Recent Post


 


moja

Responsive Advertisement
Picha na mtandao

Na Veronica Romwald, Dar es Salaam

KATI ya Novemba 25 hadi Desemba mosi, 2017 Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) ilifanya upasuaji mkubwa wa moyo wa kihistoria nchini.

Madaktari Bingwa wa JKCI kwa kushirikiana na wenzao wa Taasisi ya Open Heart International kutoka nchini Austraria waliwafanyia upasuaji wagonjwa 16 wenye matatizo mbalimbali ya moyo.

Kati ya wagonjwa hao tisa walikuwa watoto na saba walikuwa watu wazima ambao walifanyiwa upasuaji wa kubadilisha milango ya moyo iliyokuwa imeharibika na kuwekewa milango ya chuma.

Miongoni mwa watu wazima waliofanyiwa upasuaji wapo ambao walipandikizwa mishipa ya damu iliyovunwa kutoka miguuni na kwenda kuzibua ile iliyokuwa imeziba.

“Upasuaji huo kitaalamu unaitwa bi-pass surgery, hii si mara ya kwanza kwa taasisi yetu kufanya kwani tayari wagonjwa wapatao 30 wamefanyiwa kwa mwaka huu pekee,” anasema Mkurugenzi Mtendaji wa JKCI, Profesa Mohamed Janabi.
Profesa Janabi (pichani) Anasema kati ya wagonjwa hao 16 waliofanyiwa upasuaji katika kambi hiyo ya matibabu, tisa walikuwa ni watoto.

“Walikuwa na umri wa kuanzia miezi minne wakiwa na uzito wa kuanzia kilo nne hadi 12, kati ya watoto hao, mmoja (jina linahifadhiwa) alikuwa amezaliwa akiwa na moyo upande wa kulia,” anabainisha.

Ipoje?

Kibaiolojia moyo wa binadamu upo upande wa kushoto hata hivyo, Profesa Janabi anasema hutokea mara chache mtoto kuzaliwa moyo ukiwa upande wa kulia.

Chanzo ni nini?

Anasema bado haijajulikana wazi nini hasa husababisha mtoto kuzaliwa moyo wake ukiwa katika upande wa kulia.

“Duniani tafiti zinaonesha kati ya watoto 2000 wanaozaliwa basi mmoja huwa katika uwezekano wa kuzaliwa moyo wake ukiwa upande wa kulia,” anasema.

Anasema hata hivyo hakuna madhara yoyote yanayoweza kumpata mtoto ambaye moyo wake umeumbwa ukiwa upande wa kulia.

“Anaweza kuishi vema kabisa kama binadamu wengine ambao wameumbwa wakiwa na moyo katika upande wa kushoto,” anabainisha.

Kwanini walimpasua?

Profesa Janabi anasema walilazimika kumfanyia upasuaji mtoto huyo kwani alikuwa na matatizo makubwa mawili ya moyo.

“Moyo kuumbwa upande wa kulia haikuwa tatizo kubwa, isipokuwa tulibaini mishipa yake ya damu ilikuwa haifanyi kazi inavyopaswa.

“Katika moyo kuna mishipa inayoingia upande wa kulia ambayo kazi yake kuu ni kubeba damu chafu yenye hewa ya Kabonidaioksaidi na kuna inayoingia upande wa kushoto yenyewe hubeba damu safi yenye oksijeni,” anabainisha.

Anaongeza “Huyu mishipa yake ilikuwa inachanganya damu safi na chafu kwa pamoja jambo ambalo lilikuwa ni hatari kwa maisha yake.
Jengo la JKCI

Kivipi?

Anafafanua “Ni kama vile uchukue maji safi na taka halafu uyachanganye kwa pamoja kisha unywe, kamwe mwili hauwezi kuhimili mchanganyiko huo.

“Sasa yeye badala ya damu chafu kupita katika upande unaostahili ili ikasafishwe huchanganyika pamoja na damu safi iliyokwisha safishwa kisha iende mwilini kutumika, ni tatizo,” anasema.

Anasema pamoja na tatizo hilo, tatizo jingine lilikuwa kwamba mapigo yake ya moyo yalikuwa chini mno kutokana na kiwango kidogo cha umeme kwenye moyo wake.

“Kutokana na hali hiyo, ilibidi tumpandikize betri ndani ya moyo wake, hii ni oparesheni ya tatu kwa watoto na sasa mapigo yake yanakwenda vema,” anasema.

Anasema ilichukua takriban saa tisa kumfanyia na kukamilisha upasuaji huo.

“Kwa sababu kwa case kubwa namna hili hutulazimu ‘kuusimamisha’ moyo wake kwa saa kadhaa,” anabainisha.

Kisa cha kuwa bluu

Anasema ni kutokana na mchanganyiko huo wa damu safi na chafu ndipo hupelekea mtoto kugeuka kuwa na rangi ya bluu.

“Kitendo cha kugeuka kuwa na rangi ya bluu maana yake ni kwamba kile kiwango cha oksjeni kinachohitajika mwilini huwa hakitoshelezi,” anabainisha.

Dalili zake

Anasema dalili za awali kwa mtoto aliyezaliwa na tatizo la moyo ambazo mzazi anaweza kuziona ni pamoja na kushindwa kunyonya vizuri.

“Hii huwa zaidi kwa wale ambao wapo katika umri wa kunyonya lakini kwa wale ambao wapo katika umri wa kwenda shule wengi huchoka mara kwa mara,” anabainisha.
Makuzi yake

Anasema yataendeelea vizuri baada ya upasuaji huo na kwamba ataishi na kulelewa kama ilivyo kwa watoto wengine wasio na tatizo.

“Kila mshipa wa damu sasa unafanya kazi yake kama inavyotakiwa na mfumo wa umeme upo sawa sawa baada ya kumpandikiza betri hiyo,” anasema.

Anaongeza “Lakini kama asingetibiwa mapema basi kidaktari naweza kusema wazi kwamba asingefika na kusherehekea sikukuu yake ya kuzaliwa ya mwaka mmoja.

“Ila kwa kuwa tumewahi kumfanyia upasuaji tunaamini Mungu akimjalia basi atasherehekea sikukuu yake ya mwaka wa kwanza na kuendelea,” anasema.

Masharti

Anasema mtoto huyo ataishi na kula kila kitu isipokuwa amepewa masharti kadhaa.

“Tumempatia kadi maalumu ya utambuzi, hatatakiwa kupita kwenye maeneo ambayo yana sumaku kubwa kama vile uwanja wa ndege kwa sababu ile nguvu inaweza kukiwasha na kupelekea mapigo ya moyo kubadilika na kwenda kasi,” anasema.

Ushirikiano zaidi

Mkufunzi wa Wagonjwa Mahututi na daktari bingwa wa magonjwa ya moyo wa OHI, Russel Lee anasema wataendelea kushirikiana kwa ukaribu na JKIC katika kutoa matibabu.

“Kila ninapokuja Tanzania naona JKCI inazidi kufanya matibabu kwa kiwango cha juu zaidi ya awali, hili ni jambo linalotia faraja kubwa, OHI tutaendelea kushirikiana nao pia kwa kuwapatia mafunzo wataalamu wake ili wazidi kufanya vizuri zaidi,” anasema.
Faida zake ni zipi?

Daktari Bingwa wa Upasuaji Magonjwa ya Moyo kwa Watoto wa JKCI, Godwin Sharau (Pichani) anasema faida kubwa wanayopata katika kambi hizo za matibabu ni kubadilisha ujuzi.

“Kuna baadhi ya magonjwa ya moyo ambayo ni magumu sana na JKCI tunahitaji kupanda hatua kwa hatua ili tuweze kuwa- manage watoto na watu wazima ambao wana matatizo haya.

“Hivyo tunataka twende sambamba na wenzetu katika teknolojia ya kutibu magonjwa ya moyo ili kufikia adhma ya serikali kupunguza idadi ya wagonjwa wanaoenda kutibiwa nje ya nchi,” anasema.

Anaongeza “Ndiyo maana tunahitaji kukutana mara kwa mara na wenzetu ambao wamefika mbali katika utoaji matibabu ya magonjwa ya moyo kusudi tupate ule ujuzi walionao.

Wito

Anawasihi wazazi wanapoona dalili hizo wawahi kuwapeleka watoto wao hospitalini kwa uchunguzi zaidi.

“Ukimpeleka hospitalini watabaini tatizo na kama anastahili kuletwa JKCI watampa rufaa kuja huku, kuendelea kukaa naye nyumbani kutahatarisha zaidi maisha yake na kupelekea kufariki dunia.

“Lakini akiletwa hospitalini tukamfanyia uchunguzi kama atahitaji upasuaji tutamfanyia na anakuwa na uwezekano mkubwa wa kuishi maisha marefu kuliko akiendelea kukaa nyumbani,” anasema.

Anaongeza “Katika mwaka huu pekee tumeweza kuwafanyia upasuaji watoto wapatao 300 wenye matatizo ya moyo, ukijumlisha na watu wazima idadi yao inazidi 600.

“Lakini katika mwaka huu pekee watoto waliopoteza maisha ni wanne tu, hivyo wasiogope kuja kuwafanyia uchunguzi na upasuaji watoto wao,” anawasihi.

Profesa Janabi anawahimiza pia wataalamu wa afya kuhakikisha wanawapa rufaa mapema kwenda JKCI watoto wanaowapokea wakiwa na dalili hizo.

“Wawalete kwetu mapema, wasikae nao na kujaribu ‘diagnosis’ mbalimbali kwamba labda ni malaria, uti wa mgongo, nimonia au magonjwa mengineyo,” anawahimiza.

Makala haya kwa mara ya kwanza yametoka kwenye gazeti la MTANZANIA ambalo nalitumikia Desemba 21, 2017

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement