Recent Post


 


moja

Responsive Advertisement

Image result for road accident in tanzaniaGari ikiwa imeharibika vibaya baada ya ajali kutokea, picha na mtandao

NA VERONICA ROMWALD – DAR ES SALAAM

AJALI za barabarani ni janga si tu Tanzania bali duniani kwa ujumla, Shirika la Afya Duniani (WHO) linakadiria kila mwaka watu milioni 1.25 hufariki duniani kwa ajali za barabarani.

Kulingana na Shirika hilo, idadi hiyo ni sawa na vifo vya watu 3,400 kila siku, takwimu za WHO zinaonesha ajali za barabarani zinashika nafasi ya pili miongoni mwa mambo yanayosababisha vifo duniani.

Inakadiriwa asilimia 90 ya ajali hutokea katika nchi zinazoendelea ikilinganishwa na nchi zilizoendelea huku ajali zikionekana kusababisha vifo vingi kuliko hata maambukizi ya virusi vya ukimwi, kifua kikuu na malaria.

Shirika hilo linaeleza kundi linaloathirika zaidi na ajali za barabarani ni watu wenye umri wa kuanzia miaka 15 hadi 29.

Aidha, wengi wao huwa ni watumiaji wengine wa barabara ikiwamo watembea kwa miguu, waendesha pikipiki, baiskeli.

Kwa mujibu wa WHO ajali za barabarani hutokana na sababu mbalimbali hasa za makosa ya kibinadamu kama vile ulevi, mwendokasi, kutokuzingatia sheria za usalama barabarani, kutokuvaa kofia ngumu na kutokufunga mikanda.

Inaelezwa kati ya watu wanne wanaopata ajali kila siku duniani watatu huwa ni wanaume.

Shirika hilo linakadiria nchini Tanzania kila mwaka watu wapatao 16,000 hupoteza maisha kwa ajali za barabarani.

Shirika hilo linazionya nchi zote kwamba ikiwa hatua hazitachukuliwa huenda hali itakuwa mbaya zaidi ifikapo 2030 kuliko ilivyo sasa.

Nimekuwa nikiandika habari za afya kwa muda wa zaidi ya miaka mitano sasa, hiyo imeniwezesha kushuhudia na kuzungumza moja kwa moja (wodini) na watu mbalimbali walioathiriwa na matukio ya ajali.

Wengi wao huwa ni vijana huwa nakutana nao katika Taasisi ya Mifupa Muhimbili (MOI) ambako hufikishwa kwa matibabu.

Nakumbuka vema tukio la ajali ya gongo la mboto ambayo ilihusisha gari la mafuta ambalo lilianguka wakati likijaribu kupisha gari iliyokuwa ikija mbele yake ikiwa mwendo kasi.

Wakati dereva yule akijitahidi kupishana na gari lile lilimshinda akajipata gari yake ikiangukia mtoni, wananchi wakakimbilia kwenda kuchota mafuta na hatimaye baadae yalilipuka na kusababisha maafa.

Niliwaona majeruhi wa ajali ile, akiwamo utingo wa ile gari, nilibahatika kufanya naye mahojiano.. alikuwa na maumivu makali mno.

Kimsingi ajali nyingi hutokea kwa uzembe, maisha ya watu wale yalibadilika tangu pale, wapo waliopoteza viungo vyao na wengine walipoteza kabisa maisha yao.

Mzigo mkubwa kwa familia na Taifa, nguvu kazi zimepotea kutokana na uzembe wa mtu mmoja aliyedaiwa kuwa katika mwendo kasi.

Na ndipo hapo linapokuja wazo la kudhibiti mwendo kasi wa madereva, Jeshi la Polisi kwa namna moja au nyingine linajitahidi mno kutekeleza wajibu wake katika hilo, kwa kutumia ‘tochi’ za usalama barabarani.

Hivi karibuni nilisafiri kutoka Dar es Salaam hadi Morogoro kwa hakika nilifurahia safari yangu, zamani nilikuwa nikisafiri nakuwa na shaka na wasiwasi wa kule ninapokwenda, Je nitafika salama.

Hali imebadilika, angalau sasa ‘wazembe’ wanadhibitiwa hata hivyo haitoshi kusema kwamba tumeweza kubadili tabia.

Nadhani kampeni ya paza sauti ‘imeleta matunda’ lakini bado tunapaswa kuendelea kuelimisha jamii yaani madereva na abiria umuhimu wa kuzingatia alama za usalama barabarani.

Tukifuata kwa hakika alama za usalama barabarani itatusaidia kuepuka ajali zinazoweza kuepukika na hivyo kwa pamoja tukawa tumeokoa maisha ya watu wengi.

Ingawa changamoto inabaki kwa wenzetu wa bodaboda ambao wengi hujifunza vichochoroni na kuingia barabarani.

Hawa huwa hawajali hii ni njia ya abiria waenda kwa miguu au hapa natakiwa kusimama kwa sababu taa iliyowaka ni nyekundu na si ya kijani.

Huwa wanapita tu popote ni haki yao, lakini ndio hao ambao wengi huishia kuletwa MOI huku wakiwa viungo vyao vimeharibika vibaya na hivyo kulazimu madaktari kukata viungo vyao kama sehemu ya matibabu.

Lazima jamii ibadilike na kuheshimu alama za usalama barabarani ili tuepuke ajali za barabarani.

Makala haya kwa mara ya kwanza yametoka leo (Juni 4, 2018) kwenye gazeti la MTANZANIA ambalo nalitumikia

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement