Recent Post


 


moja

Responsive Advertisement

Image result for saratani ya kooKatika sehemu ya pili tumeona namna ambavyo gharama za matibabu ni changamoto kwa wagonjwa wa moyo na figo, katika makala haya nitagusia gharama za matibabu dhidi ya saratani na mambo mengine mengi... endelea. 

Na Veronica Romwald, Dar es Salaam

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu anasema kwa upande wa matibabu ya saratani serikali hutumia wastani wa Sh. milioni 5.5 kila mwaka kumtibu mgonjwa mmoja wa saratani Ocean Road.

“Ni gharama kubwa mno, zinatumika lakini hatuwezi kuacha kulipa kumtibu Mtanzania, lazima tumtibu, lakini tunaona ni vema tujikite katika kukinga wananchi wasipate magonjwa haya ambayo mengi yanaweza kuepukwa kwa watu kuviepuka vile vihatarishi,” anasema.

Mzigo kwa serikali
Gharama za matibabu hasa kwa magonjwa yasiyo ya kuambukiza licha ya kuwa ni mzigo kwa jamii sasa zinaonekana wazi kuielemea Serikali.

Sasa imeanza kuchukua hatua na kuwekeza nguvu kubwa katika kuielimisha jamii jinsi ya kuepukana na magonjwa hayo.

Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Magonjwa Yasiyo ya Kuambukiza wa Wizara hiyo, Dk. Sarah Maongezi  anasema hata hivyo inahitajika nguvu ya pamoja kufikia lengo hilo.

“Serikali tunahitaji kushirikiana bega kwa bega na wadau mbalimbali wa masuala ya afya wakiwamo waandishi wa habari hasa katika kuelimisha jamii namna ya kuepukana na magonjwa haya,” anasema.

Waziri Ummy anasema matibabu dhidi ya magonjwa hayo yamegawanyika katika makundi makuu mawili, kwamba kuna wagonjwa ambao hutibiwa kwa dawa maalum na wengine huhitaji upasuaji.

“Kwa mfano wa saratani wale hutibiwa kwa dawa na mionzi pamoja na wanaougua kisukari lakini kwa wagonjwa wa moyo, figo na maradhi mengineyo matibabu yao ukijumuisha dawa huwa pia wanatibiwa kwa kufanyiwa upasuaji,” anabainisha.

Anaongeza “Kwa matibabu ya saratani pekee tunatumia takriban Sh. bilioni saba kwa ajili ya kununua dawa kila mwaka, hapo hatujajumuisha gharama zingine za watumishi, umeme, maji na nyinginezo.

“Kumtibu mgonjwa mmoja wa moyo tulilazimika kutumia zaidi ya Sh. milioni 80 mgonjwa mmoja anayehitaji upasuaji wa kutibu ugonjwa wa moyo nje ya nchi.

“Ndiyo maana serikali iliamua kuwekeza Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) ili kuokoa fedha nyingi ambazo zilikuwa zikitumika kutibu wagonjwa nje ya nchi,” anasema.

Sera ya msamaha ‘kikwazo’

Mkurugenzi Mtendaji wa JKCI, Profesa Mohamed Janabi anasema pamoja na mafanikio ambayo Taasisi hiyo ya umma inayochunguza na kutibu magonjwa ya moyo imeyapata, sera ya msamaha inawapa changamoto kubwa.

Anasema miongoni mwa wagonjwa wanaopokelewa kliniki asilimia 38 hutibiwa kwa bima, asilimia 17 huchangia huduma na kwamba asilimia tano pekee hutibiwa kwa kulipia gharama (cash).

“Kati ya wagonjwa wote tunaowatibu, asilimia 40 huwa ni wagonjwa wa msamaha, kusema ukweli huu ni mzigo mkubwa kwa hospitali na serikali kwa ujumla.

“Kwa sababu, uchunguzi na matibabu ya magonjwa ya moyo ni gharama kubwa mno hasa pale tunapohitaji vifaa kwa mfano vile vya kupandikiza (pacemaker), huwa tunavinunua kwa kuagiza nje ya nchi ambako vinauzwa gharama kubwa mno,” anasema.

Ushauri

Dk. Pallangyo anasema kulingana na matokeo ya utafiti waliofanya wanaishauri Wizara na wadau mbalimbali wa sekta ya afya nchini kutafuta mbinu zitakazosaidia kuhakikisha wananchi wanakuwa na bima ya afya.

“Ifike mahali bima ya afya iwe ni haki ya msingi kwa kila mwananchi badala ya wachache tu kuwa nayo, maana kwa matokeo haya inaonesha wazi kwamba mtu akiwa na bima ya afya anakuwa hana ‘stress’ za jinsi gani atamudu gharama za matibabu na dawa,” anasema.

Dk. Pallangyo anaongeza “Lakini pia itafakari jinsi gani kila atakayekata bima ya afya atakuwa analipa kwa sababu sisi wafanyakazi tunakatwa kwenye mshahara lakini kuna kundi la watu ambao wamejiajiri wenyewe katika ajira ambazo si rasmi.

“Tunaona pia kuna haja zaidi ya kuwapatia elimu wananchi kuhusu umuhimu wa kukata bima ya afya na kuzingatia matumizi ya dawa kulingana na walivyoelekezwa na wataalamu wa afya katika kutibu magonjwa mbalimbali,” anasema Daktari huyo.


Kauli ya serikali

Waziri Ummy anakiri kwamba sera hiyo ni changamoto hasa katika utekelezaji wake kwani kwa wastani asilimia 40 ya wagonjwa wanaotibiwa katika taasisi zake ni wa msamaha.

“Tunajumuisha makundi maalum pia wakiwamo wajawazito, watoto wenye umri wa chini ya miaka mitano na wazee wasiojiweza, hivyo tunalazimika kuhakikisha tunapeleka bajeti ya dawa na baadhi ya vifaa tiba katika taasisi zetu.

“Lakini, kweli mzigo unakuwa mkubwa, kwa msingi huo kwenye sekta ya afya tunakusudia kuja na mkakati wa kugharamia huduma za afya (Health Sector Financing), ambao utabainisha vyanzo mbalimbali vya mapato vitakavyogharamia huduma za afya nchini,” anasema.

Vyanzo vyenyewe

Anataja chanzo kimoja wapo ni bima ya afya kwa kila Mtanzania na kwamba hilo litakapopitishwa na Bunge itamlazimu kila mmoja kuwa nayo.

“Tulichoamua kufanya ni kwamba ndani ya huo mkakati kuna mapendekezo ambayo yanayohusu Wizara ya Fedha (Hazina) na mengine yatahusu wananchi moja kwa moja hasa kuchangia gharama kabla ya kupata matibabu yaani kukata bima ya afya.

“Tunakusudia April, mwaka huu tutafanya kikao huko mjini Dodoma na wabunge pamoja na wadau wa maendeleo kutoka Benki ya Dunia (WB) ili sasa waweze kuupitia mkakati wetu tulioandaa na wao watoe maoni yao ili baada ya hapo tuuwasilishe katika Baraza la Mawaziri kabla haujaenda tena Bungeni,” anasema.

Anaongeza “Katika uandaaji wa mkakati huu, tuliangalia mfano katika nchi zingine ikiwamo Ghana ambao wao katika ile VAT (Kodi ya Ongezeko la Thamani) kuna asilimia fulani ambayo hiyo ni lazima iingizwe katika kuchangia huduma za afya.

“Afrika Kusini wenzetu wana mfumo wanauita ‘sin-taxes’ yaani kwa zile bidhaa na huduma ambazo kwa namna moja au nyingine zina athari kwa binadamu kwa mfano sukari, disko, sigara, vilevi na nyingine za namna hiyo kuna kiasi fulani cha fedha kupitia kodi kinakatwa na kwenda kuchangia huduma za afya,” anabainisha.

Chanzo kingine

“Sasa hivi ukienda pale Taasisi ya Mifupa Muhimbili (MOI) takriban asilimia 50 ya wagonjwa wanaopokelewa na kutibiwa wengi ni wa ajali hasa za bodaboda na zile za magari.

“Kwa hiyo, hivyo tumeona chanzo kingine ambacho tunaweza kupata fedha ya kuchangia huduma za afya, ikiwa wenzetu watakubaliana nasi, ni kutokana na kodi za leseni.

“Kwa kuwa watu hukata leseni na huwa zinalipiwa basi kiasi fulani cha fedha kipelekwe katika huduma za afya,” anasema.

Hali halisi..... Itaendelea

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement