Kufanya mazoezi husaidia kumuondoa mtu kwenye uwezekano wa kupata magonjwa yasiyo ya kuambukiza.
Na Veronica Romwald, Dar es Salaam
Katika sehemu ya nne tuliishiia kidokezo, bajeti ya dawa, katika sehemu hii ya tano na ya mwisho, Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk. Faustine Ndugulile anaeleza, endelea...
Dk. Ndugulile anasema ili kukabiliana na hali ya magonjwa,
serikali iliona vema kuongeza bajeti ya dawa kutoka Sh bilioni 31 mwaka 2015/16
hadi kufikia Sh. bilioni 251 mwaka 2017/18.
“Bajeti hiyo inagusa magonjwa yote, tukaona pia vema kuongeza
vituo vya usafishaji damu ambapo sasa vipo zaidi ya 17 vikiwamo vya serikali na
binafsi ili kusogeza huduma karibu zaidi na wananchi na hivyo kuwapunguzia
mzigo wa gharama za usafiri,” anasema.
Kampeni
ya mazoezi
Anaongeza “Agizo la kufanya mazoezi ni la kudumu na ni muhimu
mno watu wakalizingatia kwa sababu njia moja wapo inayoweza kuwaepusha kupata
magonjwa haya ni kuzingatia kufanya mazoezi, ulaji unaofaa na kupima afya mara
kwa mara.
Wadau watoa neno
Magonjwa hayo hivi sasa yanatajwa kuwa tishio kwa
uhai wa binadamu duniani, takwimu zikionesha kasi ya ongezeko la watu wanaougua
ikiongezeka kadiri miaka inavyosonga mbele.
Wataalamu wa afya wanaeleza ni tishio linalorejesha
nyuma juhudi za kisayansi za kuhakikisha binadamu anaishi maisha marefu zaidi
hapa duniani.
Rais wa Shirikisho la Vyama vya Magonjwa Yasiyo ya
Kuambukiza Tanzania (TANCDA), Dk. Tatizo Waane anasema nguvu zaidi inapaswa
kuwekezwa pia katika kueilimisha jamii jinsi ya kufanya ili kuwekwa kupata
magonjwa hayo.
“Kwa sababu, kulingana na tafiti mbalimbali
zilizokwisha kufanyika, magonjwa haya mengi hutokana na mfumo mbovu wa maisha
hasa ulaji usiofaa na kutokufanya mazoezi.
“Kwa kifupi magonjwa haya ni yale ambayo huwapata
watu ambao hawashughulishi miili yao kwa kazi za kutoa jasho, kutokufanya
mazoezi, ulaji wa vyakula vyenye mafuta mengi, chumvi nyingi, wanga mwingi hasa
katika umri wa utu uzima, hivyo jamii inahitaji elimu ya kutosha kuyaepuka.
“Na hicho ndicho ambacho TANCDA tumekuwa tukifanya
kwa kushirikiana na serikali, tunaielimisha jamii jinsi ya kuepuka magonjwa
haya na wale ambao wamepata wachukue hatua gani na mambo gani wanapaswa
kuzingatia ili waendelee kuishi vema,” anabainisha.
Anaongeza “Ili tuweze kuifikia jamii kwa haraka tuliona
vema kufanya kazi hiyo ya uelimishaji kwa kushirikiana kwa ukaribu na Chama cha
Waandishi Wanaopambana na Magonjwa Yasiyo ya Kuambukiza (TJNCDAF).
“Tuliona vizuri kuanzisha mfumo unaoshirikisha
vyombo vya habari nchini katika kuelimisha jamii juu ya magonjwa haya,
tulitambua kwamba ndiyo mfumo rahisi unaosaidia kuifikia jamii kwa haraka na
kupata uelewa juu ya magonjwa hayo,” anabainisha.
Anasema ufahamu huo wameuweka katika mpango ambao
unawezesha watu wa rika zote kuelimika na lengo ni kuona kwamba katika kizazi
kijacho kasi ya magonjwa hayo inapungua na kulisaidia taifa katika mambo makuu
matatu.
“Kwanza ni kuliepusha Taifa kutumia fedha nyingi
katika kutibu magonjwa haya, magonjwa mengi yasiyo ya kuambukiza ni sugu,
hayaponi hivyo muathirika inambidi kuhudhuria kliniki mara kwa mara na kutumia
dawa katika maisha yake yote,” anasema.
Dk. Waane anasema pili ni kuongeza nguvu kazi na
kuimarisha uchumi wa Taifa na jamii kwa ujumla.
“Jamii ya watu wengi wanaougua hutumia muda mrefu
kushughulikia ugonjwa na kutoa huduma kwa wagonjwa, hapa muda wa kufanya kazi
hupunguza na kuathiri uchumi na mapato kwa ujumla,” anabainisha.
Anasema tatu ni kuepusha watu wengi kufa mapema
kwamba magonjwa sugu yamekuwa yakiharakisha watu kufa mapema, hii inaweza
kutokea kwa mgonjwa kutokuwa na elimu sahihi ya namna ya kudhibiti na umuhimu
wa kupima afya mara kwa mara na kupata ushauri wa kitaalamu.
“Hivyo tunaamini kuelimisha jamii, ufahamu
utawezesha familia nyingi kutopata magonjwa haya na hata kwa wale ambao tayari
wameathirika kuwa na elimu sahihi ya kuyadhibiti,” anasema.
Chapisha Maoni