Recent Post


 


moja

Responsive Advertisement


 
MANISPAA ya Kinondoni imeingia hasara ya Sh bilioni 1.7 kwa kumlipa mkandarasi kujenga barabara ya mabatini ambayo ilianza kujengwa tangu 2007 na hadi leo bado haijakamilika.

Akizungumza na waandishi wa habari jana katika barabara hiyo ambako alifanya ziara ya ukaguzi pamoja na kamati ya fedha, Meya wa Manispaa hiyo, Boniface Jacob (Chadema) alisema kutokana na hali hiyo Manispaa imewasimamisha kazi wahandisi wake waliosimamia kazi hiyo.

Alisema barabara hiyo ambayo inajengwa chini ya kampuni ya Del Monte ilipaswa kuwa imekamilika na kutumika lakini haijakamilika licha ya kuwa Manispaa tayari imekwisha tumia kiasi hicho cha fedha.

 “Nilisikia mkoa umetoa tamko kwamba kampuni hii inapaswa kusimama kufanya kazi tena nchi nzima, nikashangaa maana tumeambiwa kuwa inapaswa kuongezewa Sh milioni 700  kwa ajili ya kumalizia kazi.

“Nikaona vyema nije eneo la tukio ili nijue ukweli kuhusu mradi huu, nimebaini kile kilichoelezwa kwenye makaratasi si ukweli halisi, kwamba kampuni hii haikuhusika kupanga mchoro wa barabara hii, kazi hiyo ilitathminiwa na wahandisi wa Manispaa na kampuni ilipokea mchoro,” alisema.

Alisema kwa hali hiyo wahandisi wa Manispaa ndio wanaopaswa kuwajibika kwa makosa yaliyopelekea kubomolewa kwa barabara hiyo na kuanza kujengwa upya.

“Kwa maana hii inapaswa wakandarasi kuwa makini siasa zisije zikawaharibia kazi, naona wazi kwamba barabara za Kinondoni zinatumika kwa watu kutaka kujipatia umaarufu, leo nimeujua ukweli na tuliwatuma vyombo vya dola kuchunguza hili.

“Sitaki kutumia siasa hapa, ndio maana nikaja kuwasikiliza mnieleze ukweli, ili tumalize matatizo haya ya fedha kutumika huku barabara zikiwa hazijajengwa, sitaki kuwaachia mzigo viongozi watakaokuja baadae,” alisema.

Meya Jacob alisema pamoja na barabara hiyo ipo nyingine ya Akachube ambayo Manispaa itairudia kwa Sh bilioni 1.2 kwakuwa haijajengwa katika kiwango kinachotakiwa.

“Kama leo hii kiongozi anaagiza kampuni isimame kufanya kazi bila kueleza kwa kina sababu ya kufanya hivyo kama hizi mlizoeleza tuna kila sababu ya kuhisi kwamba pengine anaujua ukweli na anataka kumtorosha mkandarasi husika,” alisema.

Alisema ameiagiza Del Monte kumalizia kazi hiyo kwani kwa hali ilivyo inaonesha wazi kosa hilo lilikuwa la wahandisi wa Manispaa hiyo.

“Uchunguzi unaendelea dhidi yao na atakayekutwa na hatia atabeba mzigo wake. Hatutaki kuingia tena kwenye deni ambapo hivi sasa kuna mkandarasi anadai Manispaa Sh bilioni 2.1 kwa kusimamishwa bila barua maalumu,” alisema.

Naye Mkurugenzi wa Del Monte, George Lupia alisema walijenga barabara hiyo kwa mchoro na vipimo walivyopewa na wahandisi wa Manispaa hiyo katika tenda yao.

“Tuliijenga na ikakamilika kabisa... baadae tuligundua kuwa inacheza, tukachukua udongo na kuupima tukagundua kuwa eneo hili lina maji mengi, tukaandikia barua Manispaa kuwa tunairudia kwa gharama zetu wenyewe,” alisema.

Wiki iliyopita Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda alinukuliwa na vyombo vya habari kuwa ameisimamisha kazi kampuni hiyo kwa kufanya kazi chini ya kiwango.

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement