Recent Post


 


moja

Responsive Advertisement
Image result for EBOLAMwili wa marehemu anayedhaniwa kufariki kwa Ebola huzikwa na watumishi wa afya waliovalia mavazi maalum ya kujikinga dhidi ya ebola  (Picha na mtandao).

NA VERONICA ROMWALD – DAR ES SALAAM

EBOLA ni miongoni mwa magonjwa ya mlipuko yanayotishia uhai wa viumbe hai hasa binadamu waishio katika Ukanda wa Kusini mwa Jangwa la Sahara.

Mtandao wa Wikipedia unaeleza ugonjwa huo kwamba husababishwa na virusi vya Ebola ambavyo hupelekea tatizo la damu kutoganda na unaua.

Ni ugonjwa hatari ambao husababisha kuvuja kwa damu ndani ya mwili na kutoka kupitia matundu mbalimbali ya nje ikiwamo mdomoni, sikioni, puani na hatimaye kifo.

Inaelezwa kwamba huweza kusambaa kwa haraka kupitia kwa maji maji ya mwili na dalili zake hazitambuliwi kwa urahisi.

Virusi vya Ebola viligunduliwa katika miaka ya nyuma mnamo 1976 katika milipuko miwili ambapo watu 151 walifariki katika enoe la Nzara, Sudan kusini na watu 280 waliofariki katika eneo la Yambuku karibu na mto Ebola uliopewa jina kutokana na ugonjwa huo.

Mlipuko wa Ebola wa mwaka 2014-16 Afrika uliowaua watu 11,300 ulikuwa mbaya zaidi, ulisamba kwenda miji mikuu ya nchi za Guinea, Sierra Leone na Liberia.

Inakadiriwa kati ya watu 10 wanaopata virusi vya Ebola wastani wa watano hadi tisa kati yao hufariki dunia.
Mtu hupata ugonjwa huo kwa kugusa damu au majimaji ambayo yanakuwa yametoka kwa mtu mwenye maambukizi ya ugonjwa huo.

Ama kwa kugusa maiti ya mtu aliyekufa kwa ugonjwa huo, kugusa wanyama (mizoga na wanyama wazima) walioambukizwa kama vile sokwe na swala wa msituni.

April 4, mwaka huu Shirika la Afya Duniani (WHO) ilitangaza kuzuka tena kwa ugonjwa huo huko Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC).

Viliripotiwa visa 30, watu wapatao 18 wamefariki dunia licha ya kwamba ni visa viwili tu ndivyo vilivyothibitishwa kimaabara kwamba vilitokana na  Ebola.

Ugonjwa huo uliripotiwa kutokea huko katika mji wa Biroko ulioko jimbo la Equator ambapo takriban mwaka mmoja uliopita ulitokea mlipuko mwingine ambao ulisababisha vifo vya watu wanne.

Mei 17, mwaka huu, ugonjwa huo uliripotiwa kuanza kusambaa katika eneo jingine jingine nchini humo, Waziri wa afya wa Kongo, Oly Ilunga Kalenga, alithibitisha kisa kimoja huko mjini Mbandaka.

Mji huo unatajwa kuwa na wakazi wengi kiasi cha milioni moja, upo kilomita 130 kutoka eneo ambapo kisa cha kwanza kilithibitishwa mapema mwezi huu.

Mji huo ni muhimu kwa usafiri ukiwa na barabara zinazoelekea mji mkuu Kinshasa, hofu inazidi kuenea wapi kwengine ugonjwa huo utazuka.

Ofisa wa cheo cha juu wa WHO, Peter Salama, alinukuliwa akisema kuanza kusambaa kwa Ebola kwenda Mbandaka kuna-maanisha kuwa huenda kukawa na visa vingine vya milipuko ya ugonjwa huo.

Visa vilivyothibitishwa vya ugonjwa huo vimerekodiwa sehemu tatu kwenye mkoa wa Equateus, kwa mujibu wa WHO.

Wafanyakazi wa afya wametambua watu 430 ambao huenda wakikaribiana na ugonjwa huo na wanajaribu kuwatafuta wengine 4000 ambao wametawanyika kwenda kaskazini magharibi mwa Kongo.

Siku ya Jumatano chanjo kwa ajili ya majaribio dhidi  ya ugonjwa wa ebola iliyotumwa na WHO iliwasili nchini humo huku nyingine ikitarajiwa kuwasili hivi karibuni.
 Image result for WHO GENERAL DIRECTOR
Mkurugenzi wa WHO,  Tedros Adhanom (pichani) alitembelea katika mji wa Bikoro kaskazini magharibi mwa nchi hiyo, kujionea hali halisi na kufanya tathmini namna ya kudhibiti maambukizi ya ugonjwa huo.

WHO hivi sasa inafuatilia kwa ukaribu mlipuko huo wa ugonjwa ambao unaambukizwa kwa njia ya kugusa majimaji yaliyotoka kwa mgonjwa.

Hofu iliyopo sasa ni wapi pengine ugonjwa huo utazuka na kuathiri maeneo mengine duniani, hivyo WHO tayari mashirika mengine yanayofanya kazi nchini humo na yale ya Umoja wa Mataifa yameanza kutuma timu ya waangalizi wao nchini humo ili kufuatilia na kudhibiti usienee.

Kila nchi inapaswa kuhakikisha inafuatilia kwa ukaribu ugonjwa huo na kuimarisha mifumo yake ya ukaguzi wa wageni hasa katika maeneo ya mipakani na viwanja vya ndege ili kuudhibiti.

Waziri wa Afya, Maendleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu anasema tayari wamechukua hatua juu ya hilo.

“Ebola ni kati ya magonjwa yenye hatari ya kusambaa kwa kasi na kuleta madhara makubwa kiafya duniani. Ingawa hadi sasa Tanzania hakuna mgonjwa yeyote aliyehisiwa au kuthibitishwa kuwa na virusi vya ebola, nchi yetu inapata na Kongo na ipo hatarini kuambukizwa kutokana na mwingiliano wa watu wanaosafiri, wanaotoka na kuingia.

“Kwa sababu hizi, tahadhari lazima zichukuliwe, hivyo Wizara inapenda kutahadharisha wananchi juu ya ugonjwa huu katika mikoa yote hasa iliyoko mpakani mwa Kongo ikiwamo Mwanza, Kagera, Kigoma, Katavi, Rukwa na Songwe,” anasema.

Anasema katika mikoa hiyo serikali imeweka uangalizi zaidi kwani ndiko ambako kuna muingiliano mkubwa wa watu hadi kupitia njia ya majini.

“Ingawa kuna changamoto tunaiona hasa kuwapo njia za panya ambazo baadhi ya watu wasio waaminifu huweza kuzitumia lakini pia kuna wahamiaji haramu, lakini tunashirikiana kwa ukaribu na nchi zingine kuudhibiti tukiongozwa na Sheria ya Kimataifa ya Afya (IHR) kila nchi inawajibika,” alisema.
 Image result for EBOLA
Ramani inaonesha maeneo yaliyopo hatarini kupata maambukizi ya ugonjwa huo.

Dalili

Anasema huanza kuonekana kwa mtu aliyeambukizwa baada ya siku mbili hadi 21 tangu alipoambukizwa.

“Hupata homa ya ghafla, hulegea mwili, hupata maumivu ya misuli, kuumwa kichwa na vidonda kooni, mara nyingi dalili hizi hufuatiwa na kutapika, kuharisha, vipele vya ngozi na pia figo na ini hushindwa kufanya kazi,” anasema.

Waziri Ummy anasema ugonjwa huo unaweza kuzuilika kwa mtu kujikinga kwa kuepuka kugusa au kuingiwa na mate, damu, mkojo, jasho, kinyesi, machozi na majimaji mengine yanayotoka mwilini kwa mtu mwenye dalili.

“Kwa kuepuka kushughulikia maiti ya mtu aliyekufa akiwa na dalili za ebola, badala yake watoe taarifa kwa uongozi wa kituo cha huduma za afya kwa ushauri.

“Wananchi waepuke mila na desturi zinazoweza kucheleweha kupata huduma muhimu na kuzidi kueneza ugonjwa huu,” anasema.

Anasema wanapaswa kuzingatia usafi wa mwili, kutoa taarifa mapema kwa viongozi wa serikali na wa huduma za afya katika ngazi zote pale anapotokea mtu mwenye dalili za ebola.

Anasema njia nyingine ya kuubidhiti ugonjwa huo ni kufuatilia kwa ukaribu na kuwatenga wale wanaogundulika kuwa na maambukizi hayo na kuwaweka katika mpango wa ufuatiliaji.

“Yeyote anayekuwa kwenye hatari ya kuambukizwa anafuatiliwa kwa siku 21 na maziko hufanyika kwa uangalizi ili kuudhibiti,” anasema.

Aidha, dunia haiwezi kusahau janga la Afrika magharibi mnamo 2014-16 lililozuka katika kijiji kimoja cha mpakani nchini Guinea, na muathiriwa wa kwanza anadhaniwa kuwa mtoto wa kiume mwenye umri wa miaka miwili aliyefariki duniani mnamo 2013.
 Image result for waziri ummy
Kuhusu chanjo

Waziri Ummy (pichani) anasema bado wanasubiri kupokea taarifa rasmi ya WHO na kusisitiza hadi sasa hakuna mtu aliyehisiwa kuwa na ugonjwa huo nchini.

“Tumeimarisha mfumo wa ufuatiliaji magonjwa, kila siku tunapokea taarifa kuhusu wagonjwa nchi nzima, hadi sasa hakuna taarifa ya mtu aliyehisiwa kuwa na Ebola, tupo salama,” anasema Waziri Ummy.

Ni janga

Magonjwa ya mlipuko sasa ni janga linalotesa nchi zinazoendelea hasa zilizopo kusini mwa Jangwa la Sahara ambako jamii nyingi zinaishi katika ‘dimbwi’ la umasikini.

Pamoja na magonjwa hayo, majanga mengine yanayozikumba nchi hizo ni ya kiasili kama vile ukame, mafuriko na zipo zenye migogoro ya kisiasa.

Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Afya Duniani (WHO-Kenya), Dk. James Kojo anasema kati ya majanga ya dharura 100 ya dharura yanayotajwa kila mwaka katika Ukanda huu, mengi ni yale ambayo huusisha magonjwa ya mlipuko ambayo huhitaji ufumbuzi wa haraka.

Kulingana na WHO, kipindupindu ndiyo ugonjwa wa mlipuko unaoonekana kuwa tishio zaidi huchukua kiasi cha asilimia 23 kila mwaka.

WHO inaeleza ni tatizo linalokabili nchi nyingi na kwamba majanga ya asili ni asilimia 17 na asilimia tano huwa ni majanga mengineyo ukiwamo Ebola.

Rai kwa waandishi

Kojo anasema Serikali pekee kupitia wizara ya afya haziwezi kufanya kazi peke yake kukabili magonjwa na kwamba waandishi wa habari wana nafasi kubwa kushirikiana nao kuhakikisha wanatoa taarifa sahihi ili kusaidia jamii.

“Sisi (WHO na Wizara) kazi yetu ni kutoa takwimu lakini hatuwezi kusimulia habari. Ninyi mnao uwezo huo lakini ni muhimu kuhakikisha mnakusanya taarifa kutoka kwa vyanzo sahihi ili kuisaidia jamii hasa jinsi ya kuepuka magonjwa haya,” anatoa rai.

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement