Recent Post


 


moja

Responsive Advertisement

Kamanda wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam Simon Sirro alipozungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani) hivi karibuni

KATIKA hali ya kushangaza shehena ya matofali Tani 14.2 imesafirishwa hadi nchini Ujerumani kupitia Bandari ya Dar es Salaam badala ya shehena ya tumbaku iliyopaswa kusafirishwa kwenda nchini humo.

Matofali hayo yalifungashwa pamoja na boksi 28 za tumbaku baada ya kuibwa boksi 71 zenye thamani ya sh milioni 150.
 
Taarifa hiyo ilitolewa na Kamanda wa Jeshi la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Simon Sirro mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam alipozungumza na waandishi wa habari ofisini kwake.

Alisema tumbaku hiyo ambayo ni mali ya mfanyabiashara Ahmed Huwel (36) mkazi wa Msasani Rejent zilikuwa jumla ya boksi 99 zenye uzito wa kilo 200 kila moja ambazo alizinunua katika kiwanda cha Alliance One Tobacco Tanzania Ltd kilichoko Morogoro kwa ajili ya kuzisafirisha kwenda Ujerumani.

Alisema jeshi la polisi lilipata taarifa juu ya wizi huo kutoka kwa mfanyabiashara huyo Januari 6, mwaka huu saa nane mchana ambapo alifungua kesi ya wizi dhidi ya Mohamed Waziri mkazi wa Kigogo ambaye ndiye dereva aliyemtuma kuchukua mzigo huo kiwandani.

Alisema mfanyabiashara huyo alitambua juu ya wizi huo baada ya kuelezwa na walioko Ujerumani Januari 4 mwaka huu kwamba walipokea shehena hiyo ya matofali pamoja na boksi 28 za tumbaku.

“Huwel alieleza kwamba siku ya tukio mtuhumiwa akiwa na gari aina ya Scania T. 628 CXL yenye ‘Trailer’ T. 775 CGC alimtuma kwenda mkoani Morogoro katika kiwanda hicho kuchukua tumbaku hizo boksi 99.

“Mtuhumiwa aliondoka Morogoro kuja Dar es Salaam kuleta mzigo huo bandarini kwa ajili ya kusafirisha kwenda nchini ujerumani. 

Lakini alipofika eneo la Mabibo aliingia kwenye ‘yard’ ya kuegesha magari ya Samwel Tarimo ambapo mtuhumiwa (dereva) alishirikiana na mtoto wa mwenye yard hiyo, aitwaye Samson Tarimo... walifungua ‘seal’ ya kontena na kuiba maboksi hayo 71,” alisema Kamanda Sirro.

Alisema baada ya kupata taarifa hiyo, jeshi hilo lilianza msako mara moja ambapo dereva wa gari hilo alikamatwa na kuambatana na askari kwenda kwenye eneo la tukio ambako upekuzi ulifanyika.

Alisema katika upekuzi huo waliwakamata watuhumiwa wengine wawili ambao ni Saimon Tarimo (mtoto wa mwenye ‘yard’hiyo) na Felix Tarimo ambaye ni fundi magari mkazi wa Mbezi Tangibovu.

Alisema baada ya watuhumiwa hao kuhojiwa walikiri kufanya tukio hilo na kueleza kuwa mzigo huo ulikuwa umepelekwa mafichoni mkoani Tanga Januari 9, mwaka huu ambapo askari walifanya ufuatiliaji na kukamata maboksi 54.

“Maboksi mengine 17 yalikamatwa mkoani Kilimanjaro, Wilaya ya Rombo, eneo la Tarakea Januari 17, mwaka huu yakiwa yamefichwa kwenye nyumba moja kwa ajili ya kuvushwa kwenda Nairobi, Kenya, pia kwenye tukio hilo gari aina ya Fuso lenye namba T. 611 AKA ambalo lilikodiwa na watuhumiwa Mabula na Mushi kwa ajili ya kusafirisha mzigo huo kutoka Mabibo, Dar es Salaam kwenda Rombo-Tarakea lilikamatwa,” alisema.

Alisema hata hivyo upelelezi bado unaendelea na watuhumiwa pamoja na vielelezo ambavyo ni maboksi ya tumbaku 71, sampuli ya matofali na magari yaliyotumika kwenye wizi huo vinashikiliwa na jeshi hilo.

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement