Recent Post


 


moja

Responsive Advertisement


Na Veronica Mrema – Dar es Salaam

Ujauzito/mimba, kawaida hukaa ndani ya tumbo la mama kipindi cha miezi tisa, tangu pale yai lake lililopevuka lilipoungana na mbegu ya baba na uumbaji wa kiumbe kipya kufanyika hadi kuzaliwa.

Ki-uhalisia miezi tisa ni kipindi kirefu mno, lakini si kwake Theresia Mushi katika mahojiano maalum na MATUKIO NA MAISHA BLOG hivi karibuni ndani ya Hospitali ya Taifa Muhimbili {MNH}, anasimulia magumu aliyoyapitia kipindi cha mwezi mmoja alicholazwa wodini akiuguza mwanawe.

“Mimba yangu haikunisumbua kabisa, nilikuwa nakula kama kawaida tofauti na wengi huchagua chakula, mimi sikuwa nachagua na nilikuwa nakula haswa.. sikuwa naumwa-umwa, niliendelea na shughuli zangu kama kawaida, nilikuwa nimeajiriwa duka moja la vifaa vya simu huko Kariakoo.

Anasema alipojihisi u mjamzito, ilipofika miezi mitatu ndipo alianza mahudhurio ya kliniki huko alifanyiwa uchunguzi kwa kipimo cha Ultra Sound awamu mbili tofauti na nyakati zote mtoto alionekana amekaa vizuri tumboni.

“Desemba 24, 2016 nilijifungua kwa upasuaji katika Hospitali ya Palestina, nilikuwa nashuhudia kila kinachoendelea, nilikuwa naweza kuzungumza na wataalamu {sikuchomwa sindano ya kulala moja kwa moja}.

“Walipomtoa walinionesha, nilimuona mwanangu utumbo wake ulikuwa upo nje,” anasimulia.

Theresia anasema aliogopa mno, alishangaa na maswali lukuki yalianza kukatisha kwenye ufahamu wake moja baada ya jingine, hakuwa na majibu… alikosa raha, furaha na amani ilimtoka.

“Ni mtoto wangu wa kwanza, nilishtuka… sikuwahi kuona hata kwenye familia yetu haijawahi kutokea wala sijawahi kusikia, tatizo hili,” anasema.

Anaongeza “Wataalamu waliniambia mwanangu atawahishwa Muhimbili huko atapata msaada zaidi, walinieleza wazi kupona ni 50% kwa 50%, niliogopa.. walinipa moyo niombe Mungu, atapona.

“Walimpeleka huko, mimi nilibaki Palestina, ndugu walipofika nilikosa cha kuwaeleza… niliishia kuwaambia mwanangu ana tatizo kubwa na amepelekwa Muhimbili.

“Walinisihi nisihofu kwa kuwa amewahishwa huko, atapona. Nilipumzishwa kwa muda kiasi baadae nilipelekwa Muhimbili, nilikuta tayari wamempa huduma ya kwanza.

“Ingawa utumbo bado ulikuwa nje lakini sasa ulifunikwa na mfuko mbadala,” anasimulia.

NINI KILITOKEA?

“Kitaalamu tatizo la kuzaliwa utumbo nje/ tumbo wazi huitwa ‘Gastroschisis’,”  anasema Daktari Bingwa wa Upasuaji wa Watoto Muhimbili Zaitun Bokhari.

Dkt. Bokhari anafafanua zaidi “Ni miongoni mwa matatizo ya kuzaliwa nayo ambayo hata hivyo yanaweza kuepukwa katika kipindi cha miezi mitatu ya mwanzo ya mimba.

“Kipindi cha miezi mitatu ya kwanza, ni cha muhimu mno mama kukizingatia, kimsingi mama ndiye anaweza kupredict ‘kubashiri’ afya ya mtoto wake.

“Mtindo wake wa maisha… aina ya vyakula anavyokula kipindi hicho, jinsi anavyohudhurfia kliniki ndivyo afya ya mtoto wake.

Anaongeza “Ki-baiolojia katika miezi mitatu ya kwanza, kitaalamu tunaita ‘Organogenesis’ ni kile kipindi ambacho zile ‘organs’ {viungo muhimu vya mwili ikiwamo utumbo’ hutengenezwa yaani zina-forms ile ‘mesoderm’ na ile ‘physiology’ inaanza kuonekana.

“Ndiyo maana ile miezi mitatu ya mwanzo ni muhimu sana ikiwa mtu anataka kupata mtoto mzuri, kwa sababu pia akiwahi kuanza mahudhurio ya kliniki na kuzingatia kule ataelekezwa jinsi ya kula na atapewa dawa za kumuepusha mtoto na magonjwa mbalimbali.

“Kimsingi, kipindi cha ujauzito kile chakula anachokula mama hakimsaidii tu yeye, kinamsaidia mpaka mtoto aliyembeba tumboni mwake, kadhalika zile dawa ambazo anakuwa anazitumia.

“Ni kipindi muhimu kuzingatia ulaji unaofaa na kuacha mtindo mbovu wa maisha kwa mfano unywaji wa pombe kupitiliza, nakadhalika.

Anasema hata hivyo changamoto ni pale wakina mama wengi huanza kiliniki kwa kuchelewa yaani  ile miezi mitatu inakuwa imeshapita mno. Si sahihi.

TAKWIMU ZILIVYO

Inakadiriwa kila mwaka duniani mtoto mmoja hadi wawili kati ya 100,000 huzaliwa na tatizo hilo na Ukanda wa Kusini mwa Jangwa la Sahara {Tanzania ikiwamo} takwimu zinaonesha tatizo ni kubwa zaidi, kulingana na tafiti mbalimbali.

“Miaka ya nyuma uliweza kuisha mwaka hatujapokea mtoto mwenye tatizo hili, wengi walifichwa majumbani na kupoteza maisha, lakini sasa kwa mwezi tunaweza kuona mtoto mmoja hadi watano.

“Kwa sababu ya teknolojia duni pia hatukuweza kuokoa maisha yao, wengi walipoteza maisha kwa 95% hadi 100%, lakini sasa tuna mbinu ya kisasa zaidi na mafunzo tumeweza kuokoa uhai kwa 38%,” anasema.

KIPINDI KIGUMU

Theresia anasema walikaa Muhimbili kipindi cha mwezi mmoja mwanawe akihudumia, anakumbuka namna ilivyokuwa changamoto kubwa kwake nyakati hizo.

“Mtoto alikuwa wodi namba 36 kule mnakwenda tu kuwaona na nyie wazazi kurudi katika jengo la Magufuli {Hayati Rais wa Awamu ya Tano wa Tanzania}.

Anasimulia, mwanzoni nilizuiwa kumnyonyesha moja kwa moja, maziwa yalikuwa mengi niliumia roho kwa kweli kwa kushindwa kumpa ziwa mwanangu.

“Nilielekezwa jinsi ya kuyakamua, nilimpa kwa kipimo maalum, roho ilikuwa inaniuma… lakini sina jinsi… ule utumbo ulikuwa unarudishwa ndani kidogo kidogo.

“Katika ile wodi ya wazazi kulikuwa na vitanda vya watu sita, nakumbuka ‘round’ ya kwanza, ya pili na ya tatu, wenzangu walikuja na watoto wao wenye matatizo mengineyo ikiwamo kichwa kikubwa, ‘njiti’, matatizo ya moyo na mengineyo, walifariki dunia.

 “Nilikuwa namuomba Mungu, nasema Mungu wangu ni jaribu gani, mbona hivi, unakuta mwengine anaruhusiwa kabisa kesho mtandoka, lakini mwanawe anafariki.

Anaongeza “Nilijikuta nawaambia ndugu zangu, nia yangu ya kuomba nihamishwe kutoka wodi ile na ikibidi niondoke kabisa kurudi nyumbani, ila walinitia moyo na huku madaktari wakijitahidi mno, kumsaidia mwanangu.

“Hatimaye tuliruhusiwa baada ya hali yake kuonekana ipo vizuri, siku tuliyoondoka wodini kurudi nyumbani wengi walinipongeza wakisema mimi ni mwanamke jasiri

HATUA ZA UKUAJI

Theresia {Pichani na mwanawe huyo hivi sasa} anasema ni kipindi ambacho kilimpa wakati mgumu pia, kile cha ukuaji.

“Nilikuwa nawaza mno ataweza kutembea?, ataweza kutambaa?... niliwaza mno zile hatua za mtoto, ataweza kuongea? Nakadhalika.

“Kumbuka kule wodini mwezi mzima alikuwa tu amelala, nilikuwa namnyoosha nyoosha viungo, nilikuwa kumuuliza Mungu atatembea kweli? Basi hata asipoongea aweze kutembea japo nitaweza kumtuma mahala.

“Nilipoondoka hospitali nilisema nitamnyonyesha mwanangu hadi afikishe miezi sita, alipolia nilihisi vibaya, lakini nilimpenda na kujitahidi kumsaidia, nilishauriwa nianze kumpa chakula baada ya miezi sita.

KLINIKI YA CHANJO

Anasema siku ya kwanza alipompeleka wataalamu walimshangaa kwani alikuwa na uzito wa gram 900 huku kadi yake ikionesha alizaliwa na kilogram 3.

“Walinihoji kwanini, niliwaeleza alizaliwa na tatizo na Muhimbili waliniaelekeza aendelee na chanjo kwani hamna tatizo lolote, waliwasiliana nao ndipo walianza kumpa huduma.

“Sikuwa naweza kumueleza kila mtu, maana nilipomvalisha nguo alionekana tu kama mtoto wa kawaida, japo wapo pia walioniuliza au nilijifungua ‘njiti’ {kabla ya wakati}, alipungua mno.

“Lakini sasa ni kijana mkubwa, aliweza kupitia hatua zote za ukuaji kama watoto wengine, sasa yupo shule kwa kweli nina furaha, mama yangu alikuwa akinitia moyo na kuniombea, namshukuru mno Mungu.

Anaongeza “Darasani yupo vizuri anapenda kuchora katika mtihani wake amepata 95% kwa somo hilo, somo la ‘reading’ amepata 95% na hesabu 69%, ila kuchora ndilo analolipenda zaidi.

“Nilipojifungua, nililazimika kuacha kazi niliyokuwa nafanya kariakoo, nilikaa kwa muda wa miaka minne nikimuhudumia mwanangu, nilihisi nahitaji kuwa karibu naye zaidi.

“Kwa kuwa sasa amekua, nimehamia Dodoma huko nimeajiriwa huko na mama yangu anaishi na mjukuu wake, napambana kwa ajili ya maisha yangu na yake ili asome.

“Nawashukuru wataalamu waliomsaidia, naishukuru pia Serikali kwa kuboresha huduma za afya na hapa Muhimbili walinisaidia mno maana sikuwa na bima ya afya kipindi hicho.

“Sasa natamani naye siku moja awe daktari bingwa aokoe uhai wa watoto wengine wanaozaliwa na matatizo,” anasema.

Dkt. Zaitun ambaye pia ni Mkuu wa Kitengo cha Watoto Muhimbili anasema wanamshukuru Mwenyezi Mungu kuwawezesha kuokoa uhai wa mtoto huyo ni mafanikio ambayo Muhimbili, inajivunia.

“Lakini bado nasisitiza pamoja na mafanikio haya, wito wangu kila siku kwa wanawake ni muhimu mno kuzingatia kipindi cha kwanza cha miezi mitatu ya mimba unapojihisi ni mjamzito.

“Nitoe rai kwa jamii pia, linapotokea tatizo la ki-afya mara nyingi nimeshuhudia mama akikimbiwa na mwenza na kuachiwa kulea mtoto peke yake, hili si jambo linalofurahisha.

Anaongeza “Ni muhimu wenza kuendelea kuwa pamoja kulea mtoto, baba akiwa karibu na mama wakilea pamoja, inamsaidia hata mama kuwa na afya njema ya akili.

“Wengi wanaokimbiwa huwa na msongo wa mawazo na hata kushindwa kupata matokeo chanya ya tiba mapema kuliko wale ambao wenza {wanaume} huwa karibu zaidi,” anasisitiza.

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement