Recent Post


 


moja

Responsive Advertisement
Wauguzi wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) wakiwasaidia wagonjwa kupanda katika gari tayari kwa safari ya kuhamia Hospitali ya Mloganzila hivi karibuni.

Na Veronica Romwald, Dar es Salaam

“Sitaki mnipeleke huko mnapotaka niende, mimi nilikuja hapa Muhimbili kutibiwa kama mmeshindwa bora ndugu zangu wanichukue na kunirudisha nyumbani,”.

Ni kauli ya mmoja wa wagonjwa ambaye alikuwa akisukumwa na wauguzi wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) kupelekwa katika gari la wagonjwa tayari kwa safari ya kuhamishiwa kwenda Hospitali ya Chuo Kikuu Cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili kampasi ya Mloganzila (MAMC) – Mloganzila.

Mgonjwa huyo ambaye hakutaka kutajwa jina lake gazetini, anasema hajui kwanini anahamishwa kwenda huko na anazidi kulalama kwamba arudishwe nyumbani kwake.

“Usijali mama, unapopelekwa (Mloganzila) ni pazuri zaidi ya hapa unapotolewa (Muhimbili), hautakwenda peke yako utakwenda na sisi (wauguzi) tutakuwa pamoja hadi utakapopona na kuruhusiwa kurudi nyumbani,” anaelezwa na Muuguzi mmoja aliyekuwa akisukuma kitanda hicho.

Nashuhudia wagonjwa waume kwa wake wakiendelea kutolewa katika wodi hiyo na kusaidiwa kupanda katika gari aina ya costa yenye namba T 563 CZX tayari kwa safari.

“Humo ndani mnatakiwa kupanda na msaidizi (ndugu) mmoja, hakikisheni kila mmoja amepanda na ndugu yake,” anasema Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano ya Umma na Wateja Muhimbili, Aminiel Aligaesha aliyekuwa hapo kuhakikisha kila kitu kinakwenda sawa sawa.

“Mwishoni mwa mwaka jana Rais John Magufuli akizindua MAMC alisema baadhi ya wagonjwa waliolazwa Mwaisela wahamishiwe Mloganzila ili kupunguza msongamano,” anasema.

Anasema Muhimbili walianza kutekeleza agizo hilo mwishoni mwa Desemba, mwaka jana.

“Jengo hili lina vitanda 240 na wakati wote waliolala waliokuwa wapatao 250 hadi 300 unakuta wengine walilala wawili au chini.

“Wagonjwa walikuwa hawapungui humu ndani, na hiyo ndiyo sababu kuu iliyofanya wapunguzwe kutoka hapa kwenda Mloganzila, ndani ya mwezi mmoja tutakuwa tumepeleka wagonjwa wapatao 170,” anasema. 

Wauguzi wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) wakiwasaidia wagonjwa kupanda katika gari tayari kwa safari ya kuhamia Hospitali ya Mloganzila hivi karibuni.

Anaongeza “Muhimbili tunashirikiana kwa ukaribu na Mloganzila na tumepanga madaktari wetu zamu kuhakikisha wanakwenda huko kutoa huduma.

“Mloganzila ina vifaa vya kisasa na tunapofanya matengenezo vya kwetu tunasitisha huduma na kuwapeleka Mloganzila wagonjwa, hadi sasa tumewafanyia vipimo wagonjwa wapatao 30 huko.

“Hivyo, niwatoe hofu wagonjwa wanaohamishiwa Mloganzila kwamba hatua hii haitaathiri matibabu yao kwa namna moja au nyingine, watapa huduma zote zinazostahili,” anasisitiza.

Hayo yanajiri nje ya wodi ya Mwaisela Januari 10, mwaka huu saa kumi jioni ambapo nimefika na waandishi wenzangu punde tukitokea MAMC ambako Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu alifanya ziara.

Waziri Ummy anasema serikali kupitia Wizara hiyo imehamisha rasmi Idara ya Magonjwa ya Ndani (internal medicine) ya Muhimbili katika kampasi ya Mloganzila (MAMC).

“Kutokana na hatua hiyo, tumeagiza madaktari bingwa 35 wa Idara hiyo kuhamia Mloganzila mara moja pamoja na wagonjwa  wapatao 270 waliolazwa katika idara hiyo kwa matibabu,” anabainisha.

Anasema hospitali hiyo ya MAMC sasa inatoa huduma saa 24 na kwamba ina vifaa vya kisasa vya kutosha na madaktari bingwa wa kutosha.

“Tunahamisha madaktari wote wa Idara hiyo, wauguzi pamoja na wataalamu wengine na kwa hatua hiyo. Naiagiza Muhimbili kuhakikisha wanakarabati jengo la Mwaisela wodi namba mbili hadi saba, wagonjwa watakaobaki huko ni wale walio mahututi,” anasisitiza. 

Waziri Ummy akizungumza jambo na Naibu Makamu Mkuu wa Chuo na hospitali ya MAMC, Profesa Said Abood hivi karibuni alipotembelea MAMC

Uhamisho Mkoani

Waziri Ummy anasema serikali imeanza kuwapangua madaktari bingwa 20 wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), kwenda katika Hospitali za rufaa za Mikoa.

Kutokana na hatua hiyo anawataka waganga wakuu wa Mikoa na wafawidhi katika Hospitali za Kanda kuanza kuwapeleka wagonjwa wa Magonjwa ya nje Mloganzila na si Muhimbili.

“Tumejipanga kuhakikisha hospitali zote za Mikoa zinakuwa na madaktari bingwa katika kada nane ikiwa ni pamoja na daktari bingwa wa magonjwa ya uzazi na wanawake, watoto, Magonjwa ya jumla, masuala ya radiolojia.

“Tumepokea rasmi Hospitali za Mikoa na tumefanya ya kutathimini  miundombinu iliyopo na madaktari bingwa waliopo kwa ajili ya kuanza kuwatawanya,” anabainisha.

Anaongeza “Hospitali ya Muhimbili itabaki kuwa Hospitali ya kibingwa kwa magonjwa yanayohitaji upasuaji, ingawa hivi sasa bado wataendelea pia kushirikiana kutibu pia magonjwa ya ndani.

Athari zake

Katika Kongamano la 49 la Afya Kitaifa na Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Chama cha Madaktari Tanzania (MAT), Rais wa chama hicho, Dk Obadia Nyongole alisema Tanzania inakabiliwa na uhaba wa madaktari bingwa kwa kiwango cha asilimia 82.

Alisema ili kukidhi mahitaji wanahitaji madaktari bingwa 2,453 wa fani mbalimbali hata hivyo waliopo hivi sasa ni 451 pekee ambao wanahudumia nchi nzima.

Kutokana na hali hiyo, MTANZANIA lilihitaji kujua hatua iliyochukuliwa na serikali kuwahamisha madaktari bingwa waliopo Muhimbili, je ina athari gani.

Chama cha Madaktari

Dk Obadia kwanza anaipongeza serikali kwa hatua hiyo hata hivyo anasema suala la kuboresha ni mtambuka na kwamba linategemea vitu vingi.

“Madaktari hawa wanaotolewa Dar es Salaam huko wanapotoka wanaacha uhaba, nchi yetu ina uhaba mkubwa wa madaktari bingwa hivyo suluhu ya kudumu ni kusomesha madaktari bingwa wa kutosha zaidi.

“Kwa hiyo tunaiomba serikali iendelee kusomesha madaktari katika ‘level’ ya ubingwa,” anasisitiza.

Anaongeza “Upatikanaji wa vifaa tiba ni kitu muhimu ambacho nacho lazima kitazamwe na kufanyiwa kazi, ni mapema mno kusema madaktari wamelichuliaje lakini sisi kama chama tulikaa vikao vya ndani na tukalizungumza.

Mdahalo

“ Tuliita mdahalo wa kitaaluma na madaktari waliopo Dar es Salaam,  lakini kwa bahati mbaya kutokana na sababu zilizo nje ya uwezo wetu kongamano la kitaalamu halitaweza kufanyika.

“Hata hivyo tunaamini madaktari wataendelea kutupa maoni hilo liweze kufanya na kuwa na tija zaidi kwa Taifa na naamini serikali itaendelea kuweka milango wazi ili tuendelee kushauriana zaidi na sisi wanataaluma juu ya njia nzuri zaidi ya kuitumia kuhakikisha kwamba uhamisho huu hauleti sintofahamu kati ya wanataaluma na serikali ilivyopanga. 

Mfano hai

Dk. Nyogole (pichani) anasema wanayo mifano hai wa mwaka 2011/12 kwamba kuna madaktari waliotolewa na kupelekwa kwenye baadhi ya Hospitali za Mikoa hata hivyo walipofika huko mamlaka za ajira zilisema hazina bajeti za mishahara yao.

“Walihamishiwa kule bila wao kuandaliwa kwa hiyo mazingira yakawa si rafiki kwa wale madaktari ikabidi watafute sehemu zingine za kwenda kufanya kazi,” anasema.

Ushauri  

Dk. Obadia anasema ni muhimu wale ambao watawapokea madaktari hao wahakikishe wanakuwa na taarifa sahihi na kuweka mazingira rafiki kwao.

“Sisi ni chama cha kitaaluma tupo tayari kwa majadiliano na serikali, tutawasiliana na mamlaka husika ili kuweza kujadiliana namna gani hilo litafanyika vizuri zaidi liwe na tija kwa Taifa, jamii tunayohudumia na kwa madaktari wenyewe,” anasema

Waziri awatoa hofu

Waziri Ummy anasema madaktari watakaohamishwa, watahimishwa pamoja na viwango vyao vya mishahara waliyokuwa wakipatiwa awali.

“Katika hili niwatoe hofu kabisa, ni kweli pia kwamba tuna uhaba wa madaktari bingwa  lakini tunafundishwa  kuwatawanya wachache waliopo ili kuhakikisha kila Mtanzania anapata huduma za kibingwa.

“Kwa sababu, kwa mfano... daktari bingwa wa wanawake Bugando anaona zaidi ya wagonjwa 20lakini wa Muhimbili anaona wagonjwa watatu na hospitali ya Rufaa ya Tanga hakuna daktari hata mmoja, lazima tuwatawanye waliopo,” anasisitiza.

Hatua zaidi

Naibu Makamu Mkuu wa Chuo na hospitali ya MAMC, Profesa Said Abood anasema hivi sasa kila mwaka chuo Cha Muhas, Bugando vinazalisha madaktari bingwa wapatao 150 hadi 180. 

“Tunatarajia madaktari hao watakaotoka vyuoni watasaidia kukabili uhaba wa madaktari bingwa ulipo hivi sasa nchini,” anasema.

Anasema pamoja na hayo wamejipanga kuhakikisha wanatoa huduma bora kwa wagonjwa wote watakaofika na wale watahamishiwa katika hospitali hiyo kutoka Muhimbili.

“Wagonjwa tutakaokuwa tunatibu ni wale ambao watakuwa hawahitaji huduma za upasuaji, magonjwa hayo kitaalamu huitwa magonjwa ya ndani kama vile malaria, figo, moyo, ngozi na mengineyo,” anasema.

Picha zote na Veronica Romwald

Makala haya kwa mara ya kwanza yametoka kwenye gazeti la MTANZANIA ambalo pia nalitumikia Januari 18, 2018 

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement