moja

Responsive Advertisement


Na Veronica Mrema

Historia kubwa Barani Afrika kwa mara ya kwanza imeshuhudiwa, watafiti nguli, wataalamu wa masuala ya Magonjwa Yasiyoambukiza [NCD’s], watunga sera na watu wenye NCD’s wakijadili kwa kina pamoja.

Mjadala ulioangazia namna gani Bara hilo litaongeza kasi katika kukabili NCD’s kwani idadi kubwa ya raia wake hivi sasa wanaugua na wengi wanapoteza uhai, kila mwaka.

Ni magonjwa ambayo mtu yeyote anayeugua hawezi kumwambukiza wengine, ingawa katika kundi hili la magonjwa yapo pia baadhi yanayorithiwa.

Yaani mtu anaweza kuzaliwa na ugonjwa kwa kurithi vinasaba vya ugonjwa husika kutoka kwa mzazi / wazazi wake, kwa mfano Siko Seli.

“Nikiwa ‘ki-changa’ mno muda mwingi nilikuwa nalia sana, wazazi wangu hawakuelewa kilichokuwa kinanisumbua,” anasema Edith Mukantwari.

Ni raia wa Uganda anasimulia maisha yake halisi ya utotoni, ilikuwa kipindi kigumu zaidi alichopitia, muda mwingi na mara kwa mara alilazwa hospitalini kupatiwa matibabu.

Aliishi hivyo hadi alipofikia umri wa miezi minane, alipofanyiwa uchunguzi wa kina na kugundulika hospitalini, amezaliwa na ugonjwa wa Kisukari aina ya kwanza [T1D].

Shirika la Afya Duniani [WHO] inautaja ugonjwa wa Kisukari ni muuaji wa kimya-kimya kwa raia wengi Barani Afrika.

WHO inaeleza kipindi cha 2011 hadi 2021 Afrika ilirekodi ongezeko la juu mara tano zaidi la T1D kwa kundi la watoto na vijana balehe chini ya umri wa miaka 19.

WHO inasisitiza ikiwa juhudi hazitafanyika hali hiyo huenda idadi itaongezeka kutoka watoto wanne katika kila watoto 1,000 wenye T1D hadi watoto 20 kwa kila watoto 1,000.

Ni 36% ya nchi za Afrika zilizoweza kuweka dawa muhimu katika vituo vyake vya kutolea huduma za afya kwa mujibu wa ripoti ya WHO ya mwaka 2019.

Edith anasema bado kuna kundi kubwa la watu wenye T1D bado hawajatambuliwa lakini pia hata waliotambuliwa wengi hushindwa kumudu gharama za matibabu kwani ni kubwa.

“Nakumbuka, hata mimi kabla sijagundulika nimepata kutibiwa mara nyingi homa, hata nilipokuwa katika shule moja ya bweni niliwahi kuugua lakini nilipopelekwa hospitalini hawakutibu inavyopaswa.

“Ilipelekea kupoteza kwa kiasi fulani uwezo wangu wa uoni, usiku niliteseka mno kwa kupata haja ndogo mara nyingi kila baada ya dakika 30.

Anasimulia “Nilikuwa nalala na ndoo chumbani kwangu ili nijisaidie humo, ni miaka 16 sasa naishi na T1D.

“Si maisha mepesi  … ni lazima nipate sindano kila siku ili hali yangu iwe sawa na niweze kuendelea na maisha yangu mengine kama watu wengine wasio na ugonjwa,” anasimulia.

‘NILIKIONA KIFO’

Saratani ni kati ya NCD’s ambazo zinaathiri pia raia wengi wa Afrika na hata kusababisha vifo.

Akiwa na umri wa miezi 9 Mosses Echodu aligundulika ana ugonjwa wa Saratani na tayari ulifika hatua ya nne, ambayo kwa kawaida ni ngumu kutibika na kupona.

“Nilikuwa naishi na bibi yangu, mama yangu alikuwa amerudi shule,[alijifungua mimi akiwa na umri mdogo],” anabainisha.

Anasimulia “Siku moja nilipokuwa nikicheza na wenzangu ghafla nguvu ziliniishia, nilijihisi vibaya, nilirudi nyumbani.

“Nilipelekwa hospitalini mara kadhaa, walikuwa wakinitibu homa niliyokuwa nayo,” anasema.

Anasema ni hadi pale mjomba wake mmoja alipofika, alimchukua kutoka kijijini huko Entebbe na kumpeleka hospitali moja iliyopo Kampala, Uganda.

“Kipindi kile, usafiri ulikuwa changamoto kubwa, tulisafiri takriban saa sita kufika Kampala kutokea Entebbe tofauti na sasa unaweza kufika kwa saa mbili,”.

Anasema ndipo aligundulika ana saratani na kuongeza, “Hali yangu haikuwa nzuri, nilijua mwisho wangu umefika .., ninakufa, lakini namshukuru Mungu bado nipo hai hadi leo.

‘BETRI YA MOYO’

‘Rheumatic Heart Disease’ ni ugonjwa wa moyo ambao mtu huzaliwa nao, Ruth Wahu Ngwaro akiwa na umri wa miezi mitatu aligundulika ana tatizo hilo.

Anasema si safari nyepesi kuishi, akikabiliana nao, anakumbuka akiwa na umri wa miaka 15 ilikuwa nyakati ngumu zaidi.

“Familia yangu ni duni na baba yangu alihitaji kiasi cha Dola 200,000 kwa ajili ya kufanikisha upasuaji wangu.

“Nilishindwa kabisa kwenda shule, ilibidi ahangaike kuomba huku na kule hadi tukapata fedha hiyo nikapandikizwa ‘betri’ ya moyo [pacemaker] ambayo naishi nayo hadi leo,” anasema.

‘SI HALI INAYOTABIRIKA’

Arafa Said yeye amezaliwa na ugonjwa wa Siko Seli anasema si hali inayotabirika na kuzoeleka hata kidogo juu ya ugonjwa huo.

“Ni kama vile ‘there is a ghost in my body’ [kuna kitu kigeni, kikubwa na kibaya mno ninaishi nacho ndani ya mwili wangu], kinaendesha maisha yangu.

“Yaani unaniona hapa mbele yako sasa hivi ni mzima lakini punde naweza kuugua na nikalazimika kulazwa wodini kwa matibabu,”.

Ni raia wa Tanzania anasimulia, “Ni hali ambayo nyakati nyingine hutusababishia changamoto lukuki tunapata ‘complications’ [madhara yatokanayo na ugonjwa huu].

“Yaani [complication] inaweza kukushambulia popote pale ikaathiri figo zako na kila kitu,” anasema.

‘MZIGO MZITO’

Ni wachache kati ya wengi wanaopambana na NCD’s Afrika kila siku ya maisha yao, walipata nafasi ya kupaza sauti zao mbele ya dunia.

Tanzania ilichaguliwa na WHO Kanda ya Afrika [AFRO-WHO] kuandaa mkutano huo mkubwa wa kwanza wa aina yake ICPPA, washiriki zaidi ya 300 kutoka mataifa zaidi ya 15 walijadili pamoja.

PEN-Plus huu ni mpango mahususi unaangazia zaidi magonjwa makuu matatu ya NCD’s yanayoathiri kundi kubwa la watoto wa Afrika [Kisukari aina ya kwanza, Siko Seli na Magonjwa ya Moyo].

NCD’s, takwimu za WHO zinaeleza huchangia zaidi ya 70% ya vifo vinavyotokea kila mwaka Barani Afrika na wengi wanaofariki ni watoto na vijana.

Nchi zilizopo Kusini mwa Jangwa la Sahara ndiko haswa vifo vingi hurekodiwa, ikiwamo Tanzania, Taifa hilo la Afrika Mashariki kila mwaka Wizara ya Afya hurekodi zaidi ya vifo 40% kwa NCD’s.

“Ni vigumu mno kuishi na T1D nchini Uganda pia, nimewahi kukutana na mwanamke mwenye Kisukari na wanawe wawili pia waligundulika wana T1D,” anasema Edith.

Anaongeza “Mama yule alifariki, wanawe walibaki wakihangaika wenyewe siku moja mmoja wao alinitafuta na kuniambia [“Dada tunakosa hata hela ya kwenda hospitali kupata dawa,”].

HALI NGUMU

“Aliniambia nisichoke kuwasaidia kwani wananihitaji mno, ilikuwa siku ngumu kwangu, napenda mjue ilivyo vigumu kuishi na NCD’s.

“Ikiwa hutapata tiba stahiki unakuwa kwenye hatari ya kupata magonjwa mengine ya NCD’s hata 3 au 4.

“Ukweli tunahitaji kuifikia jamii na kuielimisha kuhusu magonjwa haya ili wayaepuke na kuwasaidia pia wale wanaohitaji kupata huduma,” anasema.

Ruth anasimulia alipata wakati mgumu pia alipokutana na mgonjwa mmoja wa moyo aliyeshindwa kumudu kununua dawa zake, ilibidi amsaidie kununua siku hiyo.

“Nilimkuta wodini hakuwa na uwezo nilitoa za kwangu, ni lazima nchi za Afrika ziimarishe mifumo yake ya upatikanaji wa huduma lakini pia kupunguza gharama za matibabu,” anasisitiza.

‘PEN-Plus VOICES’

Arafa anasema kwa upande wa Tanzania inafanya vema katika kuukabili ugonjwa wa Siko Seli hata kuimarisha huduma za tiba za kibingwa na bobezi, hatua ambayo ni ya kupongeza.

Anasema pamoja na hayo bado kuna uhitaji mkubwa wa uelimishaji huku akibainisha kwa sababu ya uelewa duni kumekuwa na muendelezo wa vitendo vya unyanyapaa kwa wagonjwa ndani ya jamii.

“Sisi tunaishi na magonjwa haya, tunafahamu lugha ya kuzungumza na jamii zetu na wakatuelewa kwa urahisi zaidi,” anasema.

Hoja ambayo ‘inaungwa mkono’ na Echodu anasisitiza “Ni muhimu tafiti zikaendelea kufanyika pia ili kuboresha huduma lakini ni muhimu pia nchi za Afrika zikatuhusisha katika upelekaji elimu.

“Ninyi [wataalamu/watafiti] mnaijua sayansi [ya NCD’s] ila sisi tunaishi na magonjwa haya, tunaijua safari hii, tushirikisheni … tukasaidie jamii,” anatoa rai.

Ruth anaongeza “Tunahitaji tuwe sehemu ya kuleta mabadiliko na matokeo chanya kwa Bara la Afrika katika ‘vita’ dhidi ya NCD’s, tushirikishwe lakini si tu kuachwa pembeni na kuletewa kila kitu.

MWANZO IMARA

Umoja wa Mataifa [UN] kupitia Malengo Endelevu umedhamiria kutokomeza NCD’s ifikapo 2030.

Mtafiti mbobezi wa magonjwa ya damu hasa Siko Seli Barani Afrika Profesa Julie Makani anasema mkutano wa ICPPA umekuwa mwanzo iimara na madhubuti kwa Bara la Afrika.

“PEN-Plus ni mkakati unaoendana na malengo ya WHO Kanda ya Afrika, inaiweka nchi za Afrika kwenye nafasi nzuri zaidi katika kupambana na NCD’s,” anasisitiza.

Anasema mpango huo wa PEN-Plus umeweka msisitizo kwa nchi za Afrka kuanzisha kliniki za NCD’s hadi katika ngazi ya huduma za afya za msingi.

Anasema nchi za Afrika zimekuwa zikifanya tafiti nyingi kuangazia magonjwa hayo ili kusaidia kuboresha huduma za uchunguzi na tiba kwa raia wake.

“Kupitia mkutano huo imesisitizwa umuhimu wa wataalamu na watafiti kuzidi kushirikiana katika kukabili magonjwa hayo.

Anatolea mfano Tanzania inaweza kushirikiana na Msumbiji katika kutoa huduma, Kenya na Uganda na si wataalamu wa nchi moja ‘kujifungia’ milango peke yake.

“Kusema sisi [nchi fulani] tutakaa tu kupambana na Saratani au Kisukari, uwezekano wa kufikia malengo ni mdogo,” anasisitiza na kuongeza,

“.., umeonesha pia ni muhimu kushirikiana na watu wenye haya magonjwa, washiriki mapambano haya.

“Kuhakikisha wanajipanga na wanakuwepo kwenye kongamano, mikutano, mijadala,” anasema na kuongeza,

 “Ni muhimu kuhakikisha wanashiriki tafiti, kushauri huduma zinakuwaje na hata kwenye kuongea na viongozi na jamii ili tuweze kwenda mbele zaidi.

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement