MKAZI wa Mabibo jijini Dar es Salaam, Abraham Warioba
(50), amehukumiwa kutumikia kifungo cha miaka 20 jela au kulipa faini ya Sh
milioni 39 baada ya kupatikana na hatia ya kumiliki Digidigi 20 huku vibali
vyake vikiwa vimeisha muda jambo ambalo ni kinyume cha sheria.
Hukumu hiyo ilitolewa jana na Hakimu Mkazi Mwandamizi,
Juma Hassan baada ya kujilidhisha na ushahidi uliowasilishwa mahakamani hapo na
mashahidi wanne wa upande wa mashataka ambao ni Serikali.
“Mahakama inamtia hatiani mtuhumiwa kwa kumiliki
Digidigi 20 ambazo ni nyara za serikali kwa vibali vilivyoisha muda wake jambo
ambalo nikinyume cha sheria, hivyo atatumikia kifungo cha miaka 20 gerezani au
kulipa faini Sh. Milioni 39, adhabu hii itaanza mara tu baada ya kukamatwa.
“Kwani alipo ni rahisi tu kuweza kukamatwa kwakuwa
kila kitu kipo cha kumfanya akamatwe, hivyo mahakama inatoa amri akamatwe ili
iwe fundisho kwa wote wenye tabia za kumiliki nyara za serikali kinyume cha
sheria,” alisema Hakimu Hassan.
Warioba ambaye pia ni mfanyabiashara aliruka dhamana wakati
shahidi wa tatu akiwasisha ushahidi wake hivyo ataanza kutumikia adhabu hiyo
mara baada ya kukamatwa.
Kesi hiyo ilikuwa na Mawakili wawili wa serikali
ambao ni Florida Wenceslaus na Chesense Gavyole,
ambao waliiambia mahakama hiyo kuwa hakukuwa na kumbukumbu za makosa ya nyuma dhidi ya mshtakiwa na hivyo
kuiomba mahakama hiyo kutoa adhabu kali ili iwe fundisho kwa wote wenye tabia
kama hiyo ya kumiliki nyara za serikali pasi kuwa na vibali halali jambo linaloiingizia
hasara taifa.
Katika hati ya mashtaka, Warioba anadaiwa Januari 17
mwaka 2011 eneo la Pugu Kigogo Fresh, Manispaa ya Ilala jijini Dar es Salaam,
alikutwa akimiliki Digidigi 20 wenye thamani ya Sh milioni 3.9 ambao ni nyara
za serikali huku vibali vyake vya kumiliki wanyama hao vikiwa vimeisha muda
wake jambo ambalo ni kinyume cha sheria.
Chapisha Maoni