Recent Post


 


moja

Responsive Advertisement
retinoblastoma-photoPicha (na mtandao) inaonesha dalili za awali za saratani ya Retinoblastoma.

NA VERONICA ROMWALD - DAR ES SALAAM

UTAFITI uliofanywa na Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) umeonesha watoto wengi wenye saratani ya jicho wanaopokelewa hospitalini hapo wanatoka katika maeneo ya Kanda ya Ziwa. 

Hayo yalielezwa Dar es Salaam jana na Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Saratani kwa Watoto wa Muhimbili, Anna Sanyiwa alipozungumza mbele ya Mganga Mkuu wa Serikali walipotoa tamko kuhusu Maadhimisho ya Wiki ya Kuongeza Uelewa kuhusu Saratani ya Jicho (Retinoblastoma). 

"Mwaka 2007 tulifanya utafiti ulionesha hali hiyo na hivi karibuni, mwaka huu tumefanya tena utafiti bado wagonjwa wengi tunapokea kutoka ukanda huo, " alisema. 

Alisema wagonjwa wengi wanatoka maeneo ya vijijini mno hasa mkoa wa  Mwanza, Tabora, Rukwa tena kutoka jamii masikini.

"Hatujajua sababu hasa ni nini lakini mara nyingi saratani hii inatokana na hitilafu ya vinasaba, tunadhani labda pengine na changamoto za mazingira zinachangia, hilo bado hatujajua, " alisema. 

Alisema pamoja na hayo utafiti huo mpya umeonesha matumaini kidogo kuliko ule wa mwaka 2007 kwamba angalau wazazi wameanza kuwahishwa watoto hospitalini.

"Awali walifikishwa wakiwa wamechelewa mno, lakini siku hizi wanaletwa wakiwa na miezi mitano, sita na kuendelea, hata hivyo bado asilimia 85 wanakuja wakiwa wamechelewa kwa  asilimia 40 hupona  na vifo ni asilimia 50," alisema. 

Alisema katika nchi zilizoendelea asilimia 90 ya wagonjwa hupona kwani huwahishwa hospitalini.

"Inabidi tujitahidi kuhamasisha jamii walete watoto tuwachunguze mapema dawa zipo, vifaa vipo na wakiwahi matibabu wanapona, " alisema. 

Akizungumza, Mganga Mkuu wa Serikali, Profesa Mohamed Kambi alisema Retinoblastoma ni saratani inayotokea mara nyingi watoto wakiwa na umri wa mwaka mmoja hadi miaka mitano. 

"Ni tatizo la Kitaifa, hutokea kwenye pazia la fahamu la jicho, inaweza kuathiri jicho moja ama yote mawili iwapo lililoathirika huachwa bila kutibiwa, " alisema. 

Alisema hiyo huharibu jicho lote na kulazimisha jicho kutolewa amazing kuleta kifo baada ya kusambaa katika hatua za mwisho. 

"Kati ya vizazi hai 16,000 hadi 18,000 duniani asilimia moja huwa na saratani ya Retina,  huchangia asilimia tatu ya saratani za watoto duniani kote na kwa Afrika huchangia asilimia 10 hadi 15 ya saratani zote za watoto, idadi ipo sawa kwa wavulana na wasichana, " alisema. 

Alisema takwimu nchini zinaonesha watoto 137 wenye saratani hiyo walionwa kwenye vituo vya kutolea huduma za afya mwaka jana. 

Alisema watoto wanaopewa rufaa na kufika Muhimbili ni wastani wa watoto 80 hadi 100 kila mwaka, wengi hutibiwa Hospitali ya KCMC Moshi.

Alisema maadhimisho ya Wiki ya Saratani ya Retina kwa mwaka 2018 yamebebwa na kauli mbiu isemayo 'Mboni Nyeupe kwenye Jicho la Mtoto ' inaweza kuwa Saratani ya Retinoblastoma. 
 
Habari hii imetoka leo katika gazeti la MTANZANIA ambalo nalitumikia.

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement