NA VERONICA ROMWALD – DAR ES SALAAM
MIAKA ya nyuma ilikuwa ni nadra kusikia mtu amefariki dunia ghafla
hasa akiwa usingizi, wazee wetu waliishi maisha marefu kuliko ilivyo miaka ya
sasa.
Wazee hao waliishi maisha ya kiasili ambayo yaliwasaidia
kujiepusha kupata maradhi mengi. Leo hii maisha yamebadilika mno huku watu
tukipenda kuishi kisasa bila kujua tunajiumiza wenyewe miili yetu.
Siku hizi si ajabu tena kusikia mtu amefariki ghafla
usingizini, kifo cha namna hiyo huwa kinauma mno na kuliza wengi na kuacha
simanzi kubwa.
Mtindo mbovu wa maisha tulionao miaka ya sasa ndiyo ambao
unatajwa kuchangia kwa kiasi kikubwa ongezeko la magonjwa yasiyokuwa ya
kuambukiza.
Wengi wetu tunapenda kula vyakula visivyokuwa vya asili,
hatufanyi mazoezi, hatupimi afya mara kwa mara kujua mwenendo wake.
Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo wa Taasisi ya Tiba ya Moyo
ya Jakaya Kikwete, Pedro Pallangyo (anayezungumza na mgonjwa) anasema kutozingatia ulaji bora, kutokufanya
mazoezi na kutokupima afya ni hatari kwa afya zetu.
Wengi
hufa usingizini
Anasema vifo vingi vinavyotokea watu wakiwa usingizi sababu
yake kuu huwa ni kuziba kwa mishipa ya damu.
“Tatizo la kuziba mishipa ya damu tulizoea zamani lilikuwa
linazikabili zaidi nchi zilizoendelea pekee lakini sasa ni tatizo kubwa hadi katika
nchi zinazoendelea ikiwamo Tanzania,” anasema.
Anasema tatizo hilo lilikuwa nchi zilizoendelea kwa sababu
ndipo ambapo kulikuwa na sababu hatarishi zinazosababisha mishipa kuziba kuliko
nchi zinazoendelea ambapo hazikuwepo.
“Sababu hatarishi zinazotajwa hapa ndizo hizo, ulaji wa
vyakula vyenye mafuta mengi mno, kutokufanya mazoezi, unywaji wa pombe nyingi, na
kuvuta sigara.
“Nyingine ni uzito mkubwa kupindukia kulinganisha na urefu wa
mtu husika, magonjwa ya shinikizo la damu na sukari,” anasema.
Dk. Pallangyo anaongeza “Vitu vyote hivi vinapokuwa kwa mtu
na anapokuwa na vingi ndivyo anavyoongeza hatari ya kupata tatizo la kuziba kwa
mishipa ya damu.
Madaktari wa JKCI wakimfanyia upasuaji wa kuzibua moyo mmoja wa wagonjwa waliofika hospitalini hapo.
“Yaani unakuta mtu ni mvutaji wa sigara wakati huo huo ana
kisukari na shinikizo lake la damu lipo juu, mtu huyu uwezekano wa kupata
tatizo la kuziba kwa mishipa yake ya damu unaongezeka,” anasema.
Anasema visababishi vyote hivyo huashiria kuongezeka kwa kiwango
cha mafuta kwenye damu.
Anasema hata hivyo athari za kuwapo kwa kiwango cha mafuta kikiwa
kingi kwenye damu kwa muda mrefu huwa hakijitokezi mapema kwa watu wengi.
“Miaka ya nyuma wengi walianza kuona athari za mafuta kwenye
damu, walipofikisha umri wa kuanzia miaka 40 na kuendelea. Lakini leo hii
athari zinajitokeza zaidi kwa watu walio katika umri wa ujana, yaani chini ya
miaka hiyo,” anasema.
Anasisitiza sababu kuu ya tatizo hili ni mfumo mbovu wa
maisha hasa ulaji usiofaa.
“Jinsi mtu anavyozidi kuishi kwa mfumo mbovu, miaka yake
inavyozidi kusonga mbele ndivyo ambavyo mafuta yanavyozidi kuongezeka na
kutanda kwenye mishipa yake ya damu hasa ile inayopeleka damu kwenye moyo,”
anasema.
Mkurugenzi wa JKCI, Profesa Mohamed Janabi akifafanua jambo
Dk. Pallangyo anasema kadri mafuta yanavyotanda hupunguza
uwazi wa damu kupita au huziba kabisa na hivyo damu kushindwa kupita.
“Kwa kawaida mshipa wa damu hautakiwi kuwa na mafuta yeyote
lakini uwazi unapokuwa umezibwa kwa kiwango cha asilimia 50 kuendelea huyu mtu
lazima apate shida kwa sababu damu inakuwa inapita chini ya asilimia 50
inavyotakiwa,” anasema.
Anaongeza “Damu inapokuwa inapita chini ya kiwango cha
asilimia 50 au kuendelea ni lazima tumfanyie uchunguzi mgonjwa na kumfanyia
upasuaji wa kuzibua mshipa au mishipa iliyoziba.
Ushuhuda
wa mgonjwa
Faustine Mwandike ni miongoni mwa wagonjwa waliofanyiwa
uchunguzi na kugundulika kuwa na tatizo hilo ambapo tayari amefanyiwa upasuaji
wa kuzibuliwa mshipa wake wa damu uliokuwa umeziba.
Anasema kabla hajachukua hatua ya kwenda hospitalini alianza
kuhisi maumivu makali katika upande wa kushoto wa mwili wake (kwenye moyo).
“Maumivu hayo yalikuwa yakijirudia mara kwa mara, baadae
nilianza kuona mkono wangu wa kushoto unapoteza nguvu na maumivu yalikuwa
yakishuka wakati mwingine hadi kwenye miguu,” anasimulia.
Anasema ilifika mahali akawa anashindwa kumudu kuendesha vema
gari lake kwani maumivu hayo yalikuwa makali mno.
“Nikachukua hatua ya kwenda hospitalini, nikaanza kufanyiwa
vipimo mfululizo tangu Januari 11, mwaka huu, madaktari waliona kuna umuhimu wa
kuchunguza moyo
wangu hasa mishipa ya damu.
“Waligundua tatizo lilikuwa ni kuziba baadhi ya mishipa ya
damu, mmoja ulikuwa umeziba kwa kiwango cha asilimia 66 na mwingine ambao ni wa
kuingiza na kutoa damu kwenye moyo uliziba kwa asilimia 80,” anasema.
Anasema baada ya uchunguzi huo alirejea jijini Arusha kwenye
makazi yake na alirejea JKCI Januari 23 kwa ajili ya kufanyiwa upasuaji.
“Kulikuwa na kambi ya upasuaji, Januari 25, nilifanyiwa
upasuaji na mishipa hiyo ikazibuliwa, namshukuru Mungu sasa ni mzima,” anasema.
Sababu
“Ni mfumo mbovu wa maisha niliokuwa nikiishi na nadhani kama
nisingewahi kufika hospitalini basi hali yangu ingekuwa mbaya zaidi kwani
mishipa mingi ingeziba, sasa nafuata ushauri wa madaktari kuzingatia mtindo
bora wa maisha,” anasema.
Anashauri “JKCI inatoa matibabu kwa kiwango cha juu sana, ni
vema pia kami za namna hii ziwe zinazunguka nchi nzima angalau katika hospitali
za serikali ili wananchi wengi wasaidiwe.
Dalili
za tatizo
Dk. Pallangyo anataja dalili ya kwanza ni mtu kulalamika,
kuhisi maumivu ya kifua upande wa moyo mara
kwa mara hata akifanya shughuli nyepesi.
“Kawaida mtu akifanya shughuli yeyote mahitaji ya damu
yanakuwa makubwa, sasa wakati mahitaji ya damu yanaongezeka, damu haiwezi
kupita kwa sababu ule uwazi wake umeshapunguzwa kutokana na hayo mafuta,”
anasema.
Anasema baadae mtu hupata mshtuko wa moyo na hatimaye
kufariki ghafla.
“Dalili hizi huwa ni muendelezo, huanza kupata maumivu ya
kifua, mshituko hatimaye kufariki ghafla, hali hii hutokea pale ambapo mshipa
unakuwa umeziba kwa asilimia 100, damu hushindwa kabisa kwenda kwenye moyo na katika
sehemu zingine za mwili. Mshipa unapoziba damu na hewa ya oxigeni huwa zinashindwa
kupita,” anasema.
Wengi
wanaugua
Daktari huyo anasema kila siku watu watatu hadi saba hufika
katika taasisi hiyo na kufanyiwa uchunguzi na wanaokutwa na tatizo hufanyiwa
upasuaji wa kuzibuliwa.
“Idadi hii kwa wiki ni sawa na watu 35 na kwa mwezi ni sawa
na watu wapatao 140. Kwa mwaka jana pekee tuliwafanyia uchunguzi watu wapatao 400
katika mtambo wetu wa ‘cath lab’ kati yao asilimia 45 waligundulika kuwa na
tatizo,” anasema.
Anaongeza “Mishipa ilikuwa imeziba kwa kiwango ambacho
walihitaji kuzibuliwa au kuwekewa huo mrija (stand) kuizibua.
Anasema hata hivyo si wote ambao hufanyiwa upasuaji bali wale
ambao mishipa yao imeziba kwa kiwango cha asilimia 50 na kuendelea.
“Wale ambao huwa imeziba chini ya kiwango hicho huwa tunawapa
dawa za kutumia,” anasema.
Ushauri.
Anasema kwa kuwa tabia hatarishi zinazosababisha tatizo hili zinaepukika
watu wabadili mtindo wa maisha.
“Matibabu yake ni gharama kubwa, wanaomudu ni wale wenye
bima, kipimo na upasuaji hufikia hadi shilingi milioni nne, wengi wasiokuwa na
bima hushindwa kumudu, ni vema wakakate sasa,” anashauri.
Makala haya kwa mara ya kwanza yamechapishwa leo katika gazeti la MTANZANIA
Chapisha Maoni