Recent Post


 


moja

Responsive Advertisement

ASILIMIA 75 ya wagonjwa 800 waliofanyiwa upasuaji mwaka huu katika Taasisi ya Tiba ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) ni watoto wadogo huku watu wazima wakiwa ni asilimia 25.

Akizungumza na waandishi wa habari jana hospitalini hapo Dar es Salaam jana, Daktari Bingwa na Mkuu wa Kitengo cha Watoto wa JKCI, Dk. Godwin Sharau, alisema hali hiyo inatokana na mfumo mbovu wa ulaji wa vyakula pindi mama anapokuwa mjamzito, kutokuhudhuria kliniki na unywaji wa maji, vyakula vilivyo na kemikali.

Pia alisema hali hiyo inatokana na mjamzito kutopata chanjo akiwa katika kipindi hicho.

“Kuna hatari ya watoto wengi zaidi kupata tatizo hili iwapo jamii haitachukua tahadhari, kwa sababu nimegundua kwamba wanawake wengi hupata ujauzito huku wakiwa hawajapanga na wenzi wao na kwa sababu hawajapanga huendelea kunywa pombe, ulaji mbovu wa vyakula pamoja na uvutaji wa sigara, vitu ambavyo huchochea tatizo hilo.

“Kitaalamu kipindi cha wiki mbili za mwanzo za ujauzito ni cha muhimu kwa kuwa viungo vya mtoto huanza kujijenga, lakini mfumo huo wa ulaji na unywaji huenda kuvuruga ukuaji wa mtoto tumboni na ndiyo maana watoto wengi wanazaliwa na ugonjwa huo,” alisema Dk. Sharau.

Alisema unywaji wa maji na vyakula vilivyoathiriwa na kemikali ambazo wakati mwingine hutiririka kutoka migodini pia husababisha mtoto kuzaliwa na tatizo.

“Kwa mfano Mwanza tuliwahi kusikia maji ya migodini yalitiririka na kuingia kwenye mito, watu wanapotumia maji yale hasa wajawazito kuna uwezekano mkubwa wa watoto kuzaliwa wakiwa na matatizo ya moyo katika eneo lile,” alisema Dk. Sharau.

Alisema iwapo mjamzito atapata chanjo maalum katika kipindi hicho kama ya kuzuia ugonjwa wa rubera hujikuta akipata mafua makali ambayo mwishowe hupelekea mtoto kuathirika.

“Nawashauri wajawazito kuhudhuria kliniki ili wafanyiwe uchunguzi mapema kujua kama mimba ipo salama ili waweze kujifungua watoto wao bila tatizo hili,” alisema.

Awali, Kaimu Mkuu wa JKCI, Profesa Mohamed Janabi, alisema hata hivyo wanajivunia kufanikisha upasuaji wa watoto hao kwa ufanisi.

“Hivi karibuni tuliwafanyia upasiaji watoto 37 na mmoja kati yao alifariki, kwetu ni mafanikio licha ya kukabiliwa na changamoto kadhaa ikiwamo uhaba wa wataalamu, damu ya kutosha pamoja na vifaa,” alisema.

Alisema hivi sasa Taasisi hiyo itakuwa ikijitegemea na ana imani watafanya kazi kwa kiwango kikubwa hali itakayoisaidia Serikali kuokoa fedha ambazo zingetumika kuwatibu wagonjwa nje ya nchi.

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement