Hii ni sehemu ya pili ya ripoti hii ambako katika sehemu ya kwanza wanawake walipata nafasi ya kueleza changamoto walizokatana nazo katika safari yao hii.
Hapa tunaendelea, karibu, Imeandaliwa na Veronica Romwald, aliyekuwa Morogoro
Hivi karibuni
tulishuhudia jinsi ambavyo ‘sekeseke’ hilo lilipamba moto kiasi cha baadhi ya
viongozi wa serikali kuonekana waziwazi wakiwachukulia hatua wauguzi na wakunga
waliodaiwa kutoa lugha zisizofaa kwa wagonjwa kwa kuwaweka rumande.
Hata hivyo, ililazimu
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kutoa tamko la
kuwataka viongozi wa serikali kuziachia mamlaka zinazosimamia maadili ya
kitaaluma kuwachukulia hatua watumishi hao kwa kufuata misingi ya sheria,
kanuni na taratibu zilizowekwa.
Pamoja na hayo,
inadaiwa watumishi wengi wa kike wa kada hizo ndiyo ‘vinara’ wa kutoa lugha
chafu kwa wajawazito tangu wanapohudhuria kliniki na hadi kipindi cha
kujifungua kuliko watumishi wa jinsia ya kiume.
Rais wa Chama cha
Wakunga Tanzania (TAMA). Feddy Mwanga anakiri kwamba wamekuwa wakipokea
malalamiko kutoka kwa jamii dhidi ya baadhi ya wakunga.
“Wapo wanaotuhumiwa
kutoa lugha zisizofaa na tunapopokea malalamiko tunafuatilia kwa ukaribu na
ambaye anakutwa na hatia tunamchukulia hatua kwa mujibu wa sheria,”
anabainisha.
Utafiti wafichua mambo
Maurice Hiza ni Ofisa katika Idara ya Huduma na Ukunga wa Wizara ya Afya, Maendeleo
ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto anasema waliamua kufanya uchunguzi wa kina
juu ya malalamiko hayo.
“Tulipokea
malalamiko mengi mno na tukaamua kufanya uchunguzi wetu wa kina ili kujua je ni
kweli au watu walikuwa wakieneza tu uvumi, baada ya uchunguzi wetu tulibaini ni
kweli wapo baadhi ya wakunga ambao hutamka lugha zisizofaa wanapokuwa
wakihudumia wateja,” anasema.
Katibu Mkuu wa
Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk. Mpoki
Ulisubsya anasema wizara ina utaratibu maalum wa kushughulikia kero
zinazowapata wafanyakazi wake.
Anasema taratibu
hizo zinaendana na sheria za nchi na zimewekwa mahusus kuzishughulikia kero zozote
ziwe zimesababishwa na mazingira ya kazi, wafanyakazi wenzao au watu wanaokuja
kupata huduma.
“Mara nyingi
tunaweza kuwa tunashughulika na watu wanaotoa huduma baada ya wafanyakazi kuja
kutoa taarifa kwamba wamefanyiwa jambo fulani au mtu ameona mfanyakazi
amefanyiwa jambo akatupa taarifa na sisi tunafuata utaratibu.
“Tunauliza
mfanyakazi amefanyiwa jambo gani na lazima tumjue aliyefanya jambo husika,
hatua hii imetusaidia mno kutatua kero mbalimbali za wafanyakazi , vile vile
mahali pa kazi ni salama kwa sababu ya utaratibu tuliojiwekea wa ndugu, namna
ya kuingia katika maeneo ya kazi hata wagonjwa wenyewe.
“kwa hiyo
hatutegemei wakunga wanaweza kudharauliwa, kutukanwa na ndugu kwa mazingira ya
kawaida ya kazi kwa sababu anaposhughulika na wajawazitokuna utaratibu wao
ambao wanausimamia,” anasema.
Dk. Ulisubisya
anasema hata hivyo pamekuwa na malalamiko na mengi huyapokea kutoka kwa ndugu
wa wagonjwa kulalamikia huduma zinazotolewa hasa kuhusu lugha.
“Hilo tumekuwa
tukilishughulikia mno kwa kuhakikisha tunakuwa na huduma rafiki katika maeneo
yote,” anabainisha.
Wakunga wafunguka
Wakati jamii ikilalamika na kuwatuhumu baadhi ya
wakunga kutotimiza wajibu wao kwa mujibu wa misingi ya taaluma yao.
Wakunga nao wamefunguka na kutoa yale yaliyo moyoni
mwao ambapo hapa wanaeleza changamoto mbalimbali wanazokumbana nazo wakati wa
kutekeleza majukumu yao ya kila siku.
Akizungumza na MTANZANIA
Mariam Japhet, Mkunga wa Hospitali ya Ulanga mkoani Morogoro anasema
amefanya kazi hiyo tangu mwaka 1990 na kwamba amekutana na mikasa ya namna
nyingi.
“Nakumbuka kuna siku nilipokea mjamzito ambaye
mapigo yake ya moyo nay a mtoto yalionekana kushuka mno, nilimjulisha daktari alipokuwa
akimfanyia vipimo zaidi yule mama alibaini mtoto alikuwa tayari amefariki
dunia.
“Alipofanyiwa upasuaji wa kumtoa mtoto tumboni,
alikutwa na tatizo la kichwa kikubwa, basi ndugu aliyekuwa amekuja na mgonjwa
alijulishwa lakini alipokuja mumewe hakuwasilisha vizuri maelezo yale
aliyopatiwa,” anasema.
Anasema hali hiyo ilisababisha baba wa mtoto husika
na baadhi ya ndugu kuanza kulalamika kuwa mtoto wao alikuwa amefariki kutokana
na uzembe.
“Ikabidi tutumie ujasiri kumuita baba husika na kumuonesha
ule mwili wa mtoto wake alipoangalia na kuona alikuwa na tatizo la kichwa
kikubwa aliamini hakukuwa na uzembe uliokuwa umefanyika,” anasema.
Muuguzi mkunga mwandamizi Agnes Mtawa ambaye hivi
karibuni ameteuliwa kuwa Msajili wa Baraza la Wakunga Tanzania anasema katika
miaka zaidi ya 20 aliyohudumu katika fani hiyo amepitia mambo mengi.
“Katika hospitali niliyokuwa nasimamia, kuna siku
aliletwa mjamzito ambaye alifikishwa akiwa amechoka mno na bahati mbaya mtoto
alifariki tukiwa zamu ya usiku tutachukua kitenge chake tukastiri mtoto.
“Ndugu walipokuja asubuhi wakabaini kitenge
hakikuwepo wakadai kwamba kilikuwa kimeibiwa na wakunga tuliokuwa usiku ule,
kwa haraka haraka tulikubaliana tulipe.
“Lakini tulifanya jitihada kuangalia kilienda wapi,
tukakagua na kubaini kwamba tulimfungia mtoto baada ya kufariki dunia, ndugu
walikuwa tayari wamekasirika hawakuwa na uchungu tena na kifo cha mtoto wao
walikuwa na uchungu na kile kitenge.
“Kwa kawaida tulikubaliana kwamba mama akiletwa
pale hospitalini (Muhimbili) kila kitu chake alichokuja nacho lazima kiandikwe
anapoingia na anapotoka, na hatua hiyo ndiyo ilitusaidia kujua ukweli kwamba
kitenge hakikupotea bali alifungiwa mtoto kumsitiri,” anasema.
Itaendelea... Usikose nakala ya gazeti la MTANZANIA ambalo nalitumikia.
Chapisha Maoni