Recent Post


 


moja

Responsive Advertisement

Image result for LAWNA VERONICA ROMWALD – DAR ES SALAAM

MIRATHI ni utaratibu unaotumika kugawa mali zilizoachwa duniani na marehemu katika jamii nyingi za kiafrika linapofika suala la kugawa mirathi matatizo mengi huibuka.

Baadhi ya watu huanza kugombea mali za marehemu, mzozo huwa mkubwa na mgumu kuutatua hasa pale inapotokea kwamba marehemu hakuacha wosia.

Wakati mwingine hata anapokuwa ameandika na kuacha wosia ikiwa hakufuata taratibu zinazotakiwa wosia huo hushindwa kutambulika kisheria na hivyo bado huacha matatizo mengi.

Inaelezwa watu wengi hawajui jinsi ya kuandika wosia unaotambulika kisheria ingawa kuna changamoto kwamba wapo wanaoogopa kuandika kwa hofu ya kujichuria kifo.

Pamoja na hayo, MATUKIO NA MAISHA imezungumza na Wakili wa Mahakama Kuu Tanzania, Maulid Kikondo ambaye hapa anaeleza kwa kina kuhusu umuhimu wa wosia na suala zima la mirathi.

Anasema ingawa bado jamii haina uelewa na mwamko wa kutosha katika kuandika wosia na mirathi wapo baadhi ambao huzingatia umuhimu wa mambo hayo hata hivyo bado kuna changamoto.

“Wakati mwingine hata marehemu anapokuwa ameacha wosia na akaandika mirathi yake bado kuna watu wengine hujitokeza na kuyakataa maoni yaliyoachwa na marehemu,” anasema.

Anaongeza “Labda unakuta katika hiyo jamii, walikuwa wakiishi na marehemu kwa mizozo, migogoro inapofika suala la kufuata kile alichokiandika wakati wa uhai wake hawakizingatii.

“Yaani inapotokea amefariki unaweza kukuta hata wale watoto wake ambao labda waligombana naye enzi za uhai wake wanakuja na kuanza kugombea mali za marehemu na unakuta wanataka kuchukua kila kitu chake,” anasema.

Anasema wakati mwingine watu hujitokeza kudai mali za marehemu ingawa enzi za uhai wake walikuwa hawamjali au hata hawaongei naye.

“Ni tofauti kabisa na jamii za nchi zilizoendelea kwamba mtu anapofariki watoto wake wanajua wazi kama walikuwa hawaelewani wanaachana na mali zake.

“Inabidi na sisi kama jamii inabidi tufike mahala tuchague, wakati fulani unaishi na wazazi wako mnakuwa na mizozo mikubwa mara nyingine hata hamtembeleani, hamsalimiani kwa muda mrefu.


“Lakini anapofariki wewe ndiyo wa kwanza kwenda kugombani mali, matokeo yake hata wale wachache ambao waliamua kumsaidia mzazi wako kufanya kila jambo,” anasema Wakili Msomi Kikondo (pichani).

Changamoto

Anasema hali hiyo huzua ‘tafrani’ hasa ikiwa marehemu anakuwa amechagua watu na kuwaandika katika andiko lake la wosia/mirathi kuwagawia mali zake.

“Labda ndiyo waliomsaidia alipokuwa hai anaamua kuwataja ili wagawiwe mali zake ikiwa ni sehemu ya shukran zake kwao, lakini anakuja mtu ambaye hakushiriki chochote naye anataka apatiwe mali, mizozo huanzia hapo,” anabainisha.

Anasema kwa kawaida mizozo huwa mingi kulingana na jinsi jamii inakosa ule uwelewa wa kutosha kuhusu masuala ya kisheria.

“Ukiangalia Sheria ya Usimamizi wa Mirathi Sura 352 inaeleza taratibu zote za usimamizi wa mirathi kuanzia pale mtu anapofariki na jinsi gani ya kufanya lakini ni watu wachache mno wanafahamu.

“Kimsingi inapotokea mtu amefariki jambo la kwanza kujiuliza ni je ameacha wosia au la, ikiwa imetokea wanasema ameacha wosia, swali la pili litakuwa je huo wosia unakubalika kisheria, kwamba taratibu za kuandika zilizingatiwa katika huo wosia au la,” anasema.

Anasema taratibu hizo hutegemea aina ya wosia unaoandikwa, kwa mfano ikiwa anayeandika anajua kusoma na kuandika wakati anauandika huo wosia anatakiwa kuhakikisha unashuhudiwa na watu wawili wazima wenye akili timamu.

Anasema wakati muhusika akiandika na kuusaini wosia huo ni lazima watu hao wamshuhudie akiusaini wosia huo.

Hata hivyo, Wakili Kikondo ambaye amebobea zaidi  katika masuala ya sheria ya matibabu anasema mara nyingi hushuhudia watu wakiandika wosia wodini wakiwa hoi kitandani.

“Wengi nimeona waandika wosia wakiwa hoi kitandani na wakati mwingine unakuta shahidi anakuwa mkewe au ndugu yake wa karibu, kimsingi mke hapaswi kuwa sehemu ya shahidi.

“Matokeo yake, wengi wanapofariki unakuta hakuna mtu anayejua kwamba aliacha wosia au wanapokwenda mahakamani wale mashahidi wanaotajwa wakiulizwa iwapo walishuhudia akiusaini wanasema hawakuwepo,” anasema.
Related image
Anaongeza “Kisheria hapo tayari ni utata na mahakama inaweza kuamuru kwamba kwa kuwa wosia huo haukufuata taratibu hautambuliki kisheria ingawa unaweza kukubaliwa iwapo ndugu na wanafamilia watakubaliana kuuheshimu wosia husika.

“Lakini huwa ni ngumu mno kwa sababu siku zote kwenye jamii zetu tunapoandika wosia tayari humo ndani kuna fukuto unakuta mtu labda amezaa watoto wengi kwa mama tofauti sasa anahofia mizozo itakayotokea anaamua kuandika wosia.

“Wosia wa namna hiyo usipofuata taratibu tayari kuna pande mbili, tatu au zaidi unakuta zinavutana au hata ukoo nao unavutana,” anasema.

Anaongeza “Wosia ukikosewa japo kidogo, lile kosa dogo hukuzwa na kuwa kubwa, inapofika hapo ule wosia hautakubalika mahakamani na itachukuliwa mtu huyo alikufa bila kuacha wosia.

“Kwa uzoefu wangu inapotokea mwanaume amezaa na mwanamke zaidi ya mmoja unakuta kila mama anataka mtoto wake apate urithi zaidi ya mwingine.

“Hata wale waliozaliwa wengi kwa mama mmoja wakati mwingine changamoto hujitokeza, unakuta wametofautiana kielimu, kiuchumi na mambo mengine mengi, ugomvi huwa mkubwa katika baadhi ya familia juu ya mali za marehemu.

“Au kuna baadhi ya makabila, ukoo unaona ni heri mali za marehemu zilithiwe na kaka au mdogo wa marehemu kwamba iendelee kubaki kwenye ukoo kuliko ikirithiwa na watoto wa marehemu wakihofia zitapotea,” anasema.

Hatua za kuchukua

Anasema ikitokea bahati mbaya mirathi inakuwa na shida inabidi familia ya marehemu itumie taratibu zinazotambulika kisheria kudai haki yao.

“Kumbuka ule wosia unaweza kukubalika au kukataliwa, ukikataliwa itachukuliwa ni sawa na mtu yule alifariki bila kuacha wosia, lakini yule anayeandika wosia ni muhimu akumbuke kuandika msimamizi wa mirathi yake.

“Katika kuteua msimamizi wa mirathi inahitaji umakini, inabidi ateue mtu ambaye ni mwadilifu kweli kweli, Ingawa hata asipoteua haibatilishi ule wosia anaouandika,” anabainisha.

Ufunguzi wa kesi

Wakili Kikondo anasema ikiwa marehemu aliacha wosia na katika wosia huo akataja msimamizi wa mirathi yake bado wosia huo unakuwa haufanyi kazi hadi pale unapopelekwa mahakamani.

“Hauwezi kufanya kazi ‘automatic’, lazima kesi ifunguliwe mahakamani, itasikilizwa na mahakama itatoa hukumu yake, yaani haiwezekani yule msimamizi wa mali za marehemu ‘kujitapa’ kwamba ndiye msimamizi ikiwa kesi haijapelekwa mahakamani,” anasema.

Anaongeza “Lazima upitiwe mahakamani, na apitishwe kwamba ndiye msimamizi wa mali hizo kwa sababu baada ya hapo kuna mambo ya msingi ya kufanya juu ya mali hizo.

Hubatilishwa

Wakili Kikondo anasema wosia huweza kubatilishwa lakini muhusika anapoubatilisha ni lazima aandike kwamba anaubatilisha ule wa kwanza aliouandika.

“Inahitaji umakini wa hali ya juu wakati unapoandika wosia na kuuhifadhi, ukizagaa zagaa si jambo zuri na umakini huhitajika pia katika kutafsiri sheria,” anasema.

Anasema mtu anapoandika wosia ni muhimu kubaki na nakala na kwamba huwa unahifadhiwa ama mahakama Kuu, kwa wakili au katika taasisi mbalimbali zinazotambulika kisheria.

“Kwa mfano Tanzania tunaweza kuhifadhi katika RITA lakini unaopeleka huko kuhifadhi lazima mtu (shahidi) wako ajue ili unapofariki aweze kutoa taarifa kule ulipohifadhi kusudi hatua zianze kuchukuliwa,” anasema.

Anaongeza “Ikitokea wosia umebatilishwa na mahakama ile familia ya marehemu hutakiwa kwenda kukaa kikao na ukoo kisha wataandaka muhtasari wa kikao hicho.

“Katika muhtasari huo watatakiwa kutaja mali zote za marehemu na warithi wake pia watateua msimamizi wa mirathi hiyo, lakini kuna tofauti kubwa ya kurithisha na kugawa mirathi.Image result for LAW

Madeni ya marehemu

“Kwa mfano marehemu ikiwa aliacha madeni msimamizi wa mirathi anayeteuliwa hapo huwajibika kulipa madeni yote yaliyoachwa na marehemu.

“Mnapotua msimamizi mteue mtu mwadilifu ingawa zipo sheria zinazosimamia iwapo atachakachua mali za marehemu atahukumiwa kama wanavyohukumiwa wahalifu wengine,” anasema.

Anasema msimamizi wa mirathi anapoteuliwa wanafamilia ni lazima warudi mahakamani ambako hupewa fomu namba moja na kuijaza kuomba usimamizi wa mirathi husika.

“Hapo watalipia gharama za faili na wataambatanisha fomu hiyo na cheti cha kifo au kiapo cha kifo cha marehemu, kisha wataambatanisha ule muhtasari wa kikao,” anasema.

Anasema watatakiwa kutoa tangazo katika gazeti lolote ndani ya siku 90 ili kutoa nafasi kwa wale wanaotilia shaka kuwasilisha malalamiko yao mahakamani.

“Kama hakuna malalamiko mahakama itampitisha yule aliyeteuliwa kusimamia mirathi husika lakini kabla hajagawa mali hizo lazima alipe madeni yote yaliyoachwa na marehemu,” anasisitiza.

Anasema hata hivyo wengi husahau kulipa madeni ya marehemu mara baada ya kukubaliwa kusimamia mirathi.

“Wanapopewa kibali tu huenda kugawa mali na kuwasahau kabisa wale waliokuwa wakimdai marehemu, ni makosa makubwa kisheria,” anasema.

Sheria mbadala

Anasema wakati mwingine sheria ya kidini hasa ya kiislamu huweza kutumika katika suala la usimamizi wa mirathi au sheria ya kimila.

“Lakini ili itumike sheria ya kiislamu ni lazima iwe marehemu alikuwa akiyaishi maisha ya dini hiyo vinginevyo hamuwezi kuitumia, au sheria ya kimila lazima wote wawili wawe wametoka katika kabila moja.

“Lakini ikiwa wameowana kutoka kabila tofauti hapo sheria ya kimila haiwezi kufanya kazi katika kugawa mali za marehemu hata hivyo katika miaka ya hivi karibuni sheria ya kimila imekuwa ikikosa nguvu kwani mambo mengi yanakwenda kinyume na haki za binadamu,” anabainisha.

Maulid Kikondo ni Daktari na Wakili wa Mahakama Kuu Tanzania anapatikana kwa nambari, +255 713 304 149, Unaweza kuwasiliana naye ikiwa unahitaji msaada wa kisheria yupo tayari kukusikiliza.

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement