Wakazi wa Tanga waliojitokeza katika kampeni maalum ya uchunguzi wa saratani ya mlango wa kizazi pamoja na saratani ya tezidume wakisikiliza jambo kwa makini kutoka kwa mtaalamu.
Uchunguzi wa awali wa saratani ya mlango wa kizazi ni
muhimu kuzingatiwa hata kama mwanamke ameacha kujamiiana na hata kama katika
uchunguzi aliowahi kufanyiwa hakukutwa na mabadiliko yoyote.
Muuguzi Mkuu wa Taasisi ya Saratani Ocean Road (ORCI),
Jesca Kawegere ametoa rai hiyo leo, wakati alipokuwa akijibu swali la mwanamke
(jina linahifadhiwa) aliyejitokeza katika kampeni ya uchunguzi wa awali wa
saratani ya mlango wa kizazi inayofanyika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Tanga -
Bombo.
Mama huyo ambaye alitaja wazi kwamba yeye ni mwathirika wa
Ukimwi, alihoji kuna umuhimu gani kuendelea kufanya uchunguzi wa awali ikiwa
katika uchunguzi aliowahi kufanyiwa mara kadhaa hakukutwa na mabadiliko yoyote
na sasa ameacha kujamiiana.
“Nazingatia matumizi ya dawa za ARVs, nimechunguzwa mara
kadhaa saratani ya mlango wa kizazi, sijakutwa na mabadiliko ya awali, nimeacha
kujamiiana, Je! bado kuna sababu za mimi kuendelea kuchunguzwa saratani hiyo,?
Alihoji.
Akijibu swali hilo, Muuguzi Mkuu wa ORCI, Kawegere amesema
“Ni muhimu kuendelea kufanya uchunguzi wa awali wa saratani ya mlango wa kizazi
hata kama mwanamke ameacha kujamiiana.
“Kwa sababu ni vigumu kujua, kubaini lini kirusi cha Human
Papilloma (HPV) kinachosababisha ugonjwa huo kitaleta mabadiliko katika mwili
wake na hatimaye kuleta athari kubwa endapo hakitagundulika mapema,” amesema.
Amesema kirusi cha HPV huweza kukaa ndani ya mwili wa mwanamke hata kwa miaka 10 na kuanza kuonesha athari na ndiyo maana wanahimiza uchunguzi wa awali mara kwa mara.
Akitoa elimu kuhusu saratani ya tezidume, Mtaalamu Mbobezi
Masuala ya Afya Jamii wa Taasisi ya Saratani Ocean Road (ORCI), Johnson
Katanga, (pichani) amehimiza wanaume hasa wenye umri kuanzia miaka 40 na kuendelea
kujenga utamaduni wa kuchunguza saratani hiyo mara kwa mara.
“Sasa hivi tuna kipimo cha damu, kama vile unavyochunguzwa malaria, kipimo hicho kinatuwezesha wataalamu kufanya uchunguzi wa awali wa saratani ya tezidume, msiogope,” ametoa rai.
Wananchi waliojitokeza kwenye uchunguzi huo ambao leo ni
siku ya pili, wameshukuru wataalamu wa ORCI pamoja na uongozi wa Hospitali ya
Rufaa ya Mkoa wa Tanga - Bombo kwa kuwafikisha huduma hiyo rafiki.
Wananchi wakisikiliza jambo kwa makini, wataalamu wa ORCI wamepiga kambi maalum ya uchunguzi wa awali wa saratani ya kizazi kwa wakazi wa Tanga, kambi hiyo iliyoanza Januariu 28, 2021 inayotarajiwa kukamilika Januari 30, 2021 imeenda sambamba na utoaji wa mafunzo kwa watoa huduma za afya zaidi ya 25 wa Mkoa huo.
Chapisha Maoni