Recent Post


 


moja

Responsive Advertisement
Mwananchi akipita pembezoni mwa rundo la takataka, uchafu ni chanzo cha magonjwa mengi ikiwamo kipindupindu (picha na mtandao)

Na Veronica Romwald, Aliyekuwa Dodoma

UCHAFU wa mazingira ni chanzo kikuu cha magonjwa mengi ya kuambukiza hasa ya kuhara, kila mwaka watu bilioni 1.7 huugua magonjwa ya kuhara duniani.

Takwimu hiyo ni kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO) ambalo linaeleza watu milioni 1.8 hufariki dunia kila mwaka kutokana na magonjwa hayo.

Idadi hiyo ni sawa na wastani wa vifo vinne kila dakika, kwamba hali hiyo huchangiwa zaidi na  ukosefu wa vyoo bora.

Shirika hilo linaeleza watu bilioni 2.3 sawa na theluthi ya watu wote duniani hawatumii vyoo bora na watu milioni 892 hawana kabisa vyoo bora.

Kwa mujibu wa Shirika hilo asilimia 70 ya wakazi waishio katika Bara la Afrika hasa Kusini mwa Jangwa la Sahara, Tanzania ikiwamo hawana kabisa vyoo bora.

Takwimu zinaeleza asilimia 40.5 ya kaya zote Tanzania ndizo zenye vyoo bora huku Kaya 600,000 zenyewe hazina vyoo bora.

Aidha, kila mwaka watu 30,000 huugua magonjwa ya kuhara nchini hiyo ikiwa ni sawa na asilimia 83 ya wagonjwa wote wanaolazwa kila siku hospitalini.
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu na Makamu wa Rais Samia Suluhu Hasaan wakipiga makofi kushangilia baada ya uzinduzi wa awamu ya pili ya Kampeni ya Taifa ya Usafi wa Mazingira hivi karibuni mjini Dodoma

Ni idadi kubwa

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu anasema katika kila wagonjwa 100 wanaofika katika vitengo vya wagonjwa wa nje hospitalini (OPD) kwa siku 60 huwa ni wale wanaougua magonjwa yatokanayo na hali ya uchafu.

“Ni wengi lakini tunaweza kukabili jambo hili kwa kuhamasisha wananchi kubadili mtizamo waliona nao juu ya ujenzi, matumizi ya vyoo bora na kuzingatia kunawa mikono baada ya kutoka chooni,” anasema.

Anaongeza “Nasema hivi kwa sababu, ingawa Rais John Magufuli ametuongezea bajeti ya dawa lakini ikiwa hatutaweza kukabili magonjwa haya itakuwa ni sawa na bure.

“Uchambuzi wa Benki ya Dunia (WB) inatueleza kila mwaka tunatumia zaidi ya Sh bilioni 400 kutokana na hali ya uchafu ni fedha nyingi ambazo tutaweza kuziokoa ikiwa tutafanikiwa kuhamasisha wananchi katika hili,” anasema.

Choo bora ni kipi?

Anasema katika mazingira ya Tanzania ni kile ambacho kimejengwa na kusakafiwa vema kuwezesha maji kupita kwa wepesi huku shimo linalohifadhi kinyesi likiwa limejengwa kwa nje na kikiwa kimeezekwa.

“Watanzania wasidhani ni kile minachohitaji kuwekewa masinki, tairizi… hapana, na si kwamba watanzania hawawezi kujenga vyoo bora tatizo ni ule mtizamo waliona juu ya matumizi ya vyoo, tumekusudia kuwafikishia elimu hii,” anabainisha.

Mwakilishi wa DFID

Mwakilishi Mkazi wa Shirika la DFID nchini Tanzania Elizabeth Arthur, anasema uchafu ni chanzo kikuu cha udumavu kwa watoto nchini Tanzania.

Anasema takwimu zinaonesha kila mwaka watoto 18.500 hufariki dunia sawa na watoto 50 kila siku kutokana na magonjwa ya kuhara

“Watoto wanaopata udumavu wapo katika hatari kubwa ya kuugua magonjwa mbalimbali kama vile nimonia, surua na mengineyo mengi,” anabainisha.
Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan akishiriki kufanya usafi mapema mwaka huu (picha na mtandao)

Mama Samia

Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan anasema takwimu hizo zinaonesha kwamba hali ya maisha ya binadamu si nzuri hivyo juhudi zinahitajika kufanyika kuboresha usafi wa mazingira.

“Zinaonesha pia watu wengi nchini hawana maeneo maalum ya kunawia mikono na asilimia 12 pekee ya watanzania hunawa mikono kwa maji safi na sabuni baada ya kutoka chooni,” anasema.

Akitolea mfano, anasema tangu mwaka 2015 ugonjwa wa kipindupindu ulipogundulika hadi kufikia Novemba 12, mwaka huu tayari watu 27,554 wameripotiwa kuugua.

“Katika kipindi hicho vimeripotiwa vifo 432, hii ni idadi kubwa na tungeweza kuepukana na hali hii ikiwa tungekuwa na mazingira yaliyo safi, hivyo ni lazima tuchukue hatua,” anasema.

Hatua zachukuliwa

Waziri Ummy anasema ili kukabili hali hiyo waliona umuhimu wa kuendeleza kampeni ya ‘Mtu ni Afya’ iliyoanzishwa na kutekelezwa kati ya mwaka 1973 hadi 1978 na Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere.

“Kampeni hiyo ya ‘Mtu ni Afya’ ilituchagiza Wizara pamoja na wadau wa maendeleo kuandaa kampeni inayofanana na hiyo ili tuweze kupambana na changamoto za usafi zilizopo nchini.

Anasema mwaka 2012 hadi 2016 walizindua awamu ya kwanza ya Kampeni ya Taifa ya Usafi wa Mazingira ambayo ililenga katika kuhamasisha ujenzi na matumizi ya vyoo bora.

Anasema awamu ya kwanza ya kampeni hiyo, ilihusisha Wilaya 196 nchini na kwamba mafanikio makubwa yamepatikana.

“Tumefanikiwa kuzifikia Kaya 516,444 ambazo zimejenga vyoo bora kati ya Kaya 600,000 tulizokuwa tumezikusudia hii ni sawa na asilimia 87 ya mafanikio,” anasema.

Anasema katika awamu hiyo ya kwanza ya mpango huo walilenga Kaya 800,000 zinatengeneza sehemu maalumu za kunawa mikono ambapo wamefanikiwa kuzifikia Kaya 701,788.

“Tulilenga kuboresha huduma za vyoo katika vituo vya kutolea huduma za afya, tumeweza kujenga vyoo katika vituo 441 awali tulilenga kufikia vituo 250 hivyo tumefanikiwa kwa kiwango cha asilimia 176 ya lengo letu,” anabainisha.

Anaongeza “Walilenga pia kuzifikia Kaya milioni moja ili kuzihamasisha kutibu maji ya kunywa kwa kutumia dawa ya fluoride au kwa kuyachemsha.

“Tumefanikiwa kuzifikia Kaya 684,477 ambazo sasa zimeanza kutibu na kuchemsha maji ya kunywa hii ni sawa na asilimia 93 ya lengo letu tulilokusudia,” anasema.
Njombe yatia fora

Waziri Ummy anasema Wilaya ya Njombe imefanya vizuri zaidi ambapo Kaya zote 240200 zimejenga vyoo bora.

Anasema shule za msingi 44 kati ya 52 zilizopo wilayani humo zina huduma ya vyoo bora kwa matumizi ya walimu, watumishi wasio walimu na wanafunzi (bila kusahau wenye ulemavu).

“Wametenga pia vyumba maalum kwa usafi wa wasichana waliopevuka, mafanikio haya yamepatikana katika awamu ya kwanza, tunaona wazi inawezekana kabisa kila Kaya nchini kuwa na choo bora.

Mkakati zaidi

Anaongeza “Ikiwa Njombe wameweza, tunajiuliza kwanini zingine zishindwe na ndiyo maana tunazindua awamu ya pili ya Mpango wa Taifa wa Usafi wa Mazingira.

Anasema awamu ya pili ya mpango huo utatekelezwa kwa miaka mitano kuanzia sasa hadi kufikia Juni, 2021.

“Utaenda sambamba na program ya maendeleo ya sekta ya maji wenye ‘component’ (vipengele) nne, ambapo ile ya nne inahusu masuala ya usafi wa mazingira,” anabainisha.

Malengo

Anasema wamekusudia kutekeleza maeneo manne katika awamu hii ikiwamo kuendelea kusimamia ujenzi na matumizi ya vyoo bora katika ngazi ya kaya.

“Tumekusudia kuzifikia kaya milioni 5.6, kufikia 2021, tunataka kuimarisha huduma za unawaji mikono kwa maji na sabuni kwa kaya hizo.

“Tunataka shule za msingi 3,555 ziwe na vyoo bora na sehemu za kunawia mikono pamoja na shule za sekondari 700, aidha, tumekusudia kujenga vyoo bora katika vituo 1,000 vya kutolea huduma za afya nchini” anasema.

Anasema wamekusudia pia kujenga vyoo bora 540 katika vituo vya mabasi ili kukabiliana na changamoto ya watu kujisaidia ‘porini’ wakati wa safari.

“Awamu ya pili itahusisha Wilaya zote 185 zilizopo nchini,” anabainisha Waziri Ummy

Kipimo kwa wakurugenzi

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Suleiman Jaffo anawataka wakurugenzi wa Wilaya zote nchini kuhakikisha wanatimiza wajibu wao kutekeleza Kampeni hiyo kwa vitendo.

“Katika awamu ya kwanza kuna mikoa ambayo haikufanya vizuri, katika awamu hii nataka kila mmoja atimize wajibu wake,” anatoa rai.

Anaongeza “Lengo letu tuwe na mazingira safi tukabili magonjwa yatokanayo na hali ya uchafu, ni muhimu pia wataalamu wa afya mtenge fedha za kutosha katika kusimamia jambo hili.

“Ningependa kuona kila mmoja anatimiza wajibu wake, kuna Wilaya zimefanya vizuri zimakabidhiwa zawadi zao mbalimbali, natamani ifike mahala kila tunayempima awe mshindi katika utekelezaji wa mpango huu,” anasema.

Mikopo ya vyoo

Mama Samia anazitaka taasisi za kifedha kuona umuhimu wa jambo hilo na kuanza kutoa mikopo maalumu ya ujenzi wa choo kwa wananchi.

“Waweke kipengele maalumu mwananchi akopeshwe fedha zitakazotumika kujenga choo bora, hatua hiyo itasaidia mno kukabiliana na changamoto hii.

“Tutaweza kukabiliana na magonjwa yatokanayo na hali ya uchafu wa mazingira, lazima tushirikiane katika hili ili tuweze kufikia malengo tuliyojiwekea,” anasisitiza.

Anaongeza “Kampeni hii imekuja wakati ambapo dunia inaendelea kutekeleza Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDG’s).

Anasema usafi wa mazingira ni mojawapo ya viashiria 196 vilivyomo kwenye malengo 17 ya SDG’s.

Anasema kati ya malengo hayo, lengo la tatu linahusu uboreshaji wa afya na ustawi wa jamii na lengo la sita linahusu upatikanaji wa huduma za maji safi na salama na usafi wa mazingira.

Anasema malengo hayo yanalipa Taifa msukumo wa kuhakikisha yanafikiwa kabla ya kufikia mwaka 2030.

“Ndani ya malengo haya mawili tunatakiwa kupunguza magonjwa ya kuambukiza kwa kuhakikisha tunaboresha usafi wa mazingira.

“Wachambuzi wa masuala ya mipango na maendeleo wameeleza dunia haiwezi kufikia malengo ya SDG’s ikiwa lengo la sita linalohusu huduma bora za maji na usafi wa mazingira halitafikiwa, maji ni uhai na ndiyo yanayoleta usafi wa mazingira.

Anaongeza “Kwa kuzingatia ukweli huo, serikali inatekeleza Program ya Maendeleo ya Maji ya mwaka 2006/2025 ambayo ndani yake kuna program ya usafi wa mazingira ambayo pia inasimamia kampeni ya Taifa ya Usafi wa Mazingira.

“Hivyo hatuna budi kuwekeza katika kusimamia usafi wa mazingira ili kuhakikisha tunafikia malengo ya Taifa tuliyojiwekea na haya ya Kimataifa yaliyowekwa,” anasema.

DFID wapo tayari

Mwakilishi Mkazi wa Shirika la DFID - Tanzania Elizabeth Arthur, anaipongeza serikali ya awamu ya tano kuona umuhimu wa kuendeleza mapambano dhidi ya uchafu wa mazingira ili kunusuru afya za wananchi wake.

“DFID tupo tayari kuendelea kushirikiana na serikali ya Tanzania kuiwezesha kwa kila namna ili iweze kufikia lengo iliyojiwekea kwamba kufikia mwaka 2025 kila Mtanzania awe na choo bora nyumbani kwake.

“Ni muhimu pia mashirika mengine ya kimataifa na wadau wa maendeleo wakaunga mkono jitihada hizi na wananchi kwa ujumla wakashiriki katika kampeni, usafi unahitaji nidhamu na utayari,” anashauri.

Makala haya kwa mara ya kwanza yametoka katika gazeti la MTANZANIA ambalo nalitumikia Desemba 14, 2017.

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement