Recent Post


 


moja

Responsive Advertisement
Na Veronica Romwald, Dar es Salaam

TATOO ni michoro ambayo huchorwa sehemu mbalimbali katika mwili wa binadamu, vijana ndilo kundi ambalo hupendelea zaidi kuchora michoro hiyo.

Michoro hiyo hubeba ujumbe mbalimbali kulingana na matakwa ya wale waliojichora.

Juma Kassim kijana mwenye umri wa miaka 28 mkazi wa Sinza Kijiweni amechora tattoo ya jina la mwenzi wake shingoni mwake.

“Nampenda mpenzi wangu niliamua kuchora tattoo hii shingoni ili kumuonesha jinsi gani nampenda na namthamini,” anasema.

Kassim anasema hakusudii kuja kuifuta tattoo hiyo kamwe katika maisha yake.

“Umesema ikiwa itatokea nikaachana na mpenzi wangu kwamba nitaifuta au la, siwezi kuifuta hata itokee jambo gani, hii nimeichora itakaa milele katika mwili wangu,” anasema.

Maria Elius anasema yeye amechora tattoo kwa kuandika jina la mama yake.

“Mama yangu amefariki mwaka 2013 nilijihisi mpweke mno, baba yangu simjui, sijawahi kumuona… nilielezwa na mama kwamba alimkimbia nikiwa bado sijazaliwa.

“Hivyo, alinikataa nikiwa tumboni mwa mama, nikaishi bila kumjua baba yangu hadi leo, mama alipofariki nilibaki kwa babu yangu, mwaka 2015 nikaamua kuchora tattoo hii,” anasema.

Anasema kila anapoitazama tattoo hiyo aliyoichora katika mkono wake wa kulia anahisi yupo karibu na mama yake.

“Najua si kweli lakini najihisi vizuri pale ninapomkumbuka naitazama tattoo hii najisikia faraja,” anasema.

Daktari

Hivi karibuni MTANZANIA limefanya mahojiano maalum na Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Ngozi wa Hospitali ya Taifa Muhimbili, Annete Kissongo.

Anasema vijana wengi hupenda kujichora tattoo katika miili yao bila kujua kwamba zinaweza kuwasababishia madhara mbalimbali.

“Kwa kawaida, mtu anapochora ile tattoo mwilini mwake ile rangi huenda moja kwa moja hadi katika sehemu ya ndani ya ngozi iitwayo dermis,” anabainisha.

Athari zake

Anasema tattoo huweza kusababisha magonjwa ya maambukizi hasa ikiwa chombo cha kuchorea kitatumika pasipo kusafishwa vema na kutumiwa na wengi.

“Kile chombo kinachotumika ikiwa kimetumika kwa kundi kubwa la watu, kama wana magonjwa ya maambukizi kwa mfano HIV, homa ya ini na mengineyo huwa inaongeza uwezekano wa kuambukizana magonjwa hayo na mengineyo,” anasema.

Dk. Anette anasema wakati mwingine mtu huweza kupata maambukizi ya bakteria (bacteria infection).
Anaongeza “Ile rangi inayotumika kuchora tattoo inaweza kumsababishia muhusika kupata allege (mzio).

Anasema athari huwa kubwa zaidi kwa muhiska ikiwamo kupata makovu makubwa yasiyokuwa ya kawaida kitaalamu yanaitwa keloids.

“Makovu hayo huwa makubwa kuliko kidonda cha kawaida au mchoro wa kawaida wa tattoo, haya hutokea zaidi kwa watu weusi na huharibu kabisa ule mwonekano wa ngozi ya muhusika,” anabainisha.

Anasema wapo ambao makovu hayo hufika mahali na kuanza kupungua hata hivyo wengi huwa yanaongezeka ukubwa.

Utafiti

Inaelezwa tattoo inaweza kumsababishia muhusika kupata saratani.

Hiram Castillo wa Kituo cha Radiation cha nchini Ufaransa ni miongoni mwa waandishi wa utafiti huo.

Wanasema kwamba kemikali za wino wa tattoo huweza kusafiri katika damu na kukusanyika katika mfumo wa lymph.

Hali hiyo huufanya mwili kuvimba na hivyo kuzuia uwezo wake wa kupambana na maambukizi dhidi ya magonjwa mbalimbali.

Watafiti hao wanataja kemikali ya titan-dioksaidi ambayo hutumiwa kuunda wino mweupe ni miongoni mwa kemikali zinazoongeza hatari ya mtu kupata saratani.

“Mtu anapotaka kupata tattoo, mara nyingi huwa makini sana katika kuchagua sindano ambazo hazikutumika awali lakini hakuna mtu anayeangalia kemikali ya rangi, lakini utafiti wetu unaonesha wanapaswa kufanya hivyo,” anasema Castillo.

Wanasayansi hao wa Ufaransa na Ujerumani walitumia X-rays na kipimo cha fluorescence kuchunguza chembe ndogo, waliripoti ushahidi mkubwa unaoonesha kwamba wino wa tattoo huzunguka mwili kabla ya kujenga amana (depostis).

Matokeo ya utafiti huo yamechapishwa katika majarida mbalimbali pamoja na mtandao wa daily mail Septemba 12, mwaka huu.

Zinawatesa vijana

Dk Anette anasema katika kitengo chicho wamekuwa wakipokea vijana wanaohitaji huduma ya kufutwa tattoo walizojichora mwilini.

Anaongeza “Lakini kwa sasa hapa Muhimbili hatuna ‘procedure’ ya kufuta tattoo (Laser surgery) na huwa hazifutiki kirahisi.

“Wanakosa ajira kwa sababu zipo taaluma ambazo hazipokei watu wenye tattoo au makovu,” anasema.

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement