afya na wadau wetu wa Umata, tukazileta kijiji na kuwauzia wananchi kwa bei
nafuu kabisa ili wale ambao hawakuwa na uwezo waweze kumudu gharama,
tukafanikiwa katika hilo,” anasema.
Anaongeza “Sasa watu wamehamasika na wameelewa umuhimu wa
kujenga na kutumia vyoo bora bila kusahau unawaji mikono mara baada ya kutoka
chooni.
Mafanikio
Mkurugenzi wa Umata, Nyanzobe Malimi anasema wamefanikiwa
kuhamasisha jamii kujenga vyoo na kwamba tayari asilimia 65 ya kaya vyoo vyao vimeboreshwa.
“Haikuwa kazi rahisi kufikia kiwango hicho, kati ya kaya
hizo asilimia 31 ndizo ambazo zina vyoo bora zaidi yaani kile ambacho kina
sakafu inayoweza kusafishika na mlango,” anasema.
Anasema hadi sasa ni asilimia nne tu ya kaya ambazo hazina
kabisa vyoo.
Anasema jamii sasa inaona umuhimu wa kunawa mikono hasa
baada ya kutoka chooni na kwamba hilo wamekuwa wakilizingatia ili kujikinga
dhidi ya magonjwa yatokanayo na hali ya uchafu.
“Haikuwa rahisi kufikia mafanikio haya, tumepitia
changamoto nyingi, kwa mfano kuna maeneo tunakwenda unakuta mwenyekiti wa
kijiji hana choo inakuwa ngumu kumuhamasisha mwananchi wake kujenga choo wakati
yeye mwenyewe hana.” Anabainisha.
Anaongeza “Changamoto nyingine zilijitokeza katika maeneo
ambako tulikuwa tunakwenda na kukuta viongozi wanatoka vyama tofauti vya siasa.
“Unakuta diwani anakaa pembeni na kuacha kuhamasisha
wananchi wake kujenga vyoo bora, ilitupa shida lakini tunashukuru jamii
ilitusikiliza na kutuelewa.
“Sasa hivi vijiji 76 vimefikia kiwango cha kuishi kwenye
makazi safi na salama yasiyo na kinyesi, tunasema ‘Open Defecation Fee (ODF)’
na wanapewa vyeti na Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na
Watoto kuvitambua,” anasema.
Makala haya kwa mara ya kwanza yametoka Januari 11, 2018 katika gazeti la MTANZANIA ambalo nalitumikia
Chapisha Maoni