Recent Post


 


moja

Responsive Advertisement
Tezi kibofuPicha inayoonesha mfumo wa uzazi wa mwanamume

Na Veronica Romwald, Dar es Salaam

SI jambo rahisi hata kidogo kukaa ndani ya chumba cha upasuaji na kushuhudia jinsi ambavyo madaktari wanafanya upasuaji kumtibu mgonjwa aliyelazwa mbele yao.

Kama una ‘roho nyepesi’ lazima utatamani au utaomba kabisa kutoka nje ya chumba hicho tena hasa hasa ikiwa ni mara yako ya kwanza kuingia ndani ya chumba hicho.

Hivi karibuni, nikiwa pamoja na waandishi wenzangu wa vyombo vingine vya habari tulipata fursa ya kuingia katika chumba namba mbili cha upasuaji katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH).

Katika chumba hicho madaktari bingwa wa upasuaji wa watoto wa Muhimbili na wenzao wa Hospitali ya King Faisal ya nchini Saudi Arabia walikuwa wanafanya upasuaji kwa njia ya matundu (laparoscopic).

                                                                                                                                                                                   Mwandishi wa makala haya akishuhudia upasuaji unavyoendelea.                                                                                                                                                                                                   
Niliona baadhi wakiogopa kutazama kilichokuwa kikiendelea binafsi nilijipa moyo konde na kushuhudia yote yaliyokuwa yakifanyika humo kwa zaidi ya saa mbili.  

Baada ya madaktari kumuandaa mgonjwa, mmoja alisoma orodha ya wanaoshiriki upasuaji huo kisha daktari aliyekuwa akiongoza upasuaji huo alifanya sala, wote wakaitikia amina. Ni utaratibu ulionivutia.

Upasuaji huu ulifanyika kwa siku kuanzia Februari 20 hadi 23, mwaka huu kwa watoto sita waliokuwa na matatizo mbalimbali.

Kati yao kuna ambaye alifanyiwa upasuaji wa kurudisha ndani utumbo wake ambao ulikuwa unatoka nje kila alipokuwa akijisaidia haja kubwa.

Wapo waliofanyiwa upasuaji wa kushusha kokwa za korodani, kufungua njia ya haja kubwa, katika makala haya nitagusia tatizo la kutoshuka kwa kokwa za korodani.

Unapozungumzia viungo muhimu katika mwili wa mwanamume basi huwezi kuacha kutaja korodani. Hiki ni kiungo cha kipekee ambacho kazi yake kuu ni kuzalisha mbegu za kiume na homoni za kiume iitwayo testosterone.
Upasuaji ukiendelea
 
Korodani inaposhindwa kufanya kazi yake sawa sawa hushindwa kuzalisha mbegu pamoja na homoni za kiume na matokeo yake mwanamume hushindwa kutungisha mimba.

Kawaida mwanamume anazo korodani mbili, moja katika upande wa kushoto na nyingine upande wake wa kulia. Korodani hutengenezwa tumboni na baadae hushuka hadi katika vifuko vyake vilivyoko nje ya mwili wa mwanaume.

Jinsi zinavyotengenezwa

Daktari Bingwa wa Mfumo wa Njia ya Mkojo (Urolojia) wa Muhimbili, Ryuba Nyamsogoro anasema hutengenezwa ndani ya tumbo la mtoto wa kiume, wakati mimba ikiwa katika kipindi cha kati ya mwezi wa sita na saba tangu ilipotungwa.
 
Anasema baada ya korodani kutengenezwa katika kipindi hicho tumboni mwa mama wakati wa ujauzito, huanza kushuka kuelekea kwenye vifuko vyake kupitia mrija wake wa Gubanakulamu.

Anasema hata hivyo muda wa korodani kushuka kutoka tumboni mwa mtoto kuelekea katika vifuko vyake hivyo unapofika kuna wakati mwingine hutokea  zikawa hazijashuka kutokana na matatizo mbalimbali.

“Hali hiyo huitwa korodani zisizoshuka,  Wanaume wengi hujikuta wakiwa na korodani moja isiyoshuka ingawa wakati mwingine huweza kutokea zote mbili zisishuke ila hii huwa ni mara chache mno,” anasema.

Daktari huyo anasema tafiti mbalimbali zinaonesha kwamba katika vizazi hai 100 vya watoto wa kiume kila mwaka ulimwenguni wanne huzaliwa wakiwa na tatizo hilo.

Sababu za kutoshuka korodani

Dk. Nyamsogoro anasema hata hivyo hakuna dalili zozote ambazo mjamzito anaweza kuziona ili kujua kuwa mtoto aliyembeba tumboni atazaliwa akiwa na tatizo hilo. Isipokuwa  zipo sababu mbalimbali ambazo huweza kuchangia mtoto kupata tatizo la korodani kutoshuka.
Mashine ambayo madaktari huitumia kufanya upasuaji wa kutoboa matundu

“Sababu moja wapo ni uchache wa homoni za kiume kwa mtoto iitwayo androgen. 
Homoni hii ya androgen ni ya muhimu mno kwa ajili ya viungo mbalimbali vya mwanamume sasa inapotokea zikapungua kwenye mwili wa mtoto husababisha hitilafu kwa viungo vyake mbalimbali ikiwamo korodani,” anasema.

Anataja sababu nyingine ni hitilafu ya korodani yenyewe pamoja na mrija wake uitwao ‘gubanakulamu’ambapo hitilafu hiyo hupunguza uwezo wa kushuka kwa korodani husika.

“Sababu nyingine ni mgandamizo mdogo tumboni kwa mtoto husika. Ili korodani ishuke kutoka tumboni na kwenda kwenye mfuko wake huhitajika kuwapo kwa msukumo ‘pressure’ ya kutosha kutoka ndani ya tumbo. Sasa ikiwa msukumo  uliopo hautoshi,  husababisha korodani kutoshuka. Mgandamizo huo hutokana na kuwapo kwa viungo vya kawaida vya mwili kama vile figo, ini, utumbo na vinginevyo,” anasema.

Hali ilivyo Muhimbili

Daktari Bingwa wa Upasuaji wa Watoto, Zaituni Bokhary anasema katika idara hiyo kila mwezi hupokea watoto wawili hadi watatu wenye tatizo hilo.

Zikibaki tumboni, hazai

“Kimsingi kokwa zinapaswa kushuka na kukaa katika vifuko vyake vya korodani ambavyo vipo nje ya mwili wa mwanamume. Inapotokea zimebaki ndani ya tumbo ni hatari,” anasema.

Anasema mtoto ambaye kokwa zake hazijashuka kwenye vifuko vya korodani huwa katika hatari ya kushindwa kuzalisha pindi atakapofikia umri wa kuzaa.

“Uwezekano wa mtoto ambaye kokwa zake zimebaki tumboni kushindwa kuzalisha ni mkubwa mno ikilinganishwa na wengine ambao kokwa zao zimeshuka kwenye vifuko ipasavyo,” anasema.

Anasema iwapo kokwa hazijashuka mahala pake mtoto huhitaji kufanyiwa upasuaji wa mapema ili kuzishusha kumuepusha na hali hiyo.

“Ndiyo maana tuliwafanyia upasuaji watoto hawa ili kuzishusha kokwa zao, upasuaji huo ulifanyika kwa njia ya kisasa ya matundu madogo.

“Upasuaji huo uitwao kitaalamu (Laparoscopic) huu ni tofauti na ule wa kufungua tumbo (open surgery), hapa tunakuwa tunatumia vifaa maalumu kutoboa matundu kufikia eneo ambalo tunalihitaji na kuanza kufanya upasuaji,” anasema.

Anasema mmoja wa watoto hao ana umri wa miaka minane ambaye mwishoni mwa mwaka jana alifanyiwa upasuaji wa awali wa kuzisogeza kokwa zake karibu zaidi na korodani.

“Huyu kokwa zake zilikuwa mbali mno tukazisogeza hivyo tumekamilisha upasuaji huo na tayari tumezishusha kokwa kwenye korodani na hivyo kumtoa katika hatari hiyo,” anasema.

Daktari huyo anasema kufanikiwa kwa upasuaji huo ni hatua kubwa kwa hospitali hiyo ambayo sasa inatara mkubwa  kufanyika katika hospitali hiyo ambayo inatarajia kufanya mageuzi makubwa ya kimatibabu.

Utajuaje kokwa hazijashuka

Dk. Nyamsogoro anasema mara nyingi huwa wanaweza kutambua  tatizo hilo la kutokushuka kwa korodani kwa kutumia njia kuu mbili.
Anataja njia hizo kuwa ni kuona na kugusa, kwa kuona huwa wanabaini tatizo kwa kuzitazama tofauti iliyopo kwenye ngozi ya mfuko wa korodani.

“Ukitazama vifuko vya korodani ya mtoto mwenye tatizo utaona ngozi ya upande ambao haijashuka ipo tofauti na ile ambayo imeshuka. Ile ambayo haijashuka utaona ngozi yake haijakomaa sawa sawa na iwapo utaigusa utakuta haipo kabisa.

“Wakati mwingine unaweza kukuta ipo katika sehemu ya juu eneo la tumboni au kwenye ‘kinena’ na au kwa ndani ya tumbo lakini siwashauri wazazi kuwagusa watoto kwa sababu wanaweza kuwaumiza ni vyema wawalete hospitalini tuwachunguze,” anasema.

Daktari huyo anasema hiyo ni kwa sababu wakati mwingine pamoja na kutumia njia hizo za kuona na kugusa huwa ni vigumu kuweza kubaini tatizo hadi wanapokwenda kuchunguza kwa kutumia vipimo maalumu.

“Hivyo mara nyingi huwa tunatumia vipimo vya MRI na Ultra sound. MRI ni kipimo kizuri zaidi kwani ina uwezo wa kutubainishia hadi mahala ambako korodani imejificha,” anasema.

Anasema hata hivyo mara nyingi huwa wanawashauri wakunga kuhakikisha wanawachunguza watoto punde tu baada ya kuzaliwa kwani huwa rahisi kubaini kama watakuwa wana tatizo hilo.
“Huwa pia tunawashauri wazazi na walezi wanaowalea watoto wachanga kuwa wanawachunguza maana ni rahisi na wao kuweza kuona kama kuna tofauti kati ya korodani moja na nyingine na iwapo watazibaini basi wawapeleke hospitalini,” anasema.

Hugeuka kuwa saratani.

Dk. Nyamsogoro anasema katika kliniki yao ya Ulorojia wamekuwa wakipokea hadi watu wazima wanaosumbuliwa na tatizo hilo la korodani kutoshuka.

“Wengi wao wapo katika umri wa kati ya miaka 25 hadi 30. Lakini kwa kuwa wanakuwa wamechelewa mno kuja hospitali matibabu yao huwa ni magumu mno,” anasema.

Anasema kutokana na ugumu wa matibabu hayo matokeo yake hulazimika kufanyiwa upasujia wa kuiondoa korodani husika kwani iwapo itaachwa huko ndani ilikojificha madhara makubwa huweza kutokea siku za usoni za maisha yake.

Madhara yenyewe   

Daktari huyo anasema iwapo korodani hiyo itaendelea kubakia huko ndani ya tumbo husababisha maji yaliyoko tumboni kuteremka chini kupitia mrija wa korodani hali ambayo baadae husababisha tatizo la ngiri maji (henia).

“Tumboni kuna maji maji mfano wa mate, korodani isiposhuka kupitia mrija wake matokeo yake ni kwamba mlango wa kuipitisha ili ikae kwenye sehemu yake huendelea kubakia wazi ukisubiri ishuke.

“Kwa hiyo maji maji hayo hutumia uwazi huo kushuka ndipo inatoke tatizo la ngiri maji (henia) na wakati mwingine mnaona watoto wanapata hadi tatizo la busha,” anafafanua DK. Nyamsogoro.

Anasema hata hivyo wakati mwingine huweza kutokea korodani ya mtoto ikashuka lakini bado mlango huo ukabaki wazi na ndio maana upo umuhimu wa kwenda kumpima afya ya korodani zake kila baada ya kipindi fulani.

Athari zaidi

Dk. Nyamsogoro anasema athari nyingine inayoweza kutokea iwapo korodani husika itaendelea kubakia ndani ya tumbo ni kugeuka kuwa saratani.

Anasema korodani isiyoshuka ina uwezekano mkubwa wa kugeuka kuwa saratani ingawa si mara zote na ndio maana hulazimika kuishusha na iwapo itagoma kabisa huwa tunaiondoa kwa njia ya upasuaji.
“Korodani isiyoshuka mara nyingi huwa kuna uwezekano wa kugeuka kuwa saratani kuliko ile iliyoshuka, ikiwa imebaki tumboni huwa tunajaribu kuishusha lakini ikishindikana tunaiondoa kwa upasuaji,” anasema.

Anasema ile iliyogoma kushuka hulazimika kuondolewa kwa njia ya upasujia haraka kwani ikiendelea kubakia huko ndani husababisha matatizo makubwa kwa mwanaume husika.

“Ingawa na ile ambayo tunaweza kufanikiwa kuishusha inaweza akupata saratani lakini ikiwa nje pale kwenye mfuko wake huwa rahisi kuitibia na wakati mwingine kupona kabisa kuliko ikiwa ndani ya mwili hapo huwa tunaiondoa kwa upasuaji,” anasema.

“Na ndio maana nahimiza watu wawahi hospitalini hasa wale wenye watoto wa kiume wenye tatizo ili tuwasaidie kuishusha kwa njia ya upasuaji iwe kwenye sehemu yake inayotakiwa ili hata itakapotokea ikataka kugeuka kuwa saratani iwe rahisi kuitibu kwani inapona,” anasema.
Kila kinachofanyika lazima kiandikwe

Anaongeza hata hivyo matibabu hayo huwa yanafanyika kwa watoto waliotimiza umri wa miezi sita hadi mwaka mmoja na nusu kwani kama alizaliwa zikiwa hazijashuka huweza kushuka katika kipindi hicho.

“Wakiwahi mapema katika kipindi hicho huwa wakati mwingine si lazima wafanyiwe upasujia badala yake huwa kuna dawa tunawapatia za kihomoni ambazo huwasaidia kuzishusha,” anasema.

“Hata hivyo dawa hizo zikishindwa kumsaidia kuzishusha ndipo huwa tunamfanyia upasuaji... huwa rahisi kwa mtoto mdogo kuliko mtu mzima kwani viungo vyake vinakuwa vimekomaa.

“Lakini nawashauri wanaume wenye umri mkubwa nao waende hospitali kuchunguza afya zao ili kama watakuwa na tatizo waweze kusaidia kwa kuindoa korodani hiyo kabla haijaleta madhara ikiwa huko ndani ya tumbo,” anatoa rai.

2 Maoni

  1. Mimi na matatizo ya korodani kuto kushuka sasa nifanyeje

    JibuFuta
    Majibu
    1. Pole rafiki, tunakushauri uende hospitalini ili kufanyiwa uchunguzi wa kina na wataalamu

      Futa

Chapisha Maoni

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement