Recent Post


 


moja

Responsive Advertisement
*Matokeo yabainisha sababu.

Na Veronica Romwald, Dar es Salaam

MAGONJWA yasiyo kuwa ya kuambukiza (NCD’s) ni yale ambayo mtu anapoyapata huwa hawezi kumwambukiza mwingine na ataishi nayo hadi siku atakapofariki dunia.

Kundi hilo linajumuisha magonjwa ya saratani, magonjwa ya moyo, magonjwa sugu ya njia ya hewa, seli mundu (sickle cell disease), magonjwa ya akili na dawa za kulevya, figo, kisukari, ubongo, macho na mengineyo.

Utafiti uliofanywa mwaka 2005 duniani na Shirika la Afya Duniani (WHO) ulionesha kati ya vifo milioni 58 vilivyokuwa vimetokea, vifo milioni 35 vilitokana na magonjwa yasiyo kuwa ya kuambukiza.

Nchini Tanzania utafiti uliofanyika katika wilaya nne kuanzia mwaka 1994 hadi 2002 ulionesha asilimia 18 hadi24 ya vifo vilivyokuwa vimetokea, vilitokana na magonjwa yasiyo ya kuambukiza.

Magonjwa hayo yanatajwa kuchangia asilimia 27 ya vifo vyote duniani na tafiti zinaonesha yanazidi kuongezeka hasa katika nchi zilizopo chini ya Ukanda wa Jangwa la Sahara, Tanzania ikiwamo.

WHO linakadiria kuwa asilimia 20 ya vifo vyote vilivyotokea nchini mwaka 2005 vilitokana na magonjwa yasiyo ya kuambukiza.

Utafiti huo unabainisha magonjwa ya moyo yalichangia vifo kwa asilimia tisa, saratani asilimia nne, mfumo wa hewa asilimia mbili, kisukari asilimia moa na magonjwa mengine sugu asilimia nne.

Utafiti wa viashiria vya magonjwa yasiyo ya kuambukiza uliofanywa na Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa kushirikiana na Taasisi ya utafiti wa magonjwa ya binadamu (NIMR) mwaka 2012 ulionyesha kuna ongezeko kubwa la viashiria vinavyosababisha magonjwa yasiyo ya kuambukiza.

Serikali za nchi mbalimbali sasa zimeelekeza nguvu zake katika kufanya kampeni kuelimisha jamii kuhusu magonjwa hayo ambayo yanatajwa kugharimu maisha ya watu wengi.

Magonjwa hayo yanaweza kuepukika kwa watu kuzingatia ulaji unaofaa, kufanya mazoezi, kupima afya mara kwa mara, matumizi yanayostahili ya dawa.
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu

Changamoto kubwa inayotajwa katika kukabili magonjwa haya ni gharama kubwa za matibabu ambazo mtu hukabiliana nazo hasa pale anapokuwa hana bima ya afya.

Mgonjwa

Hamis Ibrahim Mkazi wa Singida anamuuguza mtoto wake ambaye amefanyiwa upasuaji katika taasisi hiyo hivi karibuni.

“Mwanangu aligundulika kuwa na tatizo la moyo mwaka 2004 kabla ya kufika hapa nilizunguka hospitali nyingi mno lakini tatizo halikugundulika.

“Hadi pale nilipokwenda katika hospitali moja ya rufaa ipo huko Manyoni ndiko ikagundulika kwamba ana tatizo,  ‘valve’ zake zilikuwa zina-fail kusukuma damu na moyo wake ulionekana kuwa unatanuka,” anasema.

Anasema awali ilimgharimu fedha nyingi kulipia matibabu ya mtoto wake huyo ikafika wakati akashindwa kumudu gharama hizo.

“Nilikuwa natumia hadi zaidi ya Sh 200,000 kila nilipomleka  kufanyiwa uchunguzi pamoja na dawa, nikashauriwa kukata bima nikakata toto afya ya NHIF ambayo kidogo naona inanipunguzia mzigo wa gharama za matibabu,” anasema.

Anaongeza  “Nashukuru serikali naiomba isogeze huduma hizi karibu zaidi na jamii wawasaidie wanaougua ugonjwa huu wapo mikoani pia wengine hawawei kuja huku, ikiwezekana kila mkoa upate haya matibabu.

Utafiti

Pedro Pallangyo ni Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) ambaye hivi karibuni amefanya utafiti kujua hali halisi na changamoto zinazowakabili wagonjwa wa moyo nchini.

MTANZANIA limefanya naye mahojiano na anaeleza kwa kina kile alichokibaini kupitia utafiti wake huo, karibu.

Dk. Pallangyo anasema kwa kawaida wagonjwa wanaolazwa hospitalini hapo hupatiwa dawa zinazostahili kutibu magonjwa ya moyo yanayowakabili.

“Lakini kati yao wapo ambao wanaporuhusiwa kurejea nyumbani hushindwa kununua dawa wanazokuwa wameandikiwa na madaktari wanazotakiwa kuzitumia  kipindi chote wanapokuwa nyumbani kabla ya kurejea tena hospitalini,” anasema.

Anaongeza “Matokeo yake, kama wana tatizo la moyo kushindwa kufanya kazi, wakilazwa hospitalini huwa na hali nzuri lakini wakirudi nyumbani hali hubadilika na kuwa mbaya kuliko awali kwa sababu hawatumii dawa.

“Kutokana na hali hiyo wengi hurudishwa hospitalini, kwa kipindi cha miezi sita tulifanya utafiti huu kwa wagonjwa 459 kuangalia mwenendo wao wa matumizi ya dawa na mambo mengineyo,” anasema.
Dk. Pedro (anayezungumza pichani) anasema utafiti huo ulihusisha wagonjwa waliokuwa na umri wa kati ya miaka 46 na kuendelea na kwamba silimia 57 walikuwa wanawake huku asilimia 43 ikiwa ni wanaume.

“Kati ya wagonjwa hao asilimia 22 walikuwa na bima ya afya  na asilimia 68 walikuwa wakiishi katika maeneo ya mijini,” anasema.

Matokeo

Dk. Pallangyo ambaye pia ni Mkuu wa Kitengo cha Utafiti na Mafunzo wa JKCI anasema katika utafiti huo walibaini asilimia 80 ya wagonjwa wote 459 waliofanyiwa utafiti huo walikuwa na matumizi mabaya ya dawa.

“Hawakutumia dawa kama inavyotakiwa na walivyokuwa wameelekezwa na wataalamu na hiyo ilikuwa kisababishi kikubwa kilichochangia kulazwa mara kwa mara na kuwa kwenye hatari ya kupoteza maisha,” anasema.

Daktari huyo anasema matokeo ya utafiti huo yalibainisha kwamba asilimia 85 ya wagonjwa waliohojiwa walieleza sababu kubwa iliyowapelekea kuacha kuzingatia matumizi ya dawa ni kukosa fedha za kununulia dawa hizo.

“Sababu nyingine ambayo ilitajwa na kushika nafasi ya pili ilikuwa ni usahaulifu, baadhi ya wagonjwa walieleza kwamba kuna wakati walisahau kumeza dawa walizoandikiwa,” anasema.

Anasema walitumia tool ya Morsw (kipimo cha kitaalamu) kinachoshauriwa na Shirika la Afya Duniani (WHO) katika kufanya tafiti za namna hiyo.

Sababu

Anasema sababu kubwa ambayo imeonekana kuchangia hali hiyo ni gharama za ununuzi wa dawa hizo ambapo utafiti unaonesha asilimia 87.3 ya wagonjwa waliohojiwa walieleza sababu hiyo.

“Kuhusu usahaulifu ilipatikana asilimia 53.9… utaona matokeo haya hayawezi kuleta jumla ya asilimia 100 na hii ni kwa sababu katika wagonjwa tuliohoji wengine walikuwa na sababu zaidi ya moja,” anasema.

Dk. Pallangyo anasema kati ya wagonjwa waliohojiwa asilimia 34.4 walieleza kuwa waliacha matumizi ya dawa kutokana na wingi wa dawa walizokuwa wameandikiwa kwa ajili ya kuzitumia kutibu tatizo walilonalo.

“Yaani kutokana na ule wingi walilazimika kuacha baadhi ya kupunguza au kupumzika, na asilimia 26 waliacha matumizi ya dawa kutokana na uzembe,” anasema.

Anasema kwa kupata matokeo hayo walijaribu kuangalia kwa kina nini hasa vilikuwa visababishi vilivyochangia wagonjwa hao kuwa na uzingatiaji mdogo wa matumizi ya dawa walizotakiwa kutumia.
“Tulibaini umri haukuwa tatizo, jinsi haikuwa tatizo lakini kwa upande wa elimu tulibaini kulikuwa na tatizo, wagonjwa waliokuwa na elimu ndogo (Elimu ya Msingi kushuka chini) walikuwa na uzingatiaji mdogo kulinganisha na wagonjwa waliokuwa na kiwango cha Elimu ya Msingi na kuendelea,” anasema.

Anasema kwa upande wa kigezo cha ajira nacho kilikuwa ni sababu kwani utafiti ulibaini wale waliokuwa hawana ajira ya kuwaingizia kipato walikuwa na uzingatiaji mdogo wa matumizi ya dawa kuliko waliokuwa na ajira ya kueleweka.

Anasema kwa mujibu wa matokeo ya utafiti huo wagonjwa waliokuwa wanaishi katika maeneo ya vijijini tulibaini walikuwa na uzingatiaji mdogo wa matumizi ya dawa kulinganisha na wale waliokuwa wakiishi mijini.

Anaongeza “Aidha, wagonjwa ambao hawakuwa na bima walikuwa na uzingatiaji mdogo wa matumizi ya dawa mara nane zaidi ya wale ambao walikuwa na bima.

“Hivyo vigezo vya msingi ambavyo tuliona vilichangia hali hiyo, ni elimu duni, tatizo la ajira, makazi wanakoishi na kutokuwa na bima afya,” anabainisha Daktari huyo ambaye pia ni mshindi wa tuzo ya watafiti vijana Barani Afrika kwa mwaka 2017.

Hali mbaya

Dk. Pallangyo anasema katika utafiti huo walienda mbali zaidi na kuangalia maendeleo ya wagonjwa waliolazwa mara kadhaa baada ya mahojiano ya awali.

“Tulibaini baada ya mahojiano ya awali, wagonjwa ambao  hawazingatii matumizi ya dawa kama walivyotakiwa wana uwezekano wa kulazwa mara kwa mara huwa ni asilimia 70 kuliko wale ambao huzingatia,” anasema.

Anaongeza “Matokeo yanaonesha pia wagonjwa ambao huwa na uzingatiaji mbaya wa matumizi ya dawa hali inayopelekea kulazwa mara kwa mara hospitalini wapo kwenye hatari ya kufariki dunia mara tatu zaidi ya wale wanaozingatia matumizi sahihi ya dawa.

“Hii tuliibaini baada ya kuwafuatilia kwa ukaribu wagonjwa hao ambapo kati yao walikuwapo ambao walipoteza maisha ndani ya miezi sita ya utafiti huu,” anasema.

Dk. Pallangyo anasema kutokana na matokeo ya utafiti huo inawezekana sababu hizo zinachangia pia vifo vya wagonjwa kwa kutozingatia matumizi sahihi ya dawa katika magonjwa mengine.
Madaktari wa JKCI na wenzao wa Hospitali ya Apolo, India wakishirikiana kumfanyia upasuaji mgonjwa wa moyo kwa kumuwekea milango miwili ya moyo ya chuma

Umasikini huchangia?

“Huenda hii inatokea kwa sababu, jamii nyingi bado ni masikini, kusema ule ukweli bado wananchi hawawezi kumudu gharama  za kutibu magonjwa yasiyo kuwa ya kuambukiza,” anabainisha.

“Ukicha matokeo ya utafiti huu, sasa hivi tunafanya utafiti mwingine ambapo tayari tumehoji wagonjwa 500 na lengo ni kuwafikia 1,000 tukiangazia hasa kigezo hiki cha gharama na hali ya kipato cha mwananchi.

“Tunatarajia kukamilisha utafiti huu na kutoa matokeo yake ifikapo Januari, mwakani, lakini kwa kuzingatia utafiti huu tuliokamilisha, tunaishauri Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto pamoja na wadau mbalimbali wa sekta ya afya kwamba lazima watafute mbinu ama njia mbalimbali kuhakikisha kila mwananchi anakuwa na bima ya afya.

“Ifike mahali bima ya afya iwe ni haki ya msingi kwa kila mwananchi badala ya wachache tu kuwa nayo, maana kwa matokeo haya inaonesha wazi kwamba mtu akiwa na bima ya afya anakuwa hana ‘stress’ za jinsi gani atamudu gharama za matibabu na dawa,” anasema.

Dk. Pallangyo anaongeza “Lakini pia itafakari jinsi gani kila mwananchi atakayekata bima ya afya atakuwa analipa kwa sababu sisi wafanyakazi tunakatwa kwenye mshahara lakini kuna kundi la watu ambao wamejiajiri wenyewe katika ajira ambazo si rasmi.

“Tunaona pia kuna haja zaidi ya kuwapatia elimu wananchi kuhusu umuhimu wa kukata bima ya afya na kuzingatia matumizi ya dawa kulingana na walivyoelekezwa na wataalamu wa afya katika kutibu magonjwa mbalimbali,” anasema Daktari huyo.

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement