Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya nchini (DCEA) imezidi kuchukua hatua na ‘kukunjua makucha’ yake dhidi ya watu wanaojihusisha na biashara ya dawa za kulevya, awamu hii inawashikilia watu watatu akiwamo balozi wa nyumba 50, Mtaa wa Juwaje, Kunduchi Pwani, Kulwa Shamas (49).
Shamas anashikiliwa kwa tuhuma za kujihusisha
na biashara hiyo, watuhumiwa wengine wanaoshikiliwa ni Adadhati Mchongeza(20)
na Emmanuel Msakuzi (23).
Mchongeza na Msakuzi walikamatwa kwa pamoja na
maafisa wa DCEA wakiwa wameifadhi dawa aina ya heroin zenye ujazo wa gramu 400
pamoja na majani ya bangi puli moja katika mfuko wa nailoni.
Kamishna Jenerali wa Mamlaka hiyo, James Kaji amebainisha hayo leo
Jijini Dar es Salaam alipozungumza katika mkutano na waandishi wa habari.
Amesema watuhumiwa hao walikamatwa Januari 22 mwaka huu katika
eneo la kunduchi Pwani, Kauzeni Jijini humo wakiwa na unga unaodhaniwa kuwa
dawa za kulevya aina ya heroin sambamba na majani makavu ya bangi puli moja
sawa na kete 30 za bangi.
Amesema maafisa wa DCEA walifanikiwa kufanya upekuzi hatimaye
kukamata dawa za kiasi cha dawa hizo zikiwa zimeifadhiwa ndani ya mfuko wa
nailoni.
Kamshina Jenerali Kaji amesema Mamlaka hiyo inaendelea kuwashikilia
watuhumiwa hao na kwamba watafikishwa mahakamani baada ya taratibu za kisheria
kukamilika.
Amewataka wananchi kuendelea kutoa taarifa kwa Mamlaka hiyo ili
DCEA iendelee kufanya kazi ya kukomesha vitendo hivyo.
Pamoja na hilo, Kamshina Jenerali Kaji amesema katika kipindi cha
mwezi Novemba mpaka Disemba mwaka jana DCEA imefanikiwa kushinda kesi
tatu mahakamani zinazohusisha mapapa wa dawa za kulevya nchini ambao wamefungwa
jela kwa miaka tofauti tofauti.
Ametaja majina ya mapapa hao ni pamoja na mfanyabiashara maarufu
Jijini Tanga Yanga Omary Yanga maarufu Rais wa Tanga na kuhukumiwa miaka 30
jela baada ya kukutwa na hatia ya kusafirisha dawa za kulevya aina ya Heroin
uzito wa gramu 1052.63
“Mwingine ni Ayubu Mfaume maarufu kiboko ambaye alihukumiwa
kifungo cha miaka 20 kwa kosa la kusafirisha heroin zenye uzito wa
gramu 251.25,” amebainisha.
Ameogeza “Watuhumiwa wengine ni Raia wa Iran ambao walitiwa
hatiani kwa kosa la kusafirisha dawa za kulevya aina ya Heroin zenye ujazo wa
gramu 111.02 katika bandari ya Hindi ambapo mpaka sasa wanatumikia kifungo cha
miaka 30.
Vilevile amesema DCEA imefanikiwa kufungua vituo vitatu vya
kutolea tiba ya methadone katika mkoa wa Tanga , Bagamoyo, pamoja na hospital
ya Tumbi Pwani.
"Mamlaka
imeogeza wigo wa upatikanaji wa tiba ya uraibu wa dawa za kulevya kwa kuongeza
vituo vingine vitatu vya kutolea tiba ya methadone"amesema Kamshina
Jenerali Kaji.
Ameongeza “Vituo hivyo vipo katika maeneo ya Segerea, Mbagala Rangi
Tatu na Tegeta vinatarajiwa kuanza kutoa huduma Februari mwaka huu .
Amesema mpaka sasa DCEA inaendelea Kudhibiti vitendo
vinavyojiusisha na biashara haramu ya dawa za kulevya kwa kiasi kikubwa.
"Sisi
hatuna mchezo katika suala la kukamata watu wanaojiusisha na biashara haramu ya
dawa za kulevya tukikumata unakwenda jela,"amesisisitiza Kamshina Jenerali
Kaji.
Amesema vile vile DCEA inaendelea kutoa elimu juu ya tatizo la
dawa za kulevya kwa njia mbalimbali ikiwemo matukio makubwa ya kitaifa pamoja
na vyombo vya habari.
"Mamlaka imeandaa mwongozo wa uelimishaji kwa wadau wanaofanya uelimishaji kwa makundi mbalimbali ya kijamii unaotarajia kukamilika mwishoni mwa mwaka huu wa fedha," amebainisha.
Chapisha Maoni