Mtalii mmoja kutoka Japan amefariki
baada ya kuteleza na kuanguka kutoka kwenye ngazi katika jengo maarufu
la Taj Mahal nchini India.
Polisi wanasema amepoteza fahamu mara moja baada ya kuanguka na akafariki akitibiwa hospitalini.
Taj Mahal, iliyojengwa karne ya 17 na mfalme wa Mughal, Shah Jahan, baada ya kufariki dunia kwa mkewe akikusudia liwe kaburi lake, huvutia watalii karibu 12,000 kila siku.
Afisa wa polisi wa kikosi cha kulinda watalii cha mji wa Agra Sushant Gaur ameambia BBC Hindi kuwa mtalii huyo alikuwa pamoja na watu wengine watatu ajali hiyo ilipotokea.
Mwenzake mmoja alivunjika mguu, baada yao kuanguka pamoja, polisi walisema.
Ubalozi wa Japan umefahamishwa kuhusu kisa hicho na uchunguzi unafanywa.
Visa vya watu kufariki au kujidhuru wakijipiga picha wenyewe, ambazo kwa Kiingereza huitwa ‘selfie’ vimekuwa vikiripotiwa mara kwa mara.
Mwezi Mei mwaka huu, mwanamke alinusurika kifo baada yake kujipiga risasi kichwani akijipiga ‘selfie’ akiwa na bastola mjini Moscow.
Agosti, mwanamume nchini Uhispania aliuawa na fahali akijipiga picha wakati wa tamasha za kila mwaka za kukimbiza mafahali mjini Villaseca de la Sagra.
Chapisha Maoni