HOSPITALI ya Taifa Muhimbili (MNH) ipo
katika mchakato wa kuanza kutoa huduma ya
ubingwa wa juu wa kufanya upasuaji wa
kupandikiza sikio kwa watoto waliosumbuliwa na tatizo la usikivu.
Akizungumza na MTANZANIA jana hospitalini
hapo, Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano ya Umma na Huduma kwa Wateja Muhimbili,
Aminiel Aligaesha alisema tayari serikali imepeleka madaktari wapatao watano
nje ya nchi kwenda kupata mafunzo hayo.
“Tunatarajia kuanza kutoa huduma ya
upasuaji wa kupandikiza sikio hapa Muhimbili hivi karibuni, madaktari wetu wapo
nje ya nchi wakijifunza namna ya kufanya upasuaji huo,” alisema.
Alisema katika upasuaji huo, madaktari
watakuwa wakiweka kifaa maalumu ndani ya
sikio la mtoto mwenye tatizo la usikivu ambacho kitakuwa kinamuwezesha kusikia
vizuri.
“Muhimbili tunatarajia mapema wiki ijayo madaktari
hao kuwa wamerejea nchini, pindi watakapowasili basi tutaeleza kwa kina jinsi
upasuaji huo utakavyokuwa ukifanyika,” alisema.
Aligaesha (pichani ) alisema Muhimbili itaanzisha huduma hiyo
ili kuwezesha watoto wenye matatizo hayo kupata huduma kwa wakati.
Katika jarida la hospitali hiyo la Januari hadi April, mwaka huu
Mkuu wa Idara ya Magonjwa ya Masikio, Pua na Koo, Dk. Edwin Liyombo alinukuliwa
akisema kuanza kwa upasuaji huo kutasaidia kuokoa fedha nyingi.
“Mgonjwa mmoja akipelekwa nchini India kwa ajili ya kufanyiwa
upasuaji huu hugharimu kati ya Sh milioni 85 hadi 100 kwa hiyo matibabu haya iwapo
yatafanyika hapa nchini ni wazi kuwa tutaweza kupunguza gharama hizi kwa kiasi
kikubwa,” alisema.
Chapisha Maoni