MTU mmoja aliyefahamika kwa jina la Godfrey Frank ambaye
umri wake haukuweza kupatikana amefariki dunia baada ya kuchomwa kisu na rafiki
yake aliyefahamika kwa jina Hassan Hemed (22).
Mauaji hayo yaliyotokea Mei 16 maeneo ya Mikocheni jijini
Dar es Salaam majira ya saa 2 usiku ambapo inadaiwa mtuhumiwa alimtaka marehemu
kumnunulia pombe aina ya kiroba hali iliyosababisha kutoelewana baada ya
marehemu kudai kuwa hakuwa na pesa ya kumnunulia.
Taarifa zilizoifikia gazeti hili zilidai kuwa baada ya
marehemu kumwambia mtuhumiwa wa mauaji kuwa hakuwa na pesa kwa wakati huo,
mtuhumiwa alimtaka kuweka dhamana ya viatu vyake jambo ambayo marehemu
hakukubaliana nalo ndipo mtuhumiwa huyo wa mauji akaamua kumchoma kisu maeneo ya mabegani na
kusababisha kupoteza maisha akiwa njiani kuelekea hospitali.
MTANZANIA iliwasiliana na Kamanda wa Polisi Kinondoni,
Christopher Fuime ili kuthibitisha tukio hilo alisema walipokea taarifa za
mauaji hayo majira ya saa 2 usiku na kwamba mtuhumiwa wa tukio hilo la mauaji
alidai kuwa alikuwa anamdai chenji marehemu baada ya kununua sigara.
Alisema kwa mujibu wa taarifa walizopokea, tukio hilo
linadaiwa kutokea majira ya saa 2 usiku
maeneo ya Mikocheni A jijini Dar es Salaam na kwamba bado upelelezi
unaendelea.
“Ni kweli tumepokea taarifa za tukio hilo la mauaji lakini
bado hazijaeleweka vizuri kutokana na mtuhumiwa anaonekana kama mtu asiekuwa na
utimamu kichwani na mwenzake waliegombana amefariki,” alisema.
Chapisha Maoni