NAIBU Waziri wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhandisi
Hamad Masauni (mwenye suti) ameagiza kusimamishwa kazi mara moja askari watatu wa Jeshi la
Polisi Kikosi cha Zimamoto na Uokoaji kwa tuhuma ya wizi wa mafuta ya ndege na
mizigo ya abiria.
Amewataja askari hao kuwa ni Halfan Kisana, Mussa Mandauli
na Abias Mwanza ambao walipangiwa kuwako katika kituo cha Jeshi hilo huko
katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA).
Masauni alitoa agizo hilo jana katika kikao chake na
watendaji wa jeshi hilo kilichofanyika katika ukumbi wa VIP alipofanya ziara ya
ghafla uwanjani hapo.
“Mmenisomea ripoti yenu lakini nashangaa mmeshindwa
kunifafanulia suala la wizi wa mafuta kwamba mmekamata wezi wangapi na kiasi
gani cha mafuta yaliyoibiwa lakini ninazo taarifa kuwa baadhi ya askari wakiwamo
hao niliowataja wanadaiwa kuhusika katika wizi huo.
“Nina taarifa kwamba Kisana na mwenzake Mandauli Oktoba 7,
mwaka jana, saa mbili asubuhi wakitumia gari la mkuu wa kituo wa kikosi cha
zimamoto aina ya Landrover yenye namba ST 2948 walikamatwa katika lango la
kuingilia katika kikosi cha Jeshi la Wananchi (603 KJ) wakiwa wamepakia madumu
kumi ya lita 20 yakiwa na mafuta ya ndege,” alisema.
Alisema tukio hilo liliripotiwa katika kituo cha polisi hata
hivyo askari hao hawakuchukuliwa hatua zozote badala yake walipandishwa vyeo.
“Hii haiwezekani, nataka askari hawa wasimamishwe kazi na
uchunguzi ufanyike haraka ndani ya siku 14. Maana rubani naye ni binadamu... anakwenda
na kuweka mafuta kwenye ndege yake baadae anakuja kuiwasha na kuondoka akijua
yapo mafuta ya kutosha, kumbe yameibiwa bila yeye kujua matokeo yake ndege
inakwenda kuanguka, hatukubalini na suala hili, lazima hatua zichukuliwe dhidi yao ili iwe
fundisho kwa wengine,” alisema.
Naibu Waziri huyo aliagiza jeshi hilo pia kuwatafuta
wamiliki wenye gari namba T. 225 AWM aina ya Salun GX na gari namba T 786 AWZ
ambayo pia yanadaiwa kutumika kubeba mafuta yanayokuwa yameibiwa.
Alifafanua kuwa gari namba T786 AWZ ilikutwa ikiwa imebeba
mafuta Januari 8, mwaka huu huku lenye namba T 225 AWM ilibeba mafuta Januari 13, mwaka huu.
“Na hii yenye namba T 225 AWM nimeiona hapa uwanjani leo
(jana) nataka wahusika wote watafutwe, wahojiwe na waeleze yale madumu
yaliyokutwa kwenye magari yao walipeleka wapi mafuta na hata ikibainika kuwa wahusika
ni askari wenyewe wachukuliwe hatua.
“Kwa sababu hatuwezi kufika pahala tukawa na watu wa
usalama ambao nao ni wezi, nasikia kuna baadhi yenu hamtaki kukaguliwa suala
hilo nataka likome mara moja vinginevyo hawa wanaokataa kukaguliwa wanaweza
kutumiwa na watu kupitisha nyara za serikali zilizoibwa.
“Awali nimewaeleza kwamba mnafanya kazi nzuri ya kulinda
usalama lakini hawa wachache watatuchafua nimewataja hadharani ili wajue tunawajua
na tutawashughulikia,” alisema.
Alisema askari mwingine Abiasi Mwanza amekuwa akishirikiana
na mfanyakazi wa kampuni ya Swispot, Lucas Mwaganda kuiba mizigo ya abiria
uwanjani hapo.
“Nina taarifa kwamba Agosti 26, 2014 saa nane usiku, Mwanza
na Mwaganda walinaswa na kamera za usalama (CCTV) wakiiba mizigo ya abiria
iliyokuwa kule ‘Cargo’.
Mwaganda aliingia na kuitoa mizigo hiyo kisha
aliwasiliana na Mwanza ambaye alifika na pikipiki na kuichukua mizigo na
kuondoka nayo,” alisema.
Alisema tukio hilo liliripotiwa katika kituo cha polisi
hata hivyo Askari Mwanza alihamishwa na kupelekwa Makao Makuu ya jeshi hilo
ambako alipandishwa cheo na kuwa ‘Inspector’.
“Pamoja na hayo nataka muwasilishe ofisini kwangu ndani ya
siku 14 mikakati yenu endelevu ya namna ya kuepukana na aibu hii, na hii ni kwa
viwanja vyote vya ndege nchini.
“Na kule upande wa Idara ya Uhamiaji nimechukua ripoti yao
nakwenda kuiangalia kuona kama mapato ya visa tunayopata kama yanaendana na
idadi ya wateja wanaoingia nchini... maana tumepata taarifa kwamba kuna vijana
wanataka kupata utajiri wa haraka haraka hapa, tutachunguza suala hili,”
alisema.
Awali Kamanda wa Polisi, Kikosi cha Zimamoto JNIA, Martin Otieno
alisema wamekuwa wakikabiliana na changamoto mbalimbali uwanjani hapo ikiwamo
upungufu wa askari.
“Tumefanikiwa kupunguza uhalifu lakini bado tunakabiliwa na
changamoto ya wizi wa mafuta ya ndege na tuna upungufu wa askari 99 kwa ajili
ya kuimarisha ulinzi hapa uwanjani katika maeneo 31 tunayoyasimamia,” alisema
Naibu Waziri huyo, pia alikutana na Maofisa Wakuu wa Jeshi
hilo katika kikao chake cha ghafla alichokifanya ofisi za Makao Makuu ya Jeshi
hilo, Posta jijini Dar es Salaam mapema asubuhi.
Chapisha Maoni