Picha (na mtandao) inaonesha dalili za ugonjwa huo.
*Ni ugonjwa usiojulikana chanzo chake, hauna tiba
*Huweza kusababisha kuharibika
mimba
NA VERONICA ROMWALD – DAR ES
SALAAM
KWA kawaida kinga za mwili
humlinda mtu husika dhidi ya magonjwa mbalimbali, hata hivyo wapo baadhi ambao
hujipata kinga zao zikishambulia mwili badala ya kuulinda.
Ugonjwa huo kitaalamu huitwa
‘System Lupus Erythematosus (SLE), hadi sasa bado wataalamu wa afya hawajabaini
nini hasa husababisha kutokea kwake.
May 3, 2018, Onesmo Mhehwa
aliyekuwa Daktari Bingwa wa Usingizi kwa Watoto na Wagonjwa mahututi katika
Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) alifariki dunia kutokana na ugonjwa huo.
Simulizi ya mgonjwa
Meneja Utawala, Huduma za
Hospitali (HR) katika Taasisi ya Tiba ya Mifupa Muhimbili (MOI), Costansia Lima
anasema mwaka 2015 alianza kujihisi vibaya hasa sehemu za kichwa.
“Nilianza kuhisi pia sehemu ya
tumbo (eneo la chini) lilianza kuuma, nikaenda kuonana na Medical Director wa
Muhimbili nikamueleza, akanipatia daktari wa Neurology, akanichunguza kwa
vipimo mbalimbali ikiwamo MRI lakini hakuona tatizo.
“Siku zilivyoenda hali yangu
ilizidi kubadilika, nikaanza kupata reaction kwenye ngozi, nikawa napata mabaka
meusi, nywele zikaanza kunyofoka nikichana, nikabadilika sura, nilikuwa na hali
mbaya.
“Mkurugenzi wa Muhimbili
akasema kama imeshindikana kugundulika wanipe rufaa nikapelekwa India, kule
nilipata nimonia kali, lakini Mungu alinisaidia nikapata matibabu na nikapata
nafuu, nikarejea nyumbani nikapewa dawa za kunisaidia.
“Sikuweza kuzungumza na wale
madaktari nilikuwa na hali mbaya, nipo nchini naendelea na matibabu hapa
nyumbani, ni wakati sasa jamii ielezwe kwa kina kuhusu ugonjwa huu, inawezekana
wanaumwa lakini hawajui kama ni ugonjwa, mimi ilichukua muda mrefu
kugundulika,” anasema Lima huku akitokwa machozi.
Mgonjwa mwingine
Tangu mwaka 2007 hadi sasa,
Irene Kilumanga ambaye ni mke wa Balozi Chabaka Kilumanga anaishi akisumbuliwa
na ugonjwa huo na kwamba dalili zake zinafanana na za malaria, kuhisi homa
homa.
Mumewe, Balozi Kilumanga
anasema watu wanaougua ugonjwa huo unaweza kuona wanafanya makusudi kutokana na
kuugua kwa muda fulani na muda mwingine kuoneka akiwa mzima.
“Kwa mtu ambaye hana imani
anaweza kudhani amerogwa kwa sababu anaweza kuwa mzima na ghafla akajikuta
ameanguka, mwili unaanza kuishiwa nguvu na anapata maumivu,” anasema.
Anaongeza “Sisi tulimpeleka
hospitalini akawa akitibiwa baada ya muda tena anaumwa, tukimrudisha ikawa
madaktari wanajaribu kuchunguza kila aina ya ugonwja lakini hawakuweza kubaini
kilichokuwa kinamsumbua.
Daktari
Kifo cha Dk. Mhehwa (pichani) kimeipa
‘pigo’ JKCI kwani ndiye alikuwa pekee kwa upande wa matibabu ya watoto.
Mkurugenzi Mtendaji wa JKCI,
Profesa Mohamed Janabi anasema pamoja na kutojulikana chanzo cha ugonjwa huo
hauna tiba.
Anasema hata dalili zake bado
hazijathibitika na kwamba hufanana kwa ukaribu na dalili za magonjwa mengine
kama vile malaria.
“Wataalamu hata sayansi
haijaweza kujua, ile system ya mwili inaugeuka mwili wenyewe, ghafla inaanza
kuushambulia kila mahali, kwenye figo, moyo, tumbo chochote wenyewe unadhani ni
adui.
“Hauna tiba, mgonjwa akija
hospitalini kama anasumbuliwa na bakteria tunampa antibiotics, ikiwa ni virusi
nitakupa dawa ya virusi, lakini kwa kawaida mtu anapolalamika kuumwa moja kwa
moja tunaangalia labda amepata malaria.
“Lakini akipimwa malaria
haionekani, typhoid hana, hapo inabidi achunguzwe zaidi kuliko vipimo
vilivyozoeleka na ndipo tunapogundua nini kinamsumbua.
Utafiti
Kulingana na mtandao wa Medical
News Today, inaelezwa Lupus ni miongoni mwa magonjwa sugu, ambapo kinga za
mwili wa binadamu badala ya kumlinda hugeuka na kuanza kumshambulia.
Hali hiyo inapotokea muhusika
huhisi maumivu makali, huvimba mwili, homa za mara kwa mara, na baadae viungo
vyake vya ndani ikiwamo moyo, figo na mapafu navyo huathiriwa.
Mtandao huo unaeleza, kwa
kawaida mfumo wa kinga hutengeneza protin iitwayo ‘antibodies’ ambayo hulinda
na kupigana dhidi ya ‘antigens’ kama vile virusi na bakteria.
Lakini, kwa mtu mwenye Lupus
mambo huwa kinyume, yaani ule mfumo wake wa kinga wa mwili hushindwa
kutofautisha kati ya ‘antigens’ na tishu zilizo bora.
Hali hiyo husababisha mfumo wa
kinga kuziamuru ‘antibodies’ kuzishambulia tishu zilizo bora badala ya
‘antigens’ kama inavyopaswa.
Kwa mujibu wa mtandao huo,
kitendo hicho ndicho ambacho hupelekea muhusika kupata maumivu makali, uvimbe
na kuathirika kwa viungo vyake.
Inaelezwa ugonjwa huo si wa
kuambukiza na kwamba umegawanyika katika aina mbalimbali ikiwamo Lupus
Erythematosus (SLE) na Lupus Discoid (Cutaneous).
Celena Gomez ni msanii mkubwa anayesumbuliwa na ugonjwa huo,
Mtandao huo unaeleza, Kulingana
na Shirika la Lupus la nchini Amerika, watu wapatao milioni 1.5 hadi mbili
nchini humo wanakabiliwa na aina mojawapo ya Lupus.
Inaelezwa asilimia 72 ya
wamarekani wenye umri wa miaka kati ya 18 hadi 34 hawaufahamu kwa kina ugonjwa
huo.
Mtandao huo unaeleza zaidi ya
asilimia 90 ya wagonjwa wa Lupus ni wanawake na kwa kawaida huwapata watu walio
kati ya umri wa miaka 15 hadi 45.
Dalili zingine
Kulingana na mtandao wa Heath
line, watu wenye Lupus figo zao huvimba hali iitwayo kitaalamu ‘nephritis’
huzifanya zishindwe kuchuja taka mwili na kujikuta wakipoteza damu.
Mtandao huo unaeleza, kwa
mujibu wa Shirika la Lupus la Amerika, nephritis huanza kujitokeza ndani ya
kipindi cha miaka mitano tangu mtu apate ugonjwa huo.
Unaeeleza mtu mwenye Lupus
ambaye figo zake zimeanza kushindwa kufanya kazi huvimba miguu, hupata
shinikizo la damu, huona chembe chembe za damu kwenye mkojo wake.
Unaeleza wakati mwingine mkojo
huonekana kuwa wa rangi nyeusi, huenda haja ndogo mara kwa mara hasa nyakati za
usiku na hupata maumivu wakati wa kujisaidia haja ndogo.
Wakati mwingine, mtu mwenye
Lupus huugua homa ya matumbo ingawa si wote na wapo ambao hupata ukavu wa
midomo au macho na kunyonyoka nywele.
Kwa mujibu wa mtandao huo,
wagonjwa wengi wa Lupus upata vipele usoni unaozunguka (butterfly rash).
Kwanini wanawake?
Mtandao huo wa Health Line
unaeleza wanawake wanaokabiliwa na ugonjwa huo huonesha dalili pia kipindi cha
hedhi na ujauzito.
Hali hiyo inawafanya
wanasayansi kuamini kwamba huenda linachochewa zaidi na homoni ya kike
(Estrogen) hata hivyo bado
tafiti zinahitajika kuthibitisha ukweli wa mtazamo huo.
Mtandao wa Medicine Net
unaeleza mjamzito mwenye tatizo la Lupus hupaswa kufuatiliwa hali yake kwa
ukaribu zaidi kwani tatizo hilo huweza kupeleka kuharibika kwa mimba.
Visababishi
Pamoja na kuwa bado chanzo
chake hakijulikani wala tiba yake haijulikani, hata hivyo wataalamu wa afya
wanaamini kwamba huenda ugonjwa huo unatokana na sababu za mabadiliko ya
vinasaba na za kimazingira.
Inadhaniwa vitu ambavyo
huchangia mtu kupata Lupus ni pamoja na msongo wa mawazo, miale ya jua,
matumizi ya dawa za kulevya, maambukizi ya virusi vya Epstein-Barr (kwa watoto)
na yale yatokanayo na baadhi ya kemikali, mwanga wa ‘ultraviolet’, matumizi ya
sigara na dawa za kutuliza maumivu (antibiotics).
Changamoto zingine
Mtandao wa Health Line unaeleza
wagonjwa wa Lupus hukabiliwa pia na tatizo la kushindwa kuganda kwa damu,
kuvimba mishipa ya damu, mabadiliko ya tabia, kushindwa kutunza kumbukumbuku,
kuvimba mapafu, moyo na hatimaye kiharusi.
Kwa mujibu wa mtandao huo,
tafiti zinaonesha watu wanaokabiliwa na ugonjwa huo huweza kuishi nao kwa miaka
40 ikiwa watapata matibabu sahihi.
Mkakati
“Dk. Mhehwa (marehemu)
amekuwa chanzo cha watu wengi kuanza kuujua ugonjwa huu baada ya kufariki na
ndipo nilipoona Profesa Janabi akiizungumzia nikaona nimtafute ili
tushirikiane kuutangaza,” anasema Dk. Kilumanga.
Anasema wanakusudia
kuanzisha taasisi ambayo itakuwa ikijishughulisha kutoa elimu kwa umma juu ya
ugonjwa huo.
Anasema katika nchi
zilizoendelea wanaujua ugonjwa huo wa SLE ambapo kuna siku maalumu ya
kuadhimisha ambayo ni May 10 kila mwaka.
“Anasema matibabu dhidi ya
ugonjwa huo ni ghali na kwamba vidonge anavyopatiwa mgonjwa si tiba bali humsaidia
tu kupunguza yale maumivu anayoyapata ili ugonjwa huo usifikie hatua za juu (acute
stage) na kusababisha viungo vyake vya mwili kuanza kushambulia.
Ombi kwa serikali
Balozi Kilumanga anaishauri serikali
ianze kuandaa wataalamu watakaobobea kutibu ugonjwa huo tofauti na ilivyo sasa.
Aidha, anaishauri kununua vifaa
vya kupimia ugonjwa huo ili watu waweze kugundulika mapema tofauti na ilivyo
sasa ambapo wanaenda kugundulika nje ya nchi.
Balozi Chabaka Kilumanga pia
anaiomba serikali, kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na
Watoto kuangalia kwa undani suala hili ikiwa ni pamoja na kuanzisha kitengo
kitakachoangalia ugonjwa huu.
“Aidha, pamoja na kuanzisha
kitengo hicho ni muhimu pia kuangalia namna ya kuwapata wataalamu ambapo
wataushughulikia ugonjwa huu,” anatoa rai.
Makala haya kwa mara ya kwanza yametoka Mei 31, 2018 katika gazeti la MTANZANIA ambalo nalitumikia.
Chapisha Maoni