Recent Post


 


moja

Responsive Advertisement


Wabunge wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) waliokuwa wakimuunga mkono Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, katika harakati za kusaka urais, wamechukua fomu za kuomba kuteuliwa kuwania ubunge kupitia chama hicho.

Kabla ya hapo, kulikuwa na uvumi kuwa wabunge hao hawatachukua fomu kutokana na kukatwa kwa Lowassa katika kinyang’anyiro cha urais.

Baadhi ya wabunge hao ambao wamechukua fomu hizo na kuzirejesha jana ni pamoja na Kangi Lugola (Mwibara), Andrew Chenge (Bariadi Mashariki), Philipo Mulugo (Songwe).

Tanga
Mkoani Tanga, wabunge watatu waliokuwa wakimuunga mkono Lowassa nao wamechukua na kurudisha fomu za kuomba kutetea majimbo yao.

Wabunge hao ni Stephen Ngonyani maarufu kama Majimarefu ambaye ni Mbunge wa Korogwe Vijijini, Beatrice Shelukindo (Kilindi) na Henry Shekifu wa Lushoto.

Mtandao huu umefuatilia mchakato wa uchukuaji na urudishaji fomu ndani ya CCM ambao ulihitimishwa jana saa 10:00 jioni na kubaini kuwa wabunge hao wameshachukua na kurudisha fomu za kutetea nafasi zao licha ya kuwapo kwenye ushindani mkali kutokana na idadi ya wagombea kuongezeka kwenye majimbo yao.

Katika majimbo yote 11 ya Mkoa wa Tanga, wabunge wote waliokuwapo katika awamu inayomalizika, wamejitosa tena na kuchukua fomu za kuwania nafasi hiyo.

Kwa sasa Mkoa wa Tanga una jumla ya majimbo 12 baada ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec) kuongeza jimbo moja la Handeni Vijijini.

Kilimanjaro
Vigogo watano wa CCM mkoani Kilimanjaro wakiwamo Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Anne Kilango-Malecela na Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Aggrey Mwanri, ni miongoni mwa mawaziri `waliokabwa koo' kwa kupata upinzani mkali ndani ya majimbo yao.

Wengine ni Waziri wa zamani wa Mifugo na Maendeleo ya Uvuvi, Dk. Mathayo David Mathayo, ambaye anakabiliwa na upinzani mkali baada ya makada wenzake 13 kuchukua fomu za kuomba kuteuliwa kugombea kiti hicho katika Jimbo la Same Mashariki.

Waliojitosa kutaka kumng’oa Dk. Mathayo David ni John Chaggama, Daniel Mkemi, Alfred Ngelula, David Mawa, Amon Shahidi, Gerald William, Katery Daniel, Yusuph Singo, Michael Mrindoko, Ahadi Kakore, Jordan Mmbaga na Mwalimu John Singo.

Anne Kilango naye anakabiliwa na upinzani baada ya makada wanane akiwamo Dk. Michael Kadeghe, Dk. Eliji Kibacha, Semi Kiondo, Abraham Shakuri, Nyangasu Werema, Daudi Mambo na Ombeni Mfariji kujitosa kuwania kiti cha ubunge wa jimbo hilo.

Kigogo mwingine aliyepata upinzani, ni Naibu Waziri wa Tamisemi, Mwanri, ambaye jimboni kwake, wazee wa kimila wa jamii ya wafugaji wa Kimasai wamelazimika kumwangukia, Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM (Nec), Meijo Laizer, kujitoa katika orodha ya makada watatu waliotangaza kuchukua fomu za kuomba kuteuliwa kugombea kiti hicho.

Kwa upande wa Jimbo Moshi Mjini ambalo kwa muda mrefu limekuwa ngome ya Chadema, makada 12 wamejitokeza kuwania kiti hicho.

Makada hao ni Patrick Boisafi, David Mosha, Buni Ramole, Priscus Tarimo, Edmund Utaraka, Shaniel Ngindu, Innocent Siriwa, Amani Ngowi, Omari Mwariko, Michael Mwita, Daudi Mrindoko na Khalifa Kiwango.

Katika Jimbo la Moshi Vijijini, Waziri wa zamani wa Viwanda na Biashara, Dk. Cyril Chami, amekutana na kikwazo baada makada watano kujitokeza kutaka kuteuliwa kugombea kiti hicho, huku Jimbo la Vunjo likiwa na watia nia wanane ambao wanakabana koo kutaka kuteuliwa kugombea kiti hicho.

Dodoma
Waziri wa Nishati na Madini ambaye ni Mbunge anayemaliza muda wake Jimbo la Kibakwe, George Simbachawene, Livingstone Lusinde (Mtera), Gregory Teu (Mpwapwa), Omari Badwel (Bahi) na Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano, Job Ndugai (Kongwa), ni miongoni mwa makada waliochukua fomu kutetea nafasi zao.

Bahi;
Mbunge wa sasa Badwel atapambana na Pascal Mwaja, Levison Chilewa, Donald Mejitii, Hebron Kipiko, Anthony Lyamunda, Salum Kanyika na Kondo Chaurembo.

Mpwapwa:
Mbunge wa sasa Teu, amepata wapinzani ambao ni George Lubeleje, June Fusi, Nyange Mtoro, Charles Kuziganika, Rehema Halahala, Emmanuel Mbeho na Gabriel Hango.

Kibakwe:
Simbachawene atapambana na Amani Bendera, Gabriel Mwikola, Sabas Chambas, Shahel Gayesh, Aclay Mnyang’ali na Solomoni Ngiliule.

Kongwa:
Ndugui amepata wapinzani wake ambao ni Samwel Chimanyni, Dk. Elieza Chilongani, Epafra Mtango, Pascal Mahinyila, Hussein Madeni, Simon Katunga na Joseph Palingo.

Mtera:
Lusinde atapambana na Richard Masimba, Samwel Malecela, Essan Mzuri, Lameck Lubote na Dk. Michael Msendekwa.

Chilonwa:
Waliojitokeza kutaka kuwania jimbo hilo ni Peter Nasoni Mlugu (Mwalimu wa Shule ya Msingi Chilonwa), Kusakula Amosi (mfanyabiashara jijini Dar es Salaam), Chibutii Masagasi, Charles Ulang, (Mwenyekiti wa CCM wa Wilaya ya Chamwino) na Vincent Chomol.
 
Wenslous Mazanda (Mwalimu wa Shule ya sekondari Mpunguzi), Joel Mwaka  (Mwenyekiti wa jumuiya ya wazazi, Wilaya ya Chamwino), Daniel Robina Logoha, Palolet  K. Mgema (Mkuu wa Wilaya ya Nachingwea), Deo Ndejembi, Godrick Ngoli, Anderson Kusenha Magolola na Kk. David Mapana.

Kyela
WANACHAMA 10 wamejitokeza kuchukua fomu ya kuwania ubunge Jimbo la Kyela mkoani Mbeya kupambana na Mbunge wa sasa, Dk. Harrison Mwakyembe.

Dk.Mwakyembe ambaye ni Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki alichukuliwa fomu na baadhi ya wananchi ambao walijichangisha fedha na kumkabidhi jana mjini Kyela ambaye alizirudisha Makao Makuu ya CCM Kyela.

Wengine waliochukua fomu na kurejesha katika jimbo hilo ni Gabriel Kipija, ambaye ni Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Kyela, John Mwaipopo, Profesa Leonard Mwaikambo, Gwakisa Mwandembwa, Vincent Mwamakingula, George Mwakalinga, Benjamin Richard, Asajile Mwambambale na Ackim Jackison.

Mbeya Vijijini
Waliochukua fomu Jimbo la Mbeya Vijijini ni Mbunge wa sasa, Luckison Mwanjale, Oran Njera, Godon Kalulunga (Mwandishi wa Habari),Japhet Mwanasenga, Anderson Kabenga, Walimu Sikwembe, Kassim Chakachaka.

Ileje
Aliko Kibona (Mbunge wa sasa) na Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Janneth Mbene.

Mbeya mjini
Nwaka Mwakisu, Aman Kajuna, Charles Mwakipesile

Vwawa
Mchungaji Tito Nduka, Japhet Hasunga na Mtella Mwampamba.

Maswa Magharibi
Waliochukua fomu ni Michael Bukwimba, Mashimba Ndaki, Benjamin Rungu, Aaron Mbojo (Mjumbe wa Nec) na Henry Mbichi.

Maswa Mashariki
 
Waliojitokeza kuwania ubunge Jimbo la Maswi Mashariki ni George Nangale (Mbunge wa Afrika Mashariki), Peter Bunyongole (Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Maswi), George Lugomela, Ali Ntegwa, Stanslaus Nyongo na Jonathan Mnyela

MEMBE NASTAAFU SIASA
 
Waziri wa Mambo ya Nje na  ushirikiano wa kimataifa, Bernard Membe, amesema hatogombea wadhifa wowote kwenye uchaguzi mkuu wa  mwaka huu na kwamba anapanga kujishughulisha na masuala yake ya kibinafsi.

Membe ambaye alikuwa akitafuta tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ili kuwania urais mwezi Oktoba lakini akashindwa kufikia lengo hilo, amesema kuwa, hatotafuta nafasi ya ubunge katika jimbo lake la Mtama.

Hata hivyo amesema ataendelea kukiunga mkono chama chake cha CCM na atampigia debe mgombea urais aliyeteuliwa na chama hicho, Bw. John Magufuli.

Awali kulikuwa na tetesi kwamba Membe angegombea ubunge baada ya kukosa nafasi ya kuwania urais kwa tiketi ya CCM.

Huku hayo yakijiri, chama cha Mapinduzi  (CCM) kinaendelea kupata pigo baada ya baadhi ya wabunge wake kutangaza kuwa hawatogombea tena nafasi zao kupitia chama hicho kwenye uchaguzi mkuu ujao.

Tayari madiwani 20 wa CCM katika jimbo la Monduli wametangaza kuhamia Chadema na kumtaka mbunge wao, Edward Lowassa kufuata mkondo huo.

PINDA SIGOMBEI TENA 
 

Waziri mkuu Mizengo Pinda amekataa ombi la wananchi wa  jimbo lake la uchaguzi la Katavi la kumtaka agombee tena ubunge katika jimbo hilo ili kuendeleza mipango mbalimbali ya maendeleo aliyoianzisha. 
 
Akizungumza baada ya Ibada ya Jumapili katika kigango cha Kanisa Katoliki cha Kibaoni wilayani Mlele (Jumapili, Julai 19, 2015), Waziri Mkuu Pinda amesema anamshukuru Mungu kwa nafasi aliyopewa ya kulitumikia Taifa akiwa Waziri Mkuu kwa miaka minane na anaamini wakati umefika wa yeye kuwaachia wengine nafasi ya ubunge wa jimbo la Katavi.

Amesema yeye ataendelea kuwa karibu na wananchi wa Katavi wakati wote  na kwa vile atakuwa na muda wa kutosha atashiriki kikamilifu katika mikakati mbalimbali ya kuwaletea maendeleo wananchi ili waweze kujikwamua kutoka kwenye umaskini. 
 
Mheshimiwa Pinda aliwaasa wananchi wa jimbo la Katavi wawe makini katika kuchagua mbunge na madiwani na kamwe watoa rushwa na wabadhirifu wasipewe nafasi katika uchaguzi ujao. 
 
Akimshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu, Paroko wa Parokia ya Usevya wilayani Mlele, Padri Aloyce Nchimbi aliwaasa wananchi wa Wilaya ya Mlele kumuenzi Mheshimiwa Waziri Mkuu, Mizengo Pinda hata atakapokuwa amestaafu kwani bado watahitaji busara na uzoefu wake katika kujiletea maendeleo. 
 
Waziri Mkuu yuko kijijini kwake Kibaoni, wilayani Mlele kwa ajili ya mapumziko mafupi. 
  
MWINYI, HAIKUWA RAHISI KUMPATA MAGUFULI.

 
Rais mstaafu wa Awamu ya Pili, Alhaj Ali Hassan Mwinyi amesema kuwa shughuli ya kupata mgombea urais kwa tiketi ya CCM haikuwa rahisi na akashukuru kwamba imemalizika kwa amani.
 
Mchakato huo ulihitimishwa Julai 12 mjini Dodoma wakati Mkutano Mkuu wa CCM ulipopitisha jina la Dk John Magufuli kugombea nafasi ya kuongoza Serikali ya Awamu ya Tano baada ya Rais Jakaya Kikwete kumaliza muda wake mwishoni mwa mwaka.
 
Jumla ya makada 38 walijitokeza kuwania nafasi hiyo, na majina matano ndiyo yaliyopitishwa kwenda Halmashauri Kuu na baadaye matatu kwenda Mkutano Mkuu.
 
Mchakato wa urais ndani ya CCM ambao kwa kawaida hutawaliwa na msuguano kabla ya kumalizika kwa maridhiano, safari hii ulienda mbali zaidi baada ya wajumbe watatu wa Kamati Kuu kupinga nje ya kikao uamuzi wa chombo hicho na baadaye wajumbe wa Halmashauri Kuu kumwimbia mwenyekiti wao, Jakaya Kikwete wimbo wa kuonyesha wana imani na Edward Lowassa baada ya jina la mbunge huyo wa Monduli kuenguliwa na Kamati Kuu.
 
Jana, akitoa hotuba fupi baada ya kumalizika kwa sala ya Eid el Fitr kwenye viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar es Salaam, Mwinyi alizungumza kwa mara ya kwanza hadharani kuhusu mchakato huo, akidokeza hali ilivyokuwa.
 
“Haikuwa kazi rahisi kwenye mchakato huu wa kumtafuta mgombea mmoja atakaye peperusha bendera ya CCM,” alisema Mwinyi lakini akawahi kuipoza kauli hiyo kwa kuelezea amani ilivyotawala mwishoni.
 
“Kama ni jahazi basi sasa tunashukuru limefika pwani salama.”
 
“Uchaguzi huu ni kwa ajili ya kuwapata viongozi wetu, tunataka viongozi bora wa kutuletea maendeleo, mapatano na wenye mahaba na wananchi.”
 
Akizungumza hadharani kwa mara ya kwanza baada ya mchakato huo wa kumtafuta mgombea wa urais kukamilika mjini Dodoma, Mzee Mwinyi alimshukuru Mungu kwa mchakato huo kuisha salama.
 
“Haikuwa kazi rahisi kwenye mchakato huu wa kumtafuta mgombea mmoja atakaye peperusha bendera ya CCM, kama ni jahazi basi sasa tunashukuru limefika pwani salama.
 
“Sasa, ninawaomba Watanzania kuwa watulivu katika kipindi hiki cha uchaguzi wa nchi tunaoufanyika kila baada ya miaka mitano,“ alisema Rais Mwinyi ambaye alikuwa mmoja ya wajumbe wa Baraza la Ushauri waliofanya kazi ya kutuliza wajumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM hadi kuafikiana kuendelea na mchakato wa kumpata mgombea urais.
 
Aliwasisitizia Watanzania kuacha tabia ya kupenda mno na kuacha kubaguana, akisema hakuna aliye bora na kuwataka kuzidisha mapenzi miongoni mwao na kusherehekea vyema Sikukuu ya Eid el Fitr. 
 
“Hakuna jambo lenye maana kama hili la kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye kutufikisha salama siku kama hii ya leo (jana) ambayo tunasherekea Sikukuu ya Eid,” alisema Mwinyi.
 
Awali Sheikh wa Mkoa wa Dar es Salaam, Alhad Mussa Salum aliwasisitizia wananchi umuhimu wa kusherekea sikukuu hiyo katika hali ya amani na utulivu.
 
Pia, aliwashauri wazazi na walezi kuwapeleka watoto wao sehemu zenye maadili ili washerehekee kama ambavyo Mwenyezi Mungu anapenda.
 
“Leo (jana) ni siku ya furaha, naomba tusherekee maeneo salama pia Waislamu msisahau kufunga sita kwani ina malipo makubwa,” alisema Alhad Salum.
 
Mkoani Geita ambako ilifanyika sala ya kitaifa ya Eid, Makamu wa Rais, Dk Mohamed Gharib Bilal alihutubia Baraza la Eid na kusema kipindi hiki kinahitaji utulivu, kuelewa na kuheshimiana pamoja na kudumisha uhusiano ili Taifa lipate viongozi bora.
 
“Tuwe watulivu ili Tanzania ibaki kuwa nchi ya kukimbiliwa na isiwe nchi ya kukimbiwa... sisi tusiwe wakimbizi, tuwe watu wa kupendana, kuvumiliana na kuthaminiana. Tusifikie hatua ya kuchukiana, kuuana na kufanyiana ukatili,” alisema Dk Bilal.
 
Alisema amani inaweza kuvunjwa na mtu yoyote kwa namna yoyote ile, akaharibu mazuri na heshima ya Taifa na akawaomba wananchi na waumini wote wasifikie hatua hiyo akisema ndiyo wenye uwezo wa kuifanya nchi yao kuwa ya amani.
 
“Tuishi kwa kuheshimiana, kupendana na kuvumiliana tushikamane katika, hali iliyopo sasa kwa nchi yetu siyo nzuri. Si ajabu hivi sasa tunavyoongea kuna sehemu mabomu yametokea, si ajabu kuna watu wameuawa kikatili. Hii yote ni sababu watu sasa wanapoteza misingi ya kuheshimiana, upendo na kuvumiliana,” alisema Bilal kwenye Viwanja vya Karangara.
 
Awali Katibu Mkuu wa Baraza la Waislamu Tanzania, Bakwata, Sheikh Suleiman Lolela alisema waumini na wananchi wote waitumie vyema nafasi ya Uchaguzi Mkuu kuhakikisha wanachagua viongozi bora watakaoendeleza amani.
 
Kisiwani Unguja, Rais wa Zanzibar Dk Ali Mohamed Shein amewataka viongozi wa vyama vya siasa, taasisi za kijamii na madhehebu ya dini kulinda na kuheshimu msingi na malengo ya kuanzishwa Serikali ya Umoja wa Kitaifa (SUK) wakati huu wa kuelekea Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba.
 
Akiuhutubia kwenye Baraza la Eid el Fitr lililofanyika Ukumbi wa Bwawani na kuhudhuriwa pia na Makamu wa Kwanza wa Rais, Maalim Seif Sharif Hamad jana, Dk Shein alisema viongozi wa kisiasa wanapaswa kufanya siasa kwa kuzingatia misingi ya Katiba na sheria kwa madhumuni ya kuendeleza na kulinda amani na umoja wa kitaifa kwa manufaa ya Zanzibar na wananchi wake.
 
“Tunaweza kushindana bila ya kulaumiana, kukejeliana na tunaweza kushindana bila ya kudharauliana au kuhasimiana,” alisema Dk Shein kwenye shughuli hiyo iliyotaliwa na hali ya utulivu.
 
Alieleza kuwa vyama vya siasa vimeanzishwa na vipo kwa ajili ya kushindana kwa sera kwa madhumuni ya kuchochea maendeleo ya Zanzibar na siyo kugombanisha watu na kuvuruga misingi ya amani na umoja wa kitaifa.
 
Kwenye Uwanja wa Jamhuri Mjini Dodoma, sheikh wa mkoa, Ahmed Zuber aliwataka Watanzania kudumisha amani na umoja.
 
Zuber alisema dunia sasa imechafuka kutokana na uvunjifu wa amani unaochochewa na siasa chafu hivyo Watanzania bila kujali dini wala itikadi zao wanapaswa kuilinda amani iliyopo sasa.
 
“Tunahitaji utulivu. Nchi nyingi huharibikiwa kipindi kama hiki cha uchaguzi, amani hupotea kipindi hiki cha uchaguzi. Ndugu zangu Waislamu na msio Waislamu tukiichezea amani hii iliyopo sasa, tujue hakika hatuna kwa kukimbilia,” alisema.
 
Mkoani Tanga, 
 
imamu wa Msikiti wa Ibadhi, Sheikh Mohammed Said aliitaka jamii kudumisha amani na utulivu uliopo na kuacha kushabikia vyama vya siasa.
 
Sheikh huyo alisema ni wajibu wa kila mtu kutambua kuwa amani iliyopo ikitoweka ni vigumu kuirejesha na hivyo kila mmoja ahakikishe anatambua wajibu wake.
 
Alisema wakati wa uchaguzi, hutokea jamii kuhamasishana kwa mambo ya kisiasa, jambo ambalo alisema ni baya na halifai kutokea na hivyo kutaka kila mmoja kuwa mlinzi wa mwenzake.

Mkoani Lindi, Sheikh Salimu Nalinga akitoa salamu za Eid el Fitr aliwataka Waislamu kuchagua viongozi waadilifu ili kuifanya nchi kuendelea kuwa ya amani na utulivu

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement