Gundi ya viatu ikiwa kwenye chupa
NA VERONICA ROMWALD – DAR ES SALAAM
MATUMIZI ya ugoro, petrol na gundi yametajwa kuwa mabaya
zaidi kulinganisha na dawa za kulevya huku ikielezwa kwamba hakuna dawa maalumu
ya kumtibu mwathirika.
Imeripotiwa baadhi ya watu waliokuwa wakitumia dawa za kulevya nchini wamelazimika kugeukia
vilevi hivyo ili kuiridhisha miili yao kutokana na kuadimika kwa dawa za
kulevya nchini.
Hali hiyo inatokana na vita iliyoanzishwa na Mkuu wa Mkoa wa
Dar es Salaam, Paul Makonda, vita ambayo ilikolevya moto na Rais Dk. John
Magufuli ambaye alimteua Kamishna wa kupambana na Dawa za Kulevya ili aendeleze
mapambano hayo nchi nzima.
Akizungumza na MTANZANIA jana Daktari Bingwa wa Magonjwa ya
Akili, Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Dk. Cassian Nyandindi (pichani) alisema matumizi
ya vilevi hivyo viitwavyo kitaalamu inhalants husababisha madhara makubwa kwa
binadamu.
“Vilevi hivi vimekuwa vikitumia kwa muda mrefu katika baadhi
ya mikoa, awali kundi ambalo lilionekana kutumia zaidi ni wale watoto wa
mitaani,” alisema.
Alisema hata hivyo wengi hawajui kwamba vina madhara makubwa kuliko
hata dawa za kulevya.
“Mtu anayetumia dawa za kulevya anaweza kusaidiwa kwa kupewa
methadone ili aachane nazo lakini hivi vilevi vya gundi na petrol hakuna tiba
kabisa ambayo mwathirika anaweza kupewa ili aachane navyo,” alisema.
Wengi hujidunga kwa njia ya sindano
Dk. Nyandindi alisema madhara ya matumizi ya vilevi hivyo yamegawanyika
katika makundi mawili ambayo ni madhara ya muda mrefu na mfupi.
“Madhara ya muda mfupi ni pamoja na kuchanganyikiwa, kutembea
kwa kuyumba-yumba, kuhisi kizunguzungu, kuzungumza kwa lafudhi ya mlevi na
maumivu ya kichwa,” alisema.
Aliongeza “Lakini muhusika anapopatwa na hali hiyo mwenyewe
anakuwa anasikia starehe na wapo ambao baadae huona maluweluwe, hupata kifafa, hukosa
hewa na hatimaye kuzimia au hata kufariki dunia.
Dk. Nyandindi alitaja madhara ya muda mrefu ni kutanuka mishipa
ya damu, kuongezeka mapigo ya moyo, kuharibika ini na figo, kupungukiwa au
kupoteza kabisa uwezo wa kufikiri.
“Madhara mengine yaliyopo katika kundi hili ni kupoteza uwezo
wa kuona (upofu), kuwa kiziwi na kuharibika kwa mfumo wa kutengeneza
chembechembe za damu kwenye mifupa mwilini,” alisema.
Alisema iwapo mjamzito atatumia vilevi hivyo, humuweka mtoto
wake kwenye hatari ya kuzaliwa na mwili mdogo.
“Mtoto anakuwa hakui vizuri kama inavyotakiwa na anakuwa na
mwili mdogo ambao haulingani kabisa na umri wake,” alisema.
Dk. Nyandindi alisema vilevi hivyo baadae humsababishia
mtumiaji utegemezi (addiction) na pale anapovikosa huhisi kichefuchefu, hutokwa
jasho jingi na kujikuna ovyo sehemu mbalimbali za mwili wake.
Alisema mwathirika wa vilevi hivyo hupata pia matatizo ya
kukosa usingizi, huwa na hasira za karibu na kwamba tabia yake huwa haitabiriki
kwani hubadilika badilika kila mara.
“Nimesema awali kwamba hakuna dawa kwa hiyo ili kumsaidia
mwathirika huwa tunalazimika kuzitibu tu zile ‘complications’ ambazo
hujitokeza. Hivyo tunamtibu kizunguzungu alichonacho, kifafa au maumivu ya
kichwa basi,” alisema.
Dk. Nyandindi alisema tangu vita ya dawa za kulevya itangazwe
na Makonda idadi ya waathirika wanaofika kwao kupata tiba imeongezeka.
Alisema awali walikuwa wakipokea waathirika wanne kwa siku,
idadi hiyo imeongezeka hadi kufikia waathirika kati ya 10 hadi 12.
Chapisha Maoni