Recent Post


 


moja

Responsive Advertisement



MKURUGENZI wa Kampuni ya Lino International Agency, Hashim Lundenga (Pichani) amejitoa katika Kamati ya Miss Tanzania na kuunda timu nyingine ambayo itasimamia kinyang’anyiro hicho, kuanzia sasa ikiwahusisha warembo kadhaa akiwamo Jokate Mwegelo (Kidoti).

Akizungumza Dar es Salaam jana, Lundenga alisema kuwa Kamati mpya ina wajumbe 12, ikiongozwa na Mwenyekiti Juma Pinto ambaye ni Mkurugenzi wa Jambo Concept, wakati Makamu wake ni Lucas Rutta na Katibu ni Doris Mollel.

Wajumbe ni Miss Tanzania 1999 Hoyce Temu, Mohamed Bawazir, Gladyz Shao, Magdalena Munisi, Shah Ramadhani, Hamm Hashim, Khalfani Saleh na Ojambi Masaburi, wakati Jokate akiwa ni Msemaji wa Kamati hiyo. 

“Kamati iliyomaliza muda wake ilidumu kwa miaka 21, imefika wakati wale tuliokuwapo tumechoka na hivyo kutulazimu kukasimu nafasi hizi kwa wengine ili tupate mawazo mapya yatakayosaidia kuboresha kama tulivyoelekezwa na BASATA (Baraza la Sanaa la Taifa),” alisema.

Kwa upande wake, Pinto alisema: “Kamati imeanza kazi mara moja kuanzia leo (jana) baada ya kutambulishwa kwa waandishi wa habari, mashindano huenda yakafayika mwishoni mwa mwaka huu au mwanzoni mwa mwaka ujao hii ni kulingana na hali halisi kwamba tupo katika kipindi cha uchaguzi.” 

Aliongeza: “Tutaanza na changamoto zilizojitokeza mwaka jana, tutakutana na BASATA ili watupe miongozo ambayo itatufaa zaidi kusimamia na kuendesha mashindano hayo.” 

Akisisitiza katika hilo, Jokate alisema watafanya juu chini kurudisha hadhi ya mashindano hayo na kuyafanya yawe kama yale ya kimataifa.

“Tunatarajia kuamsha hisia mpya, tutatumia uzoefu wetu kuhakikisha mashindano yanakuwa bora kwa pamoja na kuwapata wawakilishi ambao watazingatia miiko,” alisema.

Mbali ya kamati hiyo ya akina Pinto, pia imeteuliwa sekretarieti itakayosimamia mashindano hayo inayoundwa na Dk Ramesh Shah, Hidan Rico, Yasson Mashaka na Deo Kapteni. 

Shindano hilo lilifungiwa kwa miaka miwili Desemba mwaka jana na BASATA kwa madai ya kukiukwa kwa taratibu, kabla ya kufunguliwa mapema mwezi huu baada ya Lundenga na timu yake kurekebisha baadhi ya kasoro zilizojitokeza.





Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement