Rais Pierre Nkurunziza
BUJUMBURA
Makundi hasimu ya wanajeshi yanakabiliana katikati ya mji mkuu wa Burundi- Bunjumbura, mahala ambapo tangazo lilitolewa jana Jumatano kuwa Rais Pierre Nkurunziza, amepinduliwa.
Makabiliano ya risasi yanaendelea kwa sasa, huku milipuko kadhaa ikisikika.
Kwa mujibu wa taarifa ya habari ya DW mchana huu, rais Nkurunzinza ametoa tamko fupi kupitia ukurasa wa twitter wa rais akiwataka wananchi wa Burundi kuwa watulivu.
Taarifa ya DW pia imearifu kuwa Mkuu wa majeshi nchini Burundi Meja Jenerali Prime Niyongabo ametangaza kuwa jaribio hilo limefeli.
Hata hivyo,Mkuu wa zamani wa idara ya upelelezi ya Burundi Meja Jenerali Godefroid Niyombare ambaye ndiye aliyeongoza mapinduzi hayo amesema kuwa hizo ni propaganda tu za baadhi ya wanajeshi watiifu kwa rais Nkurunzinza.
Niyombare amesema kuwa kama ni kweli mapinduzi yamefeli, basi rais Nkurunzinza arudi nchini leo,asiporudi leo basi hakuna haja ya kubishana juu ya uwepo wa mapinduzi hayo.
WAKATI huo huo,
Baraza la usalama la Umoja wa Mataifa linatarajiwa kufanya mkutano wa dharura hii leo kuijadili Burundi baada ya jenerali mwandamizi wa jeshi nchini humo kutangaza kumpindua Rais Pierre Nkurunzinza kutoka madarakani.
Ufaransa ndiyo imeitisha kikao hicho cha dharura ambacho kitafanyika hii leo punde tu baada ya wanachama wa baraza hilo la usalama la Umoja wa Mataifa kuijadili Iraq.
Hapo jana Meja Jenerali Godefroid Niyombare ambaye alikuwa mkuu wa shirika la ujasusi nchini Burundi, alitangaza kuwa utawala wa Rais Pierre Nkurunzinza umepinduliwa na jeshi kutoka madarakani kwa kukiuka matakwa ya raia.
Mara ya mwwisho alikuwa Tanzania
Wakati wa tangazo hilo la kupinduliwa kwa serikali, Nkurunzinza alikuwa Tanzania kuhudhuria mkutano wa viongozi wa jumuiya ya nchi za Afrika Mashariki uliotishwa na mwenyekiti wa jumuiya hiyo Rais wa Tanzania Jakaya Kikwete kuujadili mzozo huo wa Burundi.
Niyombare aliagiza viwanja vyote vya ndege na mipaka yote ya ardhini ya Burundi kufungwa.
Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki Moon ametoa wito wa dharura kwa pande zote nchini Burundi kuonyesha utulivu na kujizuia kufuatia jaribio la mapinduzi ya serikali dhidi ya Rais Nkurunzinza.
Msemaji wa katibu huyo mkuu wa Umoja wa Mataifa Stephanie Dujarric amesema Ban amesisitiza haja kwa viongozi wote wa Burundi kudumisha amani na uthabiti katika taifa ambalo limekumbwa na matukio ya ghasia mbaya katika kipindi cha nyuma.
Marekani imewataka waburundi kuweka silaha chini kufuatia ripoti za kupinduliwa kwa serikali ya Nkurunzinza na msemaji wa ikulu ya Rais wa Marekani Josh Ernest amesema nchi yake inafuatilia matukio yanavyojiri Burundi kwa makini na wasiwasi.
Marekani imesema bado inamtambua Nkurunzinza kuwa kiongozi rasmi wa Burundi lakini inamshinikiza kuheshimu katiba ya taifa hilo na mikataba ya amani ilyofikiwa mwaka 2000 kwa kutogombea muhula wa tatu.
Marekani inatambua utawala wa Nkurunzinza
Hatma ya Nkurunzinza haijulikani baada ya ofisi ya Rais hapo jana kutangza anarejea nyumbani kutoka mkutano wa viongozi wa Afrika Mashariki nchini Tanzania na alitarajiwa kulihutubia taifa.
Lakini ndege yake haikuweza kutua mjini Bujumbura baada ya viwanja vya ndege kufungwa. Afisa wa ngazi ya juu wa Uganda ambaye hakutaka kutambuliwa kwasababu haruhusiwa kuongea na vyombo vya habari amesema ndege iliyokuwa ikimbeba Nkurunzinza ilitua katika uwanja wa Entebbe nchini Uganda lakini hakutaka kuthibitisha iwapo yuko nchini humo au alirejea Tanzania.
Kiasi ya watu 20 wameuawa tangu tarehe 25 mwezi uliopita baada ya Nkurunzinza kutangaza kuwania muhula wa tatu madarakani kinyume na katiba ya taifa hilo ambayo inaruhusu mihula miwili tu ya miaka mitano kila mmoja akidai muhula wake wa kwanza alichaguliwa na bunge na wala sio wananchi. Zaidi ya waburundi 50,000 wametorokea nchi jirani kufuatia ghasia za kabla ya uchaguzi unaotarajiwa mwezi ujao.
Chapisha Maoni