Recent Post


 


moja

Responsive Advertisement
 
SERIKALI imekusudia kupeleka nchini Marekani sampuli ya damu na haja kubwa zilizochukuliwa kutoka kwa watu walioripotiwa kuugua ugonjwa usiofahamika huko mjini Dodoma.

Sampuli hizo zitapelekwa katika maabara ya Kituo cha Udhibiti wa Magonjwa cha Marekani (CDC) jijini Atlanta wakati wowote kuanzia sasa kwa uchunguzi zaidi.

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu alisema hayo jana jijini Dar es Salaam alipozungumza na waandishi wa habari ambapo alisema sampuli hizo zitakapopelekwa nchini humo wanatarajia kupata majibu yake katika kipindi kisichozidi wiki moja.

Alisema sampuli hizo zilikuwa ziwe zimekwisha safirishwa jana kwenda nchini humo lakini hadi kufikia mchana bado walikuwa hajapokea kibali.

“Mipango imekamilika, kibali bado hatujakipokea tunatarajia hadi kufikia jioni tutakuwa tumekipata na hivyo kuzisafirisha.. tunatarajia kupokea majibu yake katika kipindi kisichozidi wiki moja,” alisema.

Alisema pamoja na kusudio hilo, sampuli nyingine zikiwemo damu, haja kubwa, vinyama vya ini na chakula tayari zimepelekwa katika maabara za Mkemia Mkuu wa Serikali, Maabara ya Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA) na Maabara ya Taifa ya Magonjwa ya Binadamu na Maabara ya Hospitali ya KCMC (KCRI).

Waziri Ummy alisema sampuli hizo zimepelekwa katika maabara tofauti tofauti ili kujiridhisha kwa majibu yatakayobainika.

Alisema hadi sasa, sampuli za nafaka pekee, zimefanyiwa  uchunguzi katika maabara ya TFDA na zimeonesha kuwepo kwa uchafuzi wa sumukuvu (Aflatoxin).

“Jumla ya sampuli 13 kati ya 27 (48%) ziligundulika kuwa na uchafuzi wa sumukuvu kwa kiasi kisichokubalika kwenye nafaka kwa mujibu wa viwango vya kitaifa na zote zilitokana na mahindi. Kati ya sampuli hizo zenye sumukuvu, sampuli 12 zilitoka wilaya ya Chemba na sampuli moja ilitoka wilaya ya Kondoa.

“Sampuli saba kati ya  hizo 12 zilikuwa na kiasi kikubwa cha sumukuvu kinachozidi 150 µg/kg (micrograms per kilogram) kwa total aflatoxins, ambapo wigo wa aflatoxin B1 katika sampuli hizo ni kati ya 157.1 – 194.4 µg/kg,” alisema.

Waziri huyo alisema kiasi kama hicho kiliwahi kuhusishwa na madhara yatokanayo na sumukuvu  katika nchi za India, China na Kenya.

“Dalili za madhara ya sumukuvu  zinafanana na dalili za ugonjwa usiofahamika uliojitokeza katika Wilaya za Chemba na Kondoa. Hivyo upo uwezekano mkubwa kwamba ugonjwa huu umesababishwa na ulaji wa chakula kilichokuwa na sumukuvu na kuleta madhara,” alisema.

Alisema katika jitihada za kutambua kiini cha ugonjwa huo, Wizara imepeleka jopo la wataalam mkoani Dodoma ili waweze kushirikiana na wenzao walioko huko kufanya uchunguzi wa kina.

“Bado nasisitiza kuwa haya bado ni matokeo ya awali miongoni mwa uchunguzi unaofanywa katika kubaini kwa uhakika chanzo cha ugonjwa huu. lakini ni vyema tukaanza kufanyia kazi matokeo haya wakati tukiendelea kusibiri uchunguzi unaoendelea kufanyika katika maabara nyingine nje ya nchi,” alisema.

Alisema ugonjwa huo uliliripotiwa na Wizara Juni 19, mwaka huu katika Wilaya za Chemba na Kondoa, Mkoani Dodoma ambapo kwa wakati huo kulikuwa na jumla ya wagonjwa 21 na vifo saba.

Alisema  kumekuwako na ongezeko la wagonjwa 11 katika kipindi cha wiki moja ambapo hadi kufikia Juni 24, mwaka huu  idadi ya wagonjwa 32 huku idadi ya vifo ikiwa imebakia saba.

“Tangu ugonjwa huu ujitokeze jumla ya wagonjwa 12 wamepatiwa huduma ya matibabu katika Hospitali ya Mkoa wa Dodoma na watatu kati yao wamefariki dunia. Wagonjwa 18 wametibiwa katika Hospitali ya Kondoa, wanne kati yao wamefariki. Wagonjwa wawili hawakuwahi kulazwa hospitali.

“Hadi jana (juzi) kulikuwa na jumla ya wagonjwa tisa ambao wamelazwa katika Hospitali ya Mkoa ya Dodoma, na 14 wako katika Hospitali ya Wilaya ya Kondoa. Wagonjwa watatu waliolazwa Hospitali ya Mkoa Dodoma, na wawili waliolazwa Kondoa, bado hali zao ni tete,” alisema.

Alisema wizara ya Afya itaendelea kufanya kazi kwa ukaribu na Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi pamoja na Wizara ya Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) katika kipindi hiki cha kutambua na kudhibiti ugonjwa huu.

“Tunaendelea kutoa elimu kwa wananchi juu ya njia sahihi za uandaaji wa chakula utakaosaidia kupunguza kiasi cha sumukuvu kwenye nafaka ambazo hazijaharibika sana. Njia hizi ni pamoja na kuchambua nafaka zilizoharibika (zilizooza, kuvunjika, zilizobadilika rangi), kukoboa mahindi kabla ya kusaga au kuacha kutumia nafaka zitakazoonekana kuharibika sana,” alisema.

Alisema Serikali itaendelea kuimarisha mikakati ya kitaifa ya kupunguza uchafuzi wa sumukuvu katika vyakula, ikiwa ni pamoja na kujenga uwezo wa kupima sumukuvu katika damu na mkojo miongoni mwa taasisi za ndani ya nchi.

“Tutaendelea kutoa matibabu kwa wanachi walioathirika na Ugonjwa huu, kwenye Hospitali ya Mkoa wa Dodoma na Hospitali ya Wilaya ya Kondoa pamoja na kushirikiana na mashirika ya kimataifa kama Shirika la Afya Duniani (WHO) na Shirika la CDC katika kudhibiti ugonjwa huu,” alisema.

Naye Mganga Mkuu wa Serikali, Profesa Mohamed Bakari alisema kemikali ya sumukuvu hutokea pale ambapo vyakula hususan nafaka zinapokuwa hazijahifadhiwa vizuri.

“Nafaka zisipohifadhiwa vizuri huzalisha fangasi ambayo hutengeneza sumukuvu, kiwango cha sumukuvu kinapokuwa kikubwa husababisha madhara na athari kwenye ini, hali inayopelekea mgonjwa kutapika, kuharisha damu na nyinginezo,” alisema.

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement