Mke wa Rais Mama Janeth Magufuli akisalimiana kwa furaha na wakaazi wa Kituo cha Makazi ya Wazee na Watu Walemavu cha Nunge, Kigambo ni, jijini Dar es salaam |
MKE wa Rais Janeth Magufuli kwa mara
ya kwanza amefanya ziara tangu mumewe, Dk. John Magufuli alipoapishwa kushika
wazifa huo, Novemba 5, mwaka jana.
Janeth amefanya ziara hiyo leo kwa
kutembelea kituo cha Makazi ya Wazee na Watu Walemavu Wasiojiweza kijulikanacho
kwa jina la Nunge kilichoko huko Kigamboni.
Akiwa ameambatana na Mkuu wa Wilaya
ya Temeke Sophia Mjema, amekabidhi zawadi mbalimbali kwa wazee wa kambi hiyo.
“Zawadi tuliyoileta ni ndogo
na haiwezi kumaliza matatizo yote mliyonayo. Lakini ni matumaini yangu
kuwa zawadi hii inaweza kuwa chachu ya kuhamasisha hamasa ya watu na vikundi
vingine kujitoa kusaidia watu wasiojiweza.
"Ni imani yangu kuwa
endapo watu wote tutajitoa kwa dhati tutaweza kuwahudumia wazee na
watu wasiojiweza na hivyo kuwapunguzia makali ya maisha . Tukumbuke
‘kutoa ni moyo na si utajiri’ na kwamba “sisi sote ni wazee na walemavu
watarajiwa”.
Akikabidhi zawadi hizo |
“Na kwa kutambua hilo , mimi
na wenzangu niliombatana nao tumeamua kutoa zawadi yetu ndogo
kwenu. Zawadi hiyo inajumuisha vitu vifuatavyo mchele kilo 3000, unga
kilo 3000 na maharage kilo 1200. Kulingana na idadi yenu niliyopewa kila mmoja
atapewa kilo 25 za mchele, kilo 25 za unga na kilo 10 za maharage.
“Nawaombeni mniruhusu pia kuchukua
nafasi hii kuwasilisha kwenu salamu nyingi kutoka kwa Mhe. Dkt. John Pombe
Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
"Ameniomba niwaarifu kuwa yupo
pamoja nayi na kwamba Serikali itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali
katika kuhakikisha wazee na watu wasiojiweza wanapata huduma zote muhimu kwa
kadri ya uwezo wake,” alisisitiza Mama Magufuli.
Mama Magufuli aliongeza kwamba wazee
na watu wasiojiweza wanahitaji upendo, kuthaminiwa nakusaidiwa.
Alisema hata hivyo Serikali pekee
haiwezi kumaliza matatizo yote yanayowakabili na wazee na watu wasiojiweza.
“Hivyo nazihamasisha taasisi za
Serikali na zisizo za Serikali kushirikiana na Serikali kutatua changamoto
mbalimbali zinazozikabili Kituo cha Makazi ya Wazee na Watu Walemavu Wasiojiweza
kijulikanacho kwa jina la Nunge,viwemo vingine. Alisema vituo
hivyo jumla vipo 17, katika maeneo mbalimbali nchini.
Aliupongeza uongozi na watumishi
wote wa kituo hicho na vituo vingine nchini kwa kazi kubwa wanayoifanya licha
ya kukabiliwa na changamoto kadhaa.
Alizitaja baadhi ya changamoto
zinazokabili vituo hivyo ni uchakavu wa miundombinu, uhaba wa rasilimali
fedha na watu, pamoja na maslahi duni ya watoa huduma, upungufu wa vitendea
kazi na huduma za jamii, pamoja na uvamizi wa eneo la kituo.
Aidha Mama Magufuli alimwomba Mkuu
wa Wilaya ya Temeke, Sophia Mjema kulishughulikia taizo la uvamizi wa eneo hilo
na kulitafutia ufumbuzi.
Mke wa Rais Mama Janeth Magufuli akioneshwa maeneo mbalimbali na Bw. Ojuku Mgedzi, Mkuu wa Kituo |
Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya
Temeke , Sophia Mjema alimtaka kila mwananchi kutambua kwamba bila wazee hakuna
tutakachoweza kufanya hivyo ni muhimu kuwa enzi na kuwasaidia wazee walioko
majumbani na mitaani.
“Tuwaenzi wazee na kuwasaidia pia
hata wale walioko mitaani tuwashauri warudi majumbani ili Serikali iweze
kuwaorozesha kwa kuwa si vizuri kukaa barabarani, Serikali ya Awamu ya
Tano ya Rais Magufuli itahakikisha inawajali wazee,” alisema.
Akiwahutubia wananchi |
Naye Mwenyekiti wa wazee wa
makazi hayo, Anthony Kikongoti alimshukuru Mama Magufuli kwa niaba ya
wenzake, kwa kuanza ziara yake ya kwanza ya kutembelea kituo hicho ,ambapo
alimwomba apeleke salamu zao kwa baba yao ambaye ni Rais Magufuli kuwa
wanasema asante.
“Huu ni mwaka wa wanyonge dini zote
tumwombee kwa pamoja ili aweze kuendelea kupunguza makali ya maisha,” alisema.
Afisa Mfawidhi wa kituo hicho,
Ojuku Mgedzi alisema wanahitaji bajeti ya kutosha ya kuendesha shughuli
mbalimbali, watumishi 42 , wakiwemo walinzi, kwa kuwa waliopo sasa ni 29
na hawatoshi.
Alisema eneo hilo lina hekari 50.8
na nusu ya eneo hilo limevamiwa.
Mgedzi alisema kituo hicho kina
idadi yawakazi 112, ambapo alimkabidhi Mama Magufuli orodha ya idadi ya
watu hao.
Chapisha Maoni