JESHI la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam,
linawashikilia watu watano kwa tuhuma za kutumia vibaya mitandao ya kijamii
kufanya uhalifu wa kutengeneza habari za
uongo na uzushi dhidi ya viongozi au watu maarufu.
Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Kamishna Suleimani Kova amewaeleza waandishi wa habari jijini humo jana kuwa watu hao
wamekuwa wakitumia vibaya majina ya watu maarufu hasa wanasiasa.
Aliwataja majina ya wanasiasa hao kuwa ni mgombea ubunge Jimbo la Kibamba, John Mnyika na mgombea urais wa
Chadema chini ya mwamvuli wa Ukawa, Edward Lowassa na baadhi ya wakuu wa vyombo vya
ulinzi na usalama.
Watuhumiwa hao ni Joel Lumbay (32),
Omar Suleiman wote wakazi wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), Michael
Nickson (32) mkazi wa Tegeta, Patrick Natala
na Maxmillian Msacky wakazi wa jijini Dar es Salaam.
Alisema wamekuwa wakituma jumbe
mbalimbali wakionesha viongozi hao
walikuwa wanajadili jambo fulani dhidi ya kundi au chama kingine cha siasa kwenye mitandao.
“Wana tabia ya kutengeneza ujumbe mfupi wa
maneno (SMS) kwa lugha iliyozoeleka kama ‘kuchati,’ lakini mawasiliano hayo hayapo… yanakuwa yametengenezwa
ili kutimiza malengo yao. Jambo hili ni kosa la jinai na linaweza kuchochea
chuki katika makundi ya watu,” alisema
Kova.
Alisema jeshi hilo linaendelea kuwasaka watu
wenye tania hizo wakishirikiana na Mamlaka ya
Mawasiliano Tanzania (TCRA).
“Kiongozi au mtu yeyote atakayeona ameathirika na mbinu chafu za kihalifu asisite kutoa taarifa kwa vyombo vya dola ili hatua za kisheria zichukuliwe
mara moja,” alisema.
Chanzo, MTANZANIA
Chapisha Maoni