*Wagonjwa wazidi 400
Dk. Donald Mmbando (mwenye suti) akiwa na mwakilishi wa WHO nchini, Rufalo Chatora, alipozungumza na waandishi wa habari hapo jana. |
KATIBU Mkuu wa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, Dk. Donan
Mmbando amesema wagonjwa wa kipindupindu wameongezeka katika mikoa ya Dar es
Salaam, Pwani na Morogoro tangu ulipoibuka Agosti 15, mwaka huu.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, Dk
Mmbando alisema hadi kufikia jana idadi
ya wagonjwa kutoka katika mikoa hiyo ilikuwa imefikia 452.
“Idadi ya wagonjwa wa kipindupindu imeongezeka na kufikia
452 tangu ulipoanza, hadi sasa idadi hiyo imefikia 385 kwa jiji la Dar es
Salaam huku wanane tayari walikwishapoteza maisha,” alisema.
Akifafanua hilo, Dk. Mmbando alisema katika Halmashauri ya
Manispaa ya Kinondoni wapo wagonjwa 292, Ilala 60 na Temeke wagonjwa 33.
Alisema hadi jana kulikuwa na wagonjwa 74 waliolazwa katika
kambi zilizotengwa na serikali ikiwemo Mburahati ambayo ina idadi ya wagonjwa
53, Buguruni 14 na Temeke wagonjwa saba.
Alisema katika Mkoa wa Morogoro, idadi ya wagonjwa hadi
jana ilifikia 60 na kwamba tisa kati yao waliwekwa kambini na mmoja alifariki
dunia.
“Katika mkoa wa Pwani kulikuwa na idadi ya wagonjwa saba,
wakitokea katika mji wa Kibaha ambapo
walipatikana sita na Mkuranga mmoja na baadae mmoja alifariki akiwa kwenye
Hospitali ya Rufaa ya Tumbi,” alisema Dk. Mmbando.
Alisema tayari Wizara imepokea msaada wa kiasi cha shilingi
milioni 42.26 kutoka Shirika la Afya Duniani (WHO) ambao umelenga kuisaidia
serikali kupambana na ugonjwa huo.
“Tumepokea msaada wa fedha hizo pamoja na ‘mabox’ ya dawa
1000 za kutakasa maji (Water Guard) na lita 100 za dawa aina ya lysol kutoka
kwa WHO kwa ajili ya kudhibiti ugonjwa wa kipindupindu unaozidi kuenea nchini,”
alisema Dk. Mmbando.
Alisema serikali itawapatia wananchi dawa ya ‘water guard’
ambayo ni rahisi kuitumia ambayo pia aihitaji kuchemsha maji kutokana na
kuthibitishwa kuwa haina madhara kwa binadamu.
“Lakini bado nasisitiza kuwa ni muhimu kuzingatia suala la
usafi kwa kunywa maji safi na salama, kuepuka kula chakula kilicho poa au
kuandaliwa katika mazingira yasiyo safi, kunawa mikono kwa sabuni na maji safi
kabla ya kula,” alisema Dk. Mmbando.
Alitoa rai kwamba vyombo vya usafiri vitakavyotumika kubeba
wagonjwa wenye kuharisha au kutapika vifanyiwe usafi na kutakaswa kwenye kituo
alichofikia mgonjwa kabla ya kuendelea kutoa huduma kwa mtu mwingine.
Chapisha Maoni