WANAUME wenye umri wa kati ya miaka 25 hadi 35 ndiyo wanaoongoza kupata ulemavu kutokana na ajali za bodaboda, Takwimu za Taasisi ya Tiba ya Mifupa na Mishipa ya Fahamu (MOI) zimebainisha.
Kaimu Mkurugenzi wa Taasisi hiyo, Dk. Othuman Kiloloma alisema hayo jana alipozungumza na waandishi wa habari wakati wa hafla ya kupokea miguu 600 ya bandia yenye thamani ya Sh milioni 60.
Miguu hiyo imetolewa na Taasisi ya Legs 4 Afrika ya nchini Uingereza kwa lengo la kuwasaidia wagonjwa wenye mahitaji ya viungo hivyo.
"Kuna ongezeko kubwa la walemavu, takwimu zetu zinaonesha mwaka 2013
tulikuwa tukipokea wagonjwa 15 wa dharura watokanao na ajali, idadi hiyo
imeongezeka na sasa tunapokea wagonjwa kati ya 50 - 60 kwa siku,” alisema.
Dk. Kiloloma (pichani) alisema takwimu hizo
zinaonesha robo tatu ya majeruhi hao ni wale wanaotokana na ajali za pikipiki
maarufu bodaboda.
Alisema wapo wanaokatika mikono na
miguu hali iliyofanya kuongezeka kwa uhitaji wa viungo bandia.
“Gharama za utengenezaji wa viungo
hivi inategemea vipuri ambavyo hununuliwa nje ya nchi, baada ya utengenezaji
mguu mmoja hugharimu kati ya Sh milioni 3.5 hadi Sh milioni sita
kutegemeana na uzuri wake, chuma na aina ya joint iliyopo pale.
“Hakukuwa na uwiano kati ya vifaa
tulivyonavyo na vile vinavyohitajika, gharama yake ni kubwa mno na vifaa
tulikuwa tunavichukua toka nchini Ujerumani kuna gharama ya usafiri kuvitoa
kule viliko na hata kuvitoa bandarini vinapofika nchini,” alisema Dk Kiloloma.
Naye Mkurugenzi wa Taasisi ya Watoto
Kwanza, Janet Kiwia alisema msaada huo utaiwezesha MOI kutoa huduma kwa gharama
nafuu.
Chapisha Maoni