Recent Post


 


moja

Responsive Advertisement
HPV vaccine being injectedPicha na mtandao

NA VERONICA ROMWALD - DAR ES SALAAM

SARATANI ya mlango wa kizazi hutokana na mabadiliko ya ukuaji usio wa kawaida wa chembe-chembe au seli za mlango wa uzazi.

Mabadiliko hayo husababisha chembe-chembe hizo kushamiri na kukua kwa kasi kinyume na mpangilio wa maumbile, husababisha misuli au viungo vingine vya mwili kuathirika.

Saratani hiyo huweza kusambaa na kushambulia viungo vingine ikiwamo kibofu cha mkojo, uke na sehemu ya chini ya utumbo mkubwa na baadaye figo, ini na viungo vingine vya mwili.

Shirika la Afya Duniani (WHO) linaeleza kwamba saratani ya shingo ya kizazi inazidi kuwa tishio duniani kwa kusababisha vifo vya wanawake wengi.

Linakadiria kila mwaka wanawake zaidi ya 400,000 hugundulika kuwa na saratani hiyo Duniani.

Chanzo ni kirusi.

Kirusi cha Human Pappiloma (HPV) ndicho ambacho husababisha saratani hii, inaelezwa kirusi hiki hubebwa katika mwili wa mwanaume.

Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Saratani wa Taasisi ya Saratani Ocean Road (ORCI), Crispin Kahesa anasema kirusi hicho huingia mwilini mwa mwanamke wakati wa kujamiiana.

"Ingawa kirusi hiki kinabebwa na mwanaume hata hivyo anayeathirika ni mwanamke hasa wale ambao huanza kushiriki ngono mapema," anasema.

Kwanini

Anasema kitaalamu kirusi hicho huchukua muda wa miaka 10 hadi 20 kuanza kuonesha athari zake tangu kilipoingia katika mwili wa mwanamke.

“Ndiyo maana si rahisi kuona athari mara moja, mwanamke anayeanza kushiriki ngono mapema athari zitaonekana baada ya miaka 10 hadi 20 tangu apate maambukizi hayo," anasema.
 Image result for human papillomavirus vaccine
Tafiti

Tafiti zinaonesha wanawake wengi nchini huanza kuonesha dalili za ugonjwa huo wanapofikisha umri wa miaka 40 na kuendelea.

Inadhaniwa kwamba huenda wengi kati yao walianza kushiriki ngono wakiwa na umri wa miaka 25 kushuka chini.

Inaelezwa wasichana wanaoshiriki ngono na wanaume wengi wapo kwenye hatari zaidi ya kupata ugonjwa huo kuliko wale wanaoshiriki na mwanaume mmoja.

Ushuhuda wa mgonjwa

Sophia Mgimba (43) Mkazi wa Mbeya mama wa watoto sita ni miongoni mwa wanawake wanaotibiwa ugonjwa huo ORCI.

Anasema January, mwaka jana alianza kupata maumivu makali ya tumbo na kumwagika damu katika sehemu zake za siri.

"Nilienda katika Hospitali ya Meta kule Mbeya kupata matibabu, walichukua kinyama wakakileta huku Ocean Road kwa uchunguzi zaidi," anasema.

Anasema majibu ya vipimo yalionesha kwamba ana tatizo la saratani ya shingo ya kizazi.

"Nikapewa rufaa pale Meta kuja Ocean Road kwa matibabu zaidi ya kibingwa, sikuwa na fedha za safari, nilisaidiwa na hospitali hiyo pamoja na ndugu zangu," anasema.

Sophia anasema haikuwa rahisi kwake na mumewe kupokea majibu hayo kwani yalionesha kwamba saratani hiyo ilikuwa inasambaa kwenda kwenye kibofu cha mkojo.

"Mume wangu alifadhaika mno na mimi niliumia mno kwa majibu hayo lakini nikajipa moyo ipo siku nitapona ikiwa Mungu ameamua niishi," anasema.

Anaongeza "Katika familia yetu baba yangu aliugua saratani ya koo na Kuna baba yangu mdogo aliugua saratani ya mguu, wote wamefariki dunia kwa sababu walichelewa matibabu.

Imani potofu

Anasema wodini huwa wanasimuliana kuhusu magonjwa ya saratani yanayowakabili.

"Umeona kuna wengine wamefika hali zao si nzuri, wengi wanasema wamezunguka sehemu mbalimbali kutibiwa kwa waganga wa kienyeji wakiamini wamerogwa.

"Simulizi za imani juu ya kurogwa ni nyingi matokeo yake wanakuja hospitalini wakiwa wamechelewa," anasema.

Anaongeza "Nashukuru mimi nimewahi matibabu, sasa hali yangu ni nzuri na namwamini Mungu najua nitapona kabisa.

Visababishi

Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Saratani ORCI, Maguha Stephano, anasema vipo visababishi vingi ambavyo huchangia mwanamke kupata saratani hiyo.

"Uvutaji wa sigara, kuanza ngono mapema, ndoa za mitala na kuwa na wapenzi wengi ni miongoni mwa visababishi," anabainisha.

Dk. Maguha anaongeza "Sigara ni kisababishi kikuu cha magonjwa mengi ya saratani, wanawake wanaoishi na maambukizi ya Virusi Vya Ukimwi (VVU) wana hatari zaidi ya kupata saratani ya shingo ya kizazi kuliko wale wasiougua ugonjwa huo.
 Image result for human papillomavirus vaccine
Picha inaonesha hatua mbalimbali za saratani ya shingo ya kizazi inavyotokea (na mtandao)

Kuna aina zaidi 40 ya virusi

Wataalamu wanasema zipo aina zaidi ya 40 za virusi vya HPV ambavyo vinaweza kusababisha maambukizi kwenye njia za uzazi za wanaume na wanawake na katika sehemu za mdomoni na kooni.

Wanasema hata hivyo aina ya 16 hadi 18 ndizo ambazo husababisha saratani zote za mlango wa kizazi duniani kwa asilimia 70.

Wanasema wanawake wengi duniani wanaopata maambukizi ya virusi hivyo huwa hawapati saratani isipokuwa asilimia 10 tu ndio ambao huonesha dalili za awali za ugonjwa huo baada ya miaka 10 hadi 20 tangu wapate maambukizi.

Wanasema inaaminika asilimia 70 ya watu duniani hupata maambukizi ya virusi hivyo hiyo inamaanisha watu saba kati ya 10 walishapata virusi hivyo katika maisha yao.

Hata hivyo wanasema maambukizi ya HPV huwa hayaoneshi dalili zozote na huweza kusababisha mtu kupata ugonjwa wowote na kwamba asilimia 10 ya walioambukizwa hubaki na virusi hivyo mwilini.

Hali halisi

Magonjwa ya saratani ni tishio hivi sasa nchini, Shirika la Afya Duniani (WHO) linakadiria kila mwaka takriban wagonjwa wapya 50,000 hugundulika kuwa na aina mbalimbali za saratani.

WHO linaeleza kati ya wagonjwa wapya wanaogundulika, 13,000 pekee sawa na asilimia 26 hufanikiwa kufika hospitalini kwa matibabu.

Kwa mujibu wa Shirika hilo, asilimia 70 ya wagonjwa hufika wakati ugonjwa ukiwa umefika hatua za juu za mwisho yaani tatu na nne ambazo ni ngumu kupona.

Takwimu za ORCI

Mkurugenzi Mtendaji wa ORCI, Dk. Julius Mwaiselage anasema mwaka 2016/17 takwimu zinaonesha saratani ya shingo ya kizazi na ya matiti ndizo zinaongoza kwa idadi kubwa ya wagonjwa.

"Saratani ya shingo ya kizazi inaongoza kwa asilimia 32.8, matiti asilimia 12.9 zikifuatiwa na satatani ya ngozi (Kaposis Sarcoma) asilimia 11.7, kichwa na shingo asilimia 7.6, matezi asilimia 5.5, damu asilimia 4.3.

"Nyingine ni saratani ya kibofu Cha mkojo asilimia 3.2, ngozi asilimia 2.8, macho asilimia 2.4 na tezidume asilimia 2.3," anabainisha.
 
Waziri Ummy Mwalimu

Mpango wa chanjo

"Saratani ya shingo ya kizazi inaweza kuepukwa iwapo mtu atajiepusha kushiriki ngono mapema, kuwa na mwenzi mwaminifu, kubeba ujauzito katika umri mdogo, kutumia kondomu na kuepuka uvutaji sigara," anasema Meneja Mpango wa chanjo Taifa, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii,Jinsia, Wazee na Watoto, Dk. Dafrosa Liymo.

Anaongeza "Inazuilika kwa kutumia chanjo maalum ya HPV ambayo huchanjwa wasichana ambao bado hawajaanza kushiriki ngono.

"Serikali inatarajia kuanza utekelezaji wa mpango wa chanjo hii kuanzia April 25, mwaka huu, kwa mwaka huu watachanjwa wasichana wenye umri wa miaka 14, lakini kuanzia mwakani watachanjwa kuanzia miaka tisa hadi 14," anasema.

Anasema lengo ni kukabiliana ili kupunguza idadi ya vifo vitokanavyo na saratani hiyo pia kuzipunguzia familia na serikali mzigo mkubwa wa gharama za matibabu.

Zipoje?

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu anasema serikali hugharamia kiasi cha Sh milioni 5.5 kumtibu mgonjwa mmoja wa saratani kila mwaka ORCI.

"Ni gharama kubwa mno tunatumia kutibu lakini kumkinga msichana mmoja tutatumia Sh 30,000 tu, hivyo tunaona ni muhimu mno kuwakinga," anasisitiza.

Anaongeza "Tuliwasilisha andiko katika Shirika  Gavi la Chanjo Duniani na likakubaliwa, wametufadhili pia serikali imewekeza kiasi cha Sh  milioni 800 katika mpango huu.

Kuhusu usalama/ubora

Anasema katika mwaka 2014 jumla ya wasichana 135,700 mkoani Kilimanjaro walichanjwa na kwamba imeonesha mafanikio kwa kiwango cha zaidi ya asilimia 70.

"Maandalizi ya kuanza rasmi awamu ya kwanza ya chanjo yamekamilika, dozi hutolewa kwa awamu mbili tunakusudia kuwafikia wasichana 616,734 wenye umri wa miaka 14.

Je watawajuaje?

Ni swali ambalo wengi wanajiuliza, kwamba watajuaje wasichana ambao hawajaanza kushiriki ngono, je watawakagua au watatumia mbinu gani?.

Dk. Maguha anasema hawatawakagua kama wengi wanavyodhani na wanaamini wasichana wengi katika umri huo bado hawajaanza kushiriki ngono.

"Tutashirikiana  kwa ukaribu na walimu na wazazi wao katika utoaji wa chanjo hii, tutawapatia wasichana wote walio katika umri huo ili kuwakinga dhidi ya saratani hii," anasema.

Wito

Waziri Ummy anawasihi wananchi kutokuwa na hofu juu ya chanjo hi kwani WHO na Mamlaka ya Udhibiti wa Chakula na Dawa Tanzania (TFDA) imeithibitisha ni salama na haina madhara kwa binadamu.

"Mimi nitakuwa wa kwanza kumchanja mwanangu siku hiyo," anasema.

Kauli ya WHO

Mwakilishi wa WHO Tanzania, Ritha Njau anaipongeza serikali kwa hatua hiyo na kusisitiza kwamba Shirika hilo litaendelea kushirikiana nayo bega kwa bega katika utekelezaji wa mpango huo.

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement