WIZARA ya Ulinzi na Jeshi la
Kujenga Taifa (JKT) imekanusha uvumi ulioenea juu afya ya Mkuu wa Majeshi ya
Usalama na Ulinzi nchini, Jenerali Davis Mwamunyange (Pichani), ambao unadai kuwa alinusulika
kifo, kwa kile kilichodaiwa kuwekewa sumu kwenye chakula.
Kwa mujibu wa taarifa
iliyotolewa jana jijini Dar es Salaam na katibu mkuu wa Wizara ya ulinzi na
(JKT) Job Masima, ilisema kuwa, uvumi huo ulienda mbali zaidi baada ya kudai kuwa mkuu huyo wa majeshi alilazimika kulazwa
katika hospitali ya Aga Khan iliyopo jijini Nairobi, nchini Kenya.
Huku pia ikidaiwa kuwa mkuu
huyo amepelekwa nchini India kwa matibabu, jambo ambalo lilikanushwa na kusema kuwa ni
uongo wenye kutaka kuleta hofu ya usalama wa watanzania.
“Taarifa hizo ni za uongo
wenye kila dalili ya kutengenezwa kwa lengo la kuwatia hofu watanzania juu ya
usalama wa kiongozi huyu wa juu wa majeshi yetu.
“Ukweli ni kuwa mkuu wa
majeshi ya ulinzi, Jenerali Davis Mwamunyange, ni bukheri wa afya na hayupo
nchini Kenya wala India kama ilivyoenezwa kwenye mitandao ya kijamii na vyombo
vya habari,” alisema Masima.
Alisema wananchi hawapaswi
kuwa na hofu yeyote, kwani taarifa hizo ni uzushi mtupu na kwamba Mkuu huyo
aliondoka nchini Septemba 22, mwaka huu kuelekea Rome, Italia kwa ziara ya
kikazi.
“Jenerali Mwamunyange,
aliondoka nchini Septemba 22, mwaka huu, saa 10.45 jioni kwa ndege ya shirika
la ndege la Emirates kuelekea Rome, Italia kwa ziara ya kikazi, kufuatia
mwaliko wa Mkuu wa Majeshi nchi hiyo,
Jenerali Claudio Graziano,” alisema Masima.
Alisema wanapenda kuwahakikishia
wananchi kuwa Jenerali Mwamunyange, pamoja na ujumbe wake wanaendelea na ziara
hiyo kama ilivyopangwa na amesikitishwa na uvumi huo, na kwamba Wizara ya Ulinzi
imesikitishwa na uvumi huo.
“Wizara ya Ulinzi ya Jeshi la
Kujenga Taifa(JKT), imesikitishwa na tabia hii ya uzushi inayopingana na weledi
na kanuni za uandishi katika tasnia ya habari. Ni dhahiri tabia hii
inaidhalilisha tasnia ya habari na wanahabari wanaozingatia weledi nchini.,”
alisema Masima.
alikemea kuenezwa kwa taarifa za aina hiyo zisizokuwa na tija kwa taifa na
zilizolenga kuwasumbua ndugu, jamaa, marafiki na watumishi wenye mapenzi ya
dhati na Jenerali Mwamunyange, huku akiwataka wanahabari kutozitumia vibaya
taaluma yao.
“Tunawaasa, wanahabari
kutozitumia vibaya kalamu zao na uhuru walionao kwa namna yoyote isiyokuwa na
tija kwa taifa letu. Aidha, Wizara na Taasisi zake wakati wote zimekuwa tayari
kuthibitisha jambo lolote au kutoa ufafanuzi pale unapohitajika,” alisema.
Alisisitiza kuwa ni kitendo cha
kustaajabisha kuona walioanzisha uzushi huo na kuueneza hawakuwa tayari kuomba
uthibitisho wa namna yoyote, jambo linalotia shaka juu ya nia ya mtu au kikundi
kilichoanzisha uvumi huo.
Alisema Wizara ya ulinzi na Taasisi zake zitaendelea kutoa ushirikiano wa dhati kwa wanahabari
wenye nia ya dhati ya kujenga na kuiletea sifa tasnia ya habari kwa kuzingatia
weledi na kwamba uhuru wa vyombo vya
habari uwe ni uhuru wenye kuzingatia wajibu uliobainishwa katika maadili na
kanuni za tasnia hiyo.
Pia aliwataka walioanzisha na
kueneza uvumi huo kumuomba radhi Mkuu huyo kama ishara ya ustaarabu, na
kutambua kuteleza kwao na kwamba kutofanya hivyo itatofasirika kuwa ni kukiri kueneza uzushi huo na haikuwa kuteleza, bali
ilikusudiwa kwa dhamira fulani, na hivyo kushawishi hatua zaidi kuchukuliwa.
“Jeshi na Wizara zitaendelea
kushirikiana na mamlaka husika kuwabaini watu waliohusika kuutumia vibaya uhuru
wa habari na hivyo kuupotosha umma na kuleta usumbufu kwa familia ya jenerali
mwamunyange, Jeshi na Taifa kwa ujumla,” alisema Masima.
Chanzo: MTANZANIA
Chapisha Maoni