NA VERONICA ROMWALD – DAR ES SALAAM
MAKAMU wa Rais, Samia Suluhu Hassan ameupongeza uongozi
na wafanyakazi wa Hospitali ya CCBRT kwa kuendelea kutoa huduma bora za
matibabu kwa wananchi.
Pamoja na hayo amesema bado ipo kazi kubwa kuhakikisha
jamii inafikishiwa ujumbe kuhusu tatizo la fistula na athari zake kwa afya ya
mama na uchumi kwa ujumla.
Mama Samia amesema hayo leo alipozungumza katika viwanja
vya Hospitali ya CCBRT ambako alifanya ziara kujionea huduma mbalimbali
zinazotolewa hospitalini hapo.
“Mliponifata kuomba kurekodi ule ujumbe ambao unasambaa
mtandaoni kwa njia ya sauti na video hata sikuwa naelewa kwa kina kuhusu tatizo
hili, mkanieleza na sikujua kwamba kwa kuzungumza kule kungesaidia kufikisha
ujumbe , kumbe imesaidia.
“Lakini bado ujumbe unahitajika kupelekwa kwa jamii siku
moja nikiwa kwenye mkutano kule Zanzibar wanawake walinifuata na kunihoji
kuhusu tatizo la fistula, nikaanza kuwaeleza, utaona namn ambavyo elimu hii
inahitajika zaidi hasa katika ngazi ya chini ya jamii tena ile masikini,”
amesema.
Ameongeza “Lazima tuwaelimishe kuhusu umuhimu wa kumuacha
mtoto akue ndipo aolewe na kubeba mimba kwani tatizo hili linaepukika ikiwa
msichana anaachwa kwanza akue na viungo vyake vikomae tayari kwa kuhimili ile
hali ya ujauzito,” amesema.
Awali akizungumza Ofisa Mtendaji Mkuu wa CCBRT, Erwin
Telemans aliiomba serikali kuipunguzia kodi hospitali hiyo ili iweze kuendelea
kutoa huduma bora kwa jamii.
Akizungumza, Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia,
Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu amesema serikali inakusudia kuirejeshea tena
Hospitali ya CCBRT ruzuku kama ilivyokuwa ikipatiwa hapo awali ili kuiwezesha
izidi kutoa huduma bora kwa wananchi.
Amesema serikali inatambua mchango mkubwa unaotolewa na
hospitali hiyo katika kuhudumia watanzania na kwamba imekuwa itoa huduma bila
kujali faida.
Chapisha Maoni